HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, November 14, 2017

TRA YAONGEZA UFANISI WA UKUSANYAJI KODI YA MAJENGO

Serikali imesema mapato yatokanayo na kodi ya majengo yanayokusanywa na Serikali yameongezeka baada ya jukumu hilo kukabidhiwa kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ikilinganishwa na ilivyokuwa chini ya Halmashauri.

Hayo yameelezwa Bungeni mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), alipokuwa akijibu swali la msingi la Mbunge wa Bukoba Mhe. Wilfred Lwakatare (CHADEMA), aliyetaka kujua Serikali inazipa Halmashauri ushauri gani wa kitaalam wa hatua za kuchukua ili kuziba pengo la kibajeti.

Katika swali hilo Mhe. Lwakatare aliuliza kuwa Serikali haioni kuwa uamuzi wa kuipa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kukusanya kodi hiyo ya majengo ni kuzidi kuipa mzigo mkubwa ambao hawatauweza.

Dkt. Kijaji alisema kuwa baada ya makusanyo yatokanayo na kodi za majengo kuanza kukusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA katika Halmashauri za Miji, Manispaa na Majiji 30, yalipanda hadi kufikia Sh. bilioni 34.09 mwaka wa fedha  2016/2017 ikilinganishwa na Sh. bilioni 28.28 zilizokuwa zimekusanywa na Serikali za Mitaa mwaka wa fedha 2015/2016.

“Makusanyo hayo ni sawa na ongezeko la asilimia 20.6 ya makusanyo halisi yaliyopatikana kutoka Halmashauri husika kabla ya kodi hiyo kuhamishiwa TRA hali inayodhihirisha kuwa, TRA imefanya kazi nzuri katika kukusanya mapato ikilinganishwa na kiasi kilichokusanywa na Halmashauri hizo 30 katika mwaka wa fedha 2015/16.”. alisema Dkt. Kijaji.

“Katika robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2017/18 Julai hadi Septemba, TRA, ilipangiwa kukusanya kodi ya majengo ya kiasi cha Sh. Bil 11.9 na kufanikiwa kukusanya kiasi cha Sh. Bil. 13.2 ikiwa ni ufanisi wa asilimia 111”.  Aliongeza Dkt. Kijaji.

 “Hatua ya Serikali ya kukasimu jukumu la ukusanyaji wa kodi za majengo kwa TRA, haikulenga kuzinyang’anya Halmashauri vyanzo vya mapato bali ni kuimarisha ukusanyaji wake”. alisema Dkt. Kijaji.

Aliongeza kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kunakuwepo ufanisi katika ukusanyaji na matumizi ya kodi zote zinazokusanywa ndani ya Serikali na kwamba Halmashauri zote zinapata mgao wa fedha kwa kuzingatia makisio ya bajeti zao na makusanyo ya mapato yote ya Serikali.

Aidha, Dkt. Kijaji alisema kuwa Serikali inatambua kuwa kodi ya majengo imekuwa ikichangia kwa sehemu kubwa mapato ya Halmashauri za Miji, Manispaa na Majiji katika kutekeleza mipango na utoaji wa huduma na maendeleo kwa wananchi.

Katika swali la nyongeza Mhe. Lwakatare alihoji kwa nini Serikali isichukue maoni yake ya baadhi ya majengo makubwa yatozwe kodi na TRA na yale madogo yatozwe kodi na Halmashauri kwa kuwa kumekuwa na changamoto kwa TRA katika ukusanyaji wa kodi hiyo na kuwatumia Maafisa Watendaji wa Kata katika kukusanya kodi hizo ambao wameajiriwa na Halmashauri.

Akijibu swali la nyongeza Dkt. Kijaji amesema kuwa Serikali na Bunge lilipitisha sheria ya fedha kwamba kodi ya majengo ikusanywe na TRA kwa lengo la kuimarisha ufanisi wake katika ukusanyaji na matumizi.

“Serikali itaendelea kusimamia sheria hiyo na kuhakikisha lengo la kuchukua kodi hiyo linafanikiwa na wananchi wanapata huduma stahiki”. aliongeza Dkt. Kijaji.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad