HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, March 26, 2018

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII AFUNGA MAFUNZO KWA WAHITIMU WA JESHI USU KWA WAHITIMU 108 MKOANI KATAVI

 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga amewaagiza  wahifadhi wote nchini kuhakikisha kuwa hakuna misitu inayoendelea kuharibiwa  ikiwa ni pamoja na kuimarisha utoaji wa elimu kwa wananchi wanaozunguka misitu ya hifadhi ili wasiweze kukata miti ovyo kwa ajili ya makazi na shughuli za kilimo
  
Ametoa agizo hilo Machi 24, 2018 katika Wilaya ya Mlele Mkoani Katavi wakati akifunga mafunzo ya kwanza kwa Wakala ya Huduma za Misitu (TFS)  ya mabadiliko ya kuelekea mfumo wa Jeshi Usu kwa Maafisa na viongozi  108 wa TFS na  Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro.
“Misitu yetu inaendelea kuharibiwa kutokana na baadhi ya watu kuendesha shughuli za kibinadamu katika  maeneo ya hifadhi kama vile uchimbaji madini usiozingati taratibu, uchomaji misitu kwa ajili ya kuandaa mashamba pamoja na kilimo cha kuhama hama.’’Kazi ya ulinzi wa rasilimali zetu za asili ni yetu na tusikubali hali hii iweze kuendelea,,” alisema Waziri Hasunga 
Aidha, alitoa wito kwa wananchi wote kuendelea kuheshimu Sheria za nchi na kuacha kufanya shughuli za kibinadamu kwenye maeneo ya hifadhi ikiwemo kuingiza mifugo, kuanzisha kilimo, makazi na ukataji wa miti kwa ajili ya kuchoma mkaa na matumizi mengineyo.
Awali akizungumzia mafunzo hayo alisema, lengo ni kubadilisha utendaji katika sekta ya uhifadhi kutoka ule wa kiraia kwenda wa jeshi usu ambao utaongeza nidhamu, uwajibikaji, uadilifu na maadili kwa watumishi wote wa sekta hiyo ili waweze kusimamia ipasavyo uhifadhi endelevu wa maliasili za taifa.
Alisema katika kuelekea mfumo huo, Jeshi hilo litakuwa moja hali itakayosaidia watumishi wote kuzungumza lugha moja bila kujali kada anayoitumikia. Sheria ya Wanyamapori namba 5 ya mwaka 2009 inampa Waziri mamlaka ya kuunda Jeshi Usu. 
Alisema mfumo huo wa Jeshi Usu baada ya mchakato wake kukamilika  utakuwa na mnyororo mmoja wa mamlaka (chain of comand) na kwamba utahusisha taasisi zote za uhifadhi zilizopo chini ya wizara yake kwenye sekta ya wanyamapori, misitu na mali kale. “Kutakuwa na utaratibu kama majeshi mengine yanavyofanya, kama unataka kupanda cheo lazima uhudhurie mafunzo mengine zaidi ya haya ” alisema.
  
Akizungumzia mafanikio ya vita dhidi ya ujangili na matunda ya mafunzo hayo alisema, “Katika siku za hivi karibuni tumepiga hatua kubwa ya kupambana na usafirishaji magogo nje ya nchi kwa kuimarisha ulinzi katika bandari  , Kwa dhati napongeza jitihada zinazofanywa na zinazoendelea kufanywa na wahifadhi, maaskari watumishi wengine na wadau wetu wote kwa ujumla ambazo zimeimarisha hali ya uhifadhi wa maliasili zetu”. 
Alisema kwa kiasi kikubwa matukio ya uharibifu wa misitu pamoja na usafirishaji wa  magogo imepungua na kwamba  hata zile bandari bubu zimethibiwa kwa kiasi kikubwa hali inayopelekea majangili kuachana na kazi hiyo ili kukimbia mikono ya sheria.
Naye, Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Lilian Matinga alimuomba Naibu Waziri huyo kuona uwezekano wa Maafisa Maliasili pamoja na maafisa nyuki wa Halmashauri zote nchini nao washirikishwe katika mafunzo hayo kwa vile wote jukumu lao ni moja ambalo ni  kulinda na kuendelea uhifadhi wa maliasili.
 Kwa upande wake Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Tutubi Mangazeni akitoa nasaha zake kwa wahitimu wa mafunzo hayo ya Jeshi Usu, aliwataka wawe mfano wa kuigwa katika kutenda kazi  uhifadhi, maadili mema na nidhamu
 Naye, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) alisema licha ya  Taasisi yake kushiriki katika mafunzo hayo, inaangalia uwezekano wa kuanza kutumia satellite  pamoja na ndege zisizo na rubani ili kupunguza gharama za kufanya doria kwa kutumia magari.
 Mhifadhi  Elizabeth Malya  ambaye ni mhitimu wa magfunzo hayo  kutoka Mamlaka ya  Hifadhi ya Ngorongoro  alisema mafunzo hayo yamewafanya wawe wazalendo zaidi kwa  kutii amri na kutekeleza maagizo ya walio juu yao.
Mafunzo hayo ya wiki nne ambayo yalianza Februari, 24 mwaka huu yalihusisha Wakurugenzi , Wakuu wa vitengo kutoka Makao  makuu ya TFS, Wakuu wa Misitu ya Hifadhi, Maafisa Wanyamapori  kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro.
Mafunzo hayo yalihusisha matumizi sahihi ya silaha, mbinu mbalimbali za kupambana na uhalifu, huduma ya kwanza, ukakamavu, sheria mbalimbali zinazosimamia maliasili, ukamataji na upekuzi wa wahalifu na jinsi ya kuwafungulia hati za mashtaka.


 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akikagua gwaride la Maafisa wa Misitu na Wanyamapori 108 kutoka Wakala wa huduma za Misitu Tanzania (TFS) na Mamlaka ya Eneo la Ngorongoro muda mfupi kabla ya kuwatunuku vyeti vya kuhitimu mafunzo ya Jeshi Usu katika kituo cha Mlele mkoani Katavi.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (wa tano kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi, Maafisa wa Misitu na Wanyamapori 108 kutoka Wakala wa huduma za Misitu Tanzania (TFS) na Mamlaka ya Eneo la Ngorongoro muda mfupi baada ya kuwatunuku vyeti vya kuhitimu mafunzo ya Jeshi Usu jana katika kituo cha Mlele mkoani Katavi. 
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (wa pili kushoto ) akimkabidhi cheti cha kuhitimu mafunzo ya jeshi Usu, Mkurugenzi wa Mipango na Matumizi Endelevu ya Rasilimali za Misitu za Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Mohamed Kilongo katika kituo cha Mlele mkoani Katavi. Wa kwanza kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Lilian Matangi, wa kwanza kulia ni Mtendaji Mkuu wa TFS, Prof, Dos Santos Silayo pamoja na Tutubi Mangazeni.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akizungumza na wahitimu wa Jeshi Usu wakati wa kuhitimisha mafunzo hayo jana mkoani Katavi.

 Baadhi ya Maafisa wa Misitu na Wanyamapori 108 kutoka Wakala wa huduma za Misitu Tanzania (TFS) na Mamlaka ya Eneo la Ngorongoro wakimsikiliza, Naibu Waziri Japhet Hasunga muda mfupi kabla ya kutunukiwa vyeti vya kuhitimu mafunzo ya Jeshi Usu jana katika kituo cha Mlele mkoani Katavi.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (katikati) akipokea salamu za Jeshi Usu wakati wa kuhitimisha mafunzo hayo.
 Baadhi ya Maafisa wa Misitu na Wanyamapori 108 kutoka Wakala wa hudum za Misitu Tanzania (TFS) na Mamlaka ya Eneo la Ngorongoro wakila kiapo muda mfupi kabla ya kutunukiwa vyeti vya kuhitimu mafunzo ya Jeshi Usu jana katika kituo cha Mlele mkoani Katavi. 
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (katikati) akiwa na baadhi ya viongozi wakifurahia ulengaji wa shabaha ulioneshwa na baadhi ya wahitimu wa mafunzo hayo jana katika kituo cha cha Mlele mkoani Katavi.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (katikati ) akiwa kwenye picha ya pamoja menejimenti ya Wakala wa hudumza za Misitu Tanzania (TFS) mara baada ya kuwatunuku vyeti vya kuhitimu mafunzo ya Jeshi Usu jana katika kituo cha Mlele mkoani Katavi. 
 Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Tutubi Mangazeni akizungumza na Maafisa wa Misitu na Wanyamapori 108 kutoka Wakala wa huduma za Misitu Tanzania (TFS) na Mamlaka ya Eneo la Ngorongoro muda mfupi kabla ya kutunukiwa vyeti vya kuhitimu mafunzo ya Jeshi Usu jana katika kituo cha Mlele mkoani Katavi.
Baadhi ya Maafisa wa Misitu na Wanyamapori 108 kutoka Wakala wa hudum za Misitu Tanzania (TFS) na Mamlaka ya Eneo la Ngorongoro wakisubili kutunukiwa vyeti vya kuhitimu mafunzo ya Jeshi Usu jana katika kituo cha Mlele mkoani Katavi

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad