HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, April 16, 2018

MAMLAKA VIWANJA VYA NDEGE WATAKIWA KUTAFUTA MBINU MBADALA KUJIENDESHA

Na Ripota Wetu, Globu ya Jamii
WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amelitaka Baraza la wafanyakazi la Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kuwa na mbinu mbadala ili kuiwezesha mamlaka hiyo kujiendesha  pasipo kutegemea bajeti kutoka Serikali Kuu.

Pia amelitaka baraza hilo kujithamini kwanini viwanja vilivyopo hapa nchini havipo miongoni mwa viwanja 10 bora  Afrika na kuwataka  waandae  mkakati wa kuiwezesha viwanja hivyo kuingia katika ushindani wa kimataifa.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam baada ya  kuzindua  baraza la sita la wafanyakazi wa TAA, Prof.Mbarawa, aliyekuwa mgeni rasmi amesema haiwezekani viwanja vya ndege vilivyopo hapa nchini vikose uwezo binafsi wa kujiendesha wakati kuna fursa nyingi za kuipatia mamlaka hiyo mapato.

“Lazima mjiulize kwanini hadi leo kununua gari ndani ya uwanja wa ndege mnasubiri fedha kutoka Serikali kuu wakati katika viwanja hivi kuna sehemu mmepangisha watu fedha zinaenda wapi"

"Kwanini mnashindwa kununua gari la zimamoto, mnashindwa kutatua changamoto zinazowakabili wakati kuna miradi mingi msitegemee mapato tu ya viwanja vya ndege,"amesema.

Prof.Mbarawa amesema Serikali inazidi kuweka miundombinu ya viwanja vya ndege katika hali nzuri ili  TAA kufanya kazi kwa weledi na hivyo kuwataka wafanyakazi wa mamlaka hiyo kuhakikisha wanasimamia kuboresha na kutoa huduma kwa wananchi.

Kwa upande wa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAA Richard Mayongela amesema  mpaka sasa wamenunua magari sita kutoka kwenye mfuko wa TAA ili kuongeza ufanisi katika kazi za kila siku.

Amesema wamefanikiwa kupata fedha ya kujenga ukuta kwenye kiwanja cha ndege cha Mwanza ili kuzuia wananchi kupita kwenye uwanja huo.

"Leo tunazindua baraza la sita la wafanyakazi wa TAA ili kuongeza ufanisi kwenye viwanja vyetu vyote hapa nchini na asiyefanya kazi kwa ufanisi atawajibika,"amesema Mayongela.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa akizungumza jambo alipokuwa anafungua mkutano wa baraza kuu la wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) uliofanyika leo jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Richard Mayongela akizungumza mafaniko waliyoyapata pamoja na kuelezea changamoto wanazozipata wakati wa mkutano wa baraza kuu la wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) uliofanyika leo jijini Dar es Salaam.
 Katibu wa baraza anayemaliza muda wake na pia ni Kaimu  Meneja rasilimali watu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) akizungumza jambo wakati wa mkutano wa sita wa mkutano wa baraza kuu la wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) uliofanyika leo jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa  alipokuwa anafungua mkutano  wa baraza kuu la wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) uliofanyika leo jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa akiwa kwenye picha ya pamoja na wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) mara baada kuzindua mkutano huo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad