HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, February 13, 2018

MAKAMU WA RAIS AFANYA MAJUMUISHO YA ZIARA YAKE MKOANI IRINGA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amewataka Viongozi wa mkoa wa Iringa kushirikiana ili kuweza Kuwasaidia wananchi.
Makamu wa Rais ameyasema hayo wakati wa kutoa majumuisho ya ziara yake ya kuhamasisha shughuli za maendeleo mkoani Iringa.

Makamu wa Rais alitembelea wilaya ya Iringa, Kilolo na Mufindi ambako kote alishiriki shughuli za kimaendeleo ikiwa kuzindua Vituo vya Afya Kising’a wilaya Iringa, Jengo la Utawala na Madarasa katika Shule ya Sekondari Kilolo, 
Pia aliweka jiwe la msingi katika Ujenzi wa Maabara na Madarasa katika shule ya sekondari Mgololo na kuweka jiwe la Msingi katika upanuzi wa Kituo cha Afya cha Ihongole kilichopo Mafinga.

Makamu wa Rais pamoja na kutembelea miradi hiyo ya kimaendeleo pia alitembelea Kiwanda cha Ivori kinachotengeneza pipi na Chocolate na alitembelea kampuni ya GBRI inayoshughulika na uzalishaji na uuzaji wa bidhaa za mboga mboga.

Katika ziara hiyo Makamu wa Rais aliwapongeza wananchi wa mkoa wa Iringa kwa mapokezi mazuri waliompa kipindi chote cha ziara .
Makamu wa Rais alisisitiza juu ya utunzaji wa vyanzo vya maji na utunzaji mazingira, Aidha Makamu wa Rais aliwataka viongozi wa mkoa huo kuwa mstari wa mbele katika kutoa elimu ya mazingira na elimu juu ya ugonjwa hatari wa ukimwi ambao unaonekana kuenea kwa kasi mkoani humo.
Makamu wa Rais aliwataka viongozi kutoa elimu ya kutosha juu ya umuhimu wa wananchi kujiunga na mfuko wa afya ya Jamii.

Makamu wa Rais alitoa rai kwa Viongozi na Wananchi kuunga mkono mradi wa kuendeleza utalii ukanda wa kusini mwa Tanzania (REGROW) aliouzindua jana kwani pamoja na kufungua fursa mkoani humo lakini pia utasaidia katika kutunza mazingira.

Mwisho Makamu wa Rais aliwaahidi kubeba changamoto zote kubwa zikiwemo za barabara na huduma za afya ambazo bado ni kilio kikubwa mkoani humo.
  Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiongoza kikao wakati wa majumuisho ya ziara yake mkoani Iringa, Wengine pichani ni Mkuu wa mkoa wa Iringa Bi. Amina Masenza (kushoto) na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Bw. Salim Abri Asas. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais).
 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza wakati wa kikao cha majumuisho ya ziara yake mkoani Iringa. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi mbalimbali mara baada ya kumaliza kikao cha majumuisho ya ziara yake mkoani Iringa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad