HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, December 20, 2017

RAIS MAGUFULI ATOA ONYO KWA WALE WANAOPOTOSHA TAKWIMU.

Na Beatrice Lyimo-MAELEZO, DODOMA
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ametoa onyo kwa wale wote wanaotoa takwimu za upotoshaji kuacha mara moja na kuzitaka mamlaka husika kuwachukulia hatua.

Rais Magufuli ametoa onyo hilo leo mjini Dodoma wakati wa uwekaji jiwe la msingi la jengo la Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Dodoma.

“Watanzania mfuate takwimu zinazotolewa na vyombo husika,ukitaka takwimu zozote nendeni kwa wataalamu na wahusika wanaotoa takwimu sahihi kwa sababu ukikosea kutoa takwimu sahihi umeichafua nchi” ameongeza Dkt. Magufuli.

Dkt Magufuli ameongeza kuwa takwimu ni muhimu katika Nyanja zote ikiwemo kusaidia kupanga mipango ya maendeleo ya nchi ambapo husaidia kuweka malengo, kupanga malengo na pia kuliwezesha taifa kujipima kiasi gani imefikia maendeleo.

Aidha,akizungumzia hali ya ukuaji wa uchumi nchini Dkt Magufuli amesema kuwa katika nusu ya mwaka huu uchumi umekuwa kwa asilimia 6.8 ambao umepelekea kuongoza kwa nchi za Afrika Mashariki na kuwa miongoni mwa nchi za Afrika ambapo uchumi wake unaokuwa kwa kasi.

Wakati huo huo, Dkt Magufuli amemtaka Waziri wa Fedha na Mipango kufuatilia Kampuni ya Airtel kujua ukweli ya kwamba Kampuni hiyo ni sehemu ya Kampuni ya TTCL.

Mbali na hayo Dkt. Magufuli ameishukuru Benki ya Dunia, Serikali ya Canada na Shirika la misaada la Uingereza (DFID) kwa misaada wanayoendelea kuipatia nchi na kuwaahidi kuwa kila senti ya msaada itakayotolewa na mashirika hayo itatumika ipasavyo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) amesema kuwa Tanzania imekuwa nchi ya pili barani Afrika baada ya Afrika Kusini katika utoaji wa Takwimu bora kati ya nchi 54 ikiwa ni tathimini ya Benki ya Dunia mwaka 2016.

“Tumeendelea kutoa mafunzo kwa wanatakwimu katika taasisi za Serikali, Idara na Wizara ili kuendana na mabadiliko katika eneo la takwimu” ameongeza Dkt. Chuwa.

Nae Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango ameongeza kuwa ujenzi wa jengo hilo ni matokeo ya agizo la uhamasishaji wa Serikali kuhamia Makao Makuu ya nchi Dodoma.

“Ujenzi wa jengo hili unagharimu shilingi Bilioni 11.6 mpaka kukamilika kwakwe na pia ujenzi umetoa ajira za muda wa wastani kwa vijana 120 kila siku huku asilimia 100 ya vifaa vinavyotumika katika jengo hili ni vifaa kutoka ndani ya nchi, ujenzi wa jengo hili unatarajiwa kumalizika mwezi Januari, 2018” amefafanua Dkt. Mpango.

Pia Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia Bella Bird ameipongeza Ofisi ya Taifa ya Takwimu kwa kuwa miongozi mwa Ofisi bora katika utoaji wa takwimu.

“Tanzania imefanya maendeleo makubwa katika uhifadhi wa takwimu, hivyo Benki ya Dunia itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Ofisi ya Takwimu ili kuweka mifumo thabiti ya kukuza uchumi wa viwanda” amefafanua Mkurugenzi huyo.

Akizungumzia kuhusu upotoshaji wa takwimu hasa kwa vyombo vya habari nchini, Mkurugenzi Idara ya Habari na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbas amevitaka vyombo vya habari na wanahabari nchini kuhakikisha wanatumia takwimu sahihi na zinazotoka katika vyombo sahihi ili kuendeleza weledi wa taaluma.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli  akihutubia  wakati wa hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi jengo la ofisi ya Taifa ya Takwimu mjini Dodoma leo Desemba 20, 2017.

PICHA NA IKULU

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad