HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, March 8, 2018

BITEKO AIPONGEZA KAMPUNI YA MZAWA YA NYAMIGOGO

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko ameipongeza Kampuni ya Mzawa ya Nyamigogo Grand Vezir Holdings Ltd inayojishughulisha na uchenjuaji dhahabu kwa kuthubutu kuanzisha mradi huo na aliahidi kuwa Serikali itaendelea kutoa ushirikiano ili kuona manufaa zaidi yakipatikana.

Alitoa pongezi hizo Machi 6, 2018 alipofanya ziara kwenye mgodi huo uliopo Wilayani Nyang’hwale Mkoani Geita ili kujionea shughuli ziazoendelea sambamba na kuzungumza na watendaji wake.

Biteko aliitaka kampuni hiyo kuendelea kufuata maelekezo ya Serikali ikiwemo kufuata sheria, kulipa kodi na tozo mbalimbali za Serikali sanjari na kutunza takwimu za uendeshaji wa shughuli zao kwa mujibu wa matakwa ya sheria.

Mara baada ya kupokea taarifa ya mgodi huo, Biteko aliahidi kushughulikia changamoto mbalimbali zinazoukabili mgodi huo ikiwemo suala la maeneo ya uchimbaji na upatikanaji wa huduma ya nishati ya umeme.

“Suala la umeme nitalifikisha; tunahitaji kuona maendeleo. Tunahakikisha tunaandaa mazingira mazuri kwa wawekezaji wote wa ndani na nje,”  alisema Biteko.

Kuhusu suala la maeneo, Biteko alisema wenye maeneo ambayo hawayaendelezi watafutiwa leseni na maeneo hayo kugawiwa upya kwa wenye nia ya dhati ya kufanya maendeleo ikiwemo kampuni hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kampuni, Hussein Amar alimueleza Naibu Waziri Biteko mafanikio yaliyofikiwa tangu mradi huo uanze kufanya kazi Mwaka 2013 ikiwemo ajira kwa wananchi wa maeneo ya karibu na Watanzania kwa ujumla ambapo alisema mradi umeajiri wafanyakazi wapatao 60.

Amar aliongeza kuwa mradi huo unaunga mkono jitihada za maendeleo ikiwemo kuchangia ujenzi wa vyumba vya viwili vya madarasa katika Sekondari ya Izunya, ujenzi wa Zahanati, ujenzi wa Ofisi ya Mtendaji Kitongoji cha Ibalangulu na uanzishaji wa mradi wa ufugaji nyuki kwa wananchi wanaozunguka mradi.

Aidha, Amar alizungumzia changamoto mbalimbali zinazoukabili mradi huo ikiwemo ukosefu wa maeneo ya uchimbaji hasa ikizingatiwa kuwa mradi huo unafunga mitambo ya kuchenjulia dhahabu yenye uwezo wa kusaga mawe kiasi cha Tani 500 kwa Saa 24 na kwamba inahitaji maeneo ili kufanya uchimbaji utakaokidhi mahitaji ya uendeshaji wa mitambo hiyo.

Aliomba kusogezewa huduma ya nishati ya umeme kwakuwa gharama kubwa inatumika kununulia mafuta kwa ajili ya kuzalisha umeme hasa ikizingatiwa kuwa shughuli nyingi zinazofanyika mgodini hapo zinahitaji nishati ya umeme.

Alisema endapo huduma hiyo ya nishati itapatikana, mgodi utazalisha ajira zaidi kwani uendeshaji wake utakuwa wa muda mrefu kwa kuwa na awamu nyingi (work shifts addition) na kwamba mgodi huo kwa sasa umeajiri wafanyakazi 60.

“Tunazalisha umeme wetu kwa kutumia mafuta; hii inasababisha gharama za uendeshaji kuwa kubwa. Tunaomba Serikali itusogezee huduma ya nishati ili kupunguza gharama za uendeshaji,” alisema Amar.

Naibu Waziri Biteko amekamilisha ziara yake Mkoani Geita ambapo alitembelea maeneo mbalimbali ya uchimbaji ili kujionea shughuli zinazofanyika na kuzungumza na wachimbaji kwa utatuzi wa pamoja wa changamoto mbalimbali zinazowakabili.
 Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kushoto) akikagua eneo linalojengwa mitambo ya kusagia mawe kwa ajili ya kuchenjua dhahabu katika mgodi wa Nyamigogo Grand Vezir Holdings Ltd uliopo Wilayani Nyang’hwale Mkoani Geita.
 Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati) alipofanya ziara kwenye mradi wa kuchenjua dhahabu wa Kampuni ya Nyamigogo Grand Vezir Holdings Ltd uliopo Wilayani Nyang’hwale Mkoani Geita. Kushoto ni Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Hussein Amar.
 Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kulia) akimsikiliza Mkurugenzi wa Kampuni Nyamigogo Grand Vezir Holdings Ltd Hussein Amar (kushoto) akielezea mtambo wa kuchenjulia dhahabu wakati wa ziara yake kwenye mradi wa kuchenjua dhahabu wa kampuni hiyo.
 Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati) alipofanya ziara kwenye mradi wa kuchenjua dhahabu wa Kampuni ya Nyamigogo Grand Vezir Holdings Ltd uliopo Wilayani Nyang’hwale Mkoani Geita. Kushoto ni Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Hussein Amar.
 Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (wa pili kulia) akikagua shughuli zinazofanywa kwenye mradi wa kuchenjua dhahabu wa Kampuni ya Nyamigogo Grand Vezir Holdings Ltd uliopo Wilayani Nyang’hwale Mkoani Geita. Wa pili kushoto ni Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Hussein Amar.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati) akitembelea mradi wa kuchenjua dhahabu wa Kampuni ya Nyamigogo Grand Vezir Holdings Ltd uliopo Wilayani Nyang’hwale Mkoani Geita. Wa pili kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Nyang’hwale, Hamim Gwiyama na wa kwanza kulia ni Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Hussein Amar. 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad