HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, March 20, 2018

DC KIBAHA AZINDUA CHUO CHA VETA KUWASAIDIA VIJANA WA VIJIJINI

KATIKA kuunga mkono juhudi za Rais wa awamu ya tano Dk. John Pombe Magufuli katika kuwa na uchumi wa viwanda  hatimaye  kanisa la Mission to Unreached Area Church (MUAC) lililopo Mlandizi Wilayani Kibaha Mkoa wa Pwani limeamua kujenga chuo cha ufundi stadi (VETA) kwa lengo la kuwawezesha  vijana wanaotoka katika maeneo ya vijijini ili waweze kujifunza fani mbali mbali ambazo zitawasaidia kupata ujuzi na kuanzisha viwanda vidogovidogo na kujiajiri wao wenyewe.

Kauli hiyo ilitolewa na  Askofu mkuu  wa kanisa la Mission to Unreached Area (MUAC), Samwel Meena wakati wa sherehe za uzinduzi rasmi wa chuo hicho ambazo zimehudhuriwa na viongozi mbali mbali wa dini, serikali pamoja na wageni kutoka nchini Ujerumani ambao wanajiusisha na masuala ya kuwasaidia vijana kuwainua  kiuchumi kupitia makanisa.

Askofu huyo alibainisha  kuwa lengo kubwa la kuanzisha chuo hicho ni kutokana na kubaini kuwepo kwa wimbi kubwa la ukosefu wa ajira kwa vijana hususan wale wanaoishi vijijini na kujikuta wanashinda kutwa nzima bila ya kujishughulisha na kazi yoyote , hivyo ana imani  kuwepo kwa chuo hicho ni moja na ukombozi mkubwa ambao utaweza  kuwasaidia kuondokana na hali ngumu ya kimaisha na kuondokana na dhana ya kuwa tegemezi.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama ambaye alikuwa mgeni rasmi katika sherehe za uzinduzi huo amempongeza askofu kwa kujenga chuo hicho ambacho kitaweza kuwa ni mkombozi mkubwa katika kuleta fursa za ajira kwa vijana kupitia mafunzo ya fani mbali mbali pamoja na kuanzisha viwanda vidogo vidogo ambavyo vitaweza kuwasaidia katika kujikwamua kiuchumi.

Assumpter alisema kwamba chuo hicho kitaweza kuwaletea manufaa makubwa vijana ambao wataweza kupata faida kutokana na kufundishwa fani mbalimbali ambazo zitaweza kuwasaidia kuweza kujiajiri wao wenyewe pindi watakapomaliza masomo yao.

“Kwa kweli mimi napenda kuchukua fursa hii kwanza kumshikuru Baba Askofu kwani ameweza kufanya jambo la msingi sana kwa kuweza kuona umuhimu wa kumuunga Mkono Rais katika suala zima la uchumi wa viwanda na hawa vijana pindi wakimaliza wataweza kupata fursa ya kuweza kuanzisha viwanda vyao vidogo vidogo na kuweza kujikwamua na wimbi la umasikini,”alisema Assumpter.

Nao baadhi ya wanafunzi wa chuo hicho akiwemo Michael Adam na Rehema Deogratias walisema kwamba matarajio yao makubwa katika siku za usoni ni pindi watakapohitimu mafunzo yao ni kuweka mikakati kabambe kupitia fani zao walizosomea kwa ajili ya kuweza kufungua viwanda vidogovidogo kwa lengo la kuweza kujiajiri wao wenyewe ili kuondokana na wimbi la umasikini.

Aidha wanafunzi hao waliiomba serikali ya awamu ya tano kuweza kuwasaidia kuwawezesha katika kuwapatia mitaji mbali mbali ambayo itaweza kuwasaidia kwa kiasi kikubwa katika kufanyia shughuli  zao mbali mbali ambazo zitawasaidia  katika kuleta mabadiliko chanya ya kimaendeleo na kuondokana na tabia ya kuwa tegemezi.
 Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama akizungumza jambo wakati wa halfa ya uzinduzi rasmi wa chuo cha ufundi stadi (VETA) kilichojengwa na kanisa la Mission to Unreached Area Church (MUAC) lililopo Mlandizi Wilayani Kibaha Mkoa wa Pwani.
 Askofu mkuu wa kanisa la Mission to Unreached Area (MUAC),  Samwel Meena kulia akimpa maelezo mafupi Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama wakati wa halfa ya ufunguzi wa chuo hicho cha VETA.
Askofu mkuu wa kanisa la Mission to Unreached Area (MUAC), Samwel Meena akizungumza na waandishi wa habari kuhusu uzinduzi wa chuo hicho cha ufundi stadi amabcho imejngwa kwa ajili ya kuweza kuwasaidia vijana wanaotoka katika maeneo ya vijiji.(PICHA NA VICTOR MASANGU)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad