HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, January 26, 2018

RPC TABORA AWAOMBA WADAU KUSAIDIA UJENZI WA NYUMBA ZA MAKAZI YA POLISI.

Na Tiganya Vincent

JESHI la Polisi Mkoa wa Tabora linakabiliwa na uhaba wa nyumba za kuishi Askari wake jambo linalowafanya wengi kupanga uraini ambapo sio salama kulingana na shughuli zao.

Kauli hiyo ilitolewa jana mjini hapa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi(SACP) Wilbroad Mtafungwa wakati wa hafla fupi ya sifa na zawadi kwa askari Polisi vyeo mbalimbali mkoani humo waliotumia Jeshi hilo kwa weledi na nidhamu.

Alisema kuwa ambazo wanaishi Maaskari ni kongwe na chakavu ambapo zinahitaji ukarabati mkubwa na kujengwa mpya ambazo zitasaidia Askari waliopanga uraiani kuondoka huko na kuisha katika nyumba hizo.

SACP Mtafungwa alisema kuwa Askari wanaoishi kambini hivi sasa ni 327 na waliopo uraiani ni 853 na hivyo kufanya Askari wengi kuwa uraiani.

Kufuatia hali Kamanda huyo wa Mkoa aliwaomba wadau mbalimbali kujitokeza kusaidia Jeshi la Polisi ili liweze kupata makazi katika maeneo yao maalum ili waweze kufanyakazi kwa ufanisi wa hali ya juu zaidi.

Alisema kuwa kama wanavyochangia katika Ujenzi wa Vituo mbalimbali vya Polisi ni vema wakachangia pia ujenzi wa nyumba kwa ajili ya makazi ya Polisi ili kuondoa tatizo la ukosefu wa nyumba kwao.

Akizungumza mara baada ya kuwapa tuzo Askari wa vyeo mbalimbali waliofanya vizuri,Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri alilipongeza Jeshi hilo mkoani katika jitihada inazoendelea nazo katika kupambana na uhalifu ikiwemo mauji ya vikongwe kwa imani za kishirikina.

Alilitaka Jeshi hilo kuendelea na kazi yao waliyoanza ya kupambana na vitendo vya uhalifu kwa ajili kuifanya Tabora kuwa mahali salama na safi pa watu kuishi na kwenda kuwekeza katika sekta mbalimbali.

Aidha Mkuu wa Mkoa alitoa wito kwa raia wema kuendelea kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa mbalimbali ambazo zitasaidia kukabiliana na uhalifu mkoani humo.

Mwanri alisema kuwa ni vema namba za kutoa taarifa za uhalifu kwa Jeshi la Polisi zikaendelea kuwa wazi ili wananchi wenye taarifa ambazo ni sahihi waweze kujulisha Jeshi hilo ili liweze kuzuia.

Alisema kuwa lengo ni kutaka kuufanya Mkoa wa Tabora uwe kimbilia la wawekezaji kwa kuwa sehemu ambayo haina usalama hakuna mtu anayetaka kuwekeza fedha zake.

“Endeleeni kupambana na wahalifu wa aina zote mpaka hapo tutakapoona kuwa Mkoa wetu umekuwa na amani kama zilivyo nyumba za Ibada…na ambapo wahalifu wataogopa kuingia mkoani kwetu” alisema Mwanri.

Katika sherehe hizo jumla ya Askari 27 na raia 1 walipatiwa tuzo kwa ajili ya utumishi wao ulitukaka, unaozingatia weledi na nidhamu na hivyo kulijengea heshima Jeshi hilo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad