HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, November 17, 2017

SERIKALI YADHAMIRIA KUIMARISHA KAMPUNI YA TTCL

SERIKALI ya Tanzania chini ya Rais Dk. John Pombe Magufuli, imedhamiria kuiimarisha Kampuni ya Simu nchini (TTCL) iIi iweze kuingia kwenye ushindani wa kibiashara dhidi ya makampuni mengine ya simu.
Hayo yamesemwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa shirika hilo, Waziri Kindamba alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Makao Makuu ya TTCL jijini Dar es Salaam.
Kindamba alisema hayo kufuatia Novemba 14, mwaka huu, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kujadili na kupitisha miswada ya mapendekezo ya mabadiliko ya sheria yanayofuta sheria iliyounda Kampuni ya Simu ya TTCL (Tanzania Telecomunication Company, Incoporation Act 2002) na kutunga sheria inayounda Shirika la Mawasiliano Tanzania (Tanzania Telecommunication Corporation Act 2017).
Aliongeza kuwa, kujadiliwa na kupitishwa kwa muswada huu bungeni kunafuatia hatua za awali za miswada ya serikali ambapo maoni ya wananchi na wadau wa huduma za mawasiliano yalikusanywa na kuchambuliwa.
Aidha, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni zilichambua muswada huu na kuutolea mapendekezo yao, ambapo Kindamba alisema mambo muhimu yanayotajwa katika sheria hiyo mpya ni pamoja na; Kuweka utaratibu utakaowezesha TTCL kutekeleza majukumu yake kama shirika la Umma. Kuweka jukumu la ujenzi, usimamizi na uendeshaji wa miundombinu ya kimsingi ya Taifa, Kuweka mazingira ya kinga ya mali (Asset) na miundombinu muhimu ya mawasiliano ya shirika na Kuanzishwa kwa shirika na kuainisha uongozi wa shirika.
Mambo mengine ni pamoja na Kuanisha vyanzo vya mapato na mtaji wa shirika, Kuanisha sheria zingine zitakazoguswa, Sheria kutumika pande zote za muungano na Kufuta kampuni ya simu Tanzania na kuanzisha shirika la mwasiliano Tanzania.
Kindamba aliongeza kuwa, katika mapendekezo ya sheria mpya yaliyoridhiwa na Bunge, Shirika la Mawasiliano Tanzania linapewa jukumu la msingi la kutoa huduma za mawasiliano kwa Taifa na kuhakikisha kuwa huduma hizo zinatolewa kwa viwango vya juu vya ubora.
Aidha, Kindamba alisema sheria mpya inataja jukumu jingine kuwa ni kusimamia na kuendeleza miundombinu ya Ki-Mkakati ya Mawasiliano kama vile Mkonga wa Taifa wa Mawasiliano (NICTBB), Kituo Mahiri cha kutunzia kumbukumbu (National Data Centre) na miundombinu mingine itakayokuja siku za usoni.
Awali majukumu hayo yalikuwa yanafanywa na TTCL kwa niaba ya serikali bila kutajwa katika sheria. Amesema, miongoni mwa upungufu ulioonekana katika sheria ya awali ni kuwa, sheria hiyo ililenga kuwezesha mazingira ya ubia ndani ya TTCL, hitaji ambalo sasa halipo tena kutokana na TTCL kurejea mikononi mwa serikali kwa asilimia mia moja.
Kupitia utaratibu huo wa ubia, kwa kipindi cha miaka 15, TTCL ilimilikiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa asilimia 65 na Kampuni ya Bharti Airtel ya India kwa asilimia 35.
Kaimu ofisa mtendaji huyo mkuu wa TTC L amesema, ubia huo ulifikia ukomo Juni 2016 baada ya Bharti Airtel ya India kulipwa jumla ya Tsh 14.7 Bilioni na kuondoka ndani ya TTCL.
Kindamba amesema hoja mahususi ni kwamba Shirika la Mwasiliano ni chombo muhimu katika ustawi wa nchi na kuongeza kuwa sheria mpya itaongeza ufanisi na tija katika shirika hilo ili liweze kuchangia zaidi katika maendeleo ya Watanzania wote.
“TTCL ni taasisi yenye hazina kubwa ya watendaji wenye weledi na uzoefu mkubwa wa shughuli za mawasiliano hapa nchini,” alisema Kindamba na kuongeza; TTCL imeonesha weledi na uzoefu mkubwa katika kusimamia na kuendesha Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano wenye mtandao wa takriban kilomita elfu saba na mia nne nchi nzima.
Aidha, Kindamba amesema TTCL inasimamia na kuendesha kwa ufanisi mkubwa kituo mahiri cha kuhifadhi kumbukumbu (National Data Centre) kinachohudumia taasisi 28, taasisi 19 za serikali na taasisi 8 za sekta binafsi hadi sasa. “Makampuni yote ya mawasiliano na wadau mbalimbali wa biashara wanaotumia huduma zaTTCL wanaridhika sana na huduma inayotolewa,” alisema Kindamba na kuongeza;
“Kuhusu kuipa mtaji TTCL, serikali imeandaa mpango mkakati wa miaka mitano 2017/18-2021/2022 ambao pamoja na mambo mengine utaainisha mtaji unaohitajika na serikali ambapo serikali itatekeleza mpango huo.”
Aliongeza kuwa, kuhusu idadi ya wajumbe wa bodi kutoka Zanzibar, serikali imeridhia idadi hiyo kuongezeka kutoka mjumbe mmoja na kuwa wawili.

Kindamba amesema ieleweke kwamba mabadiliko haya ya sheria kutoka Kampuni ya Simu Tanzania kuwa Shirika la Mawasiliano Tanzania hayaathiri mikataba na makubaliano ya kibiashara yaliyofikiwa awali kati ya TTCL na wateja na wadau wa huduma zake.
Amesema madeni ambayo TTCL inadai wateja wake na ambayo TTCL inadaiwa na watoa huduma mbalimbali yapo palepale na yataendelea kufanyiwa kazi kwa mujibu wa makubaliano na mikataba ya kiabishara iliyofikiwa.

“TTCL ipo imara na thabiti zaidi kuliko ilivyokuwa awali kwa kuwa sasa inatarajia kupata mamlaka zaidi na uwezo zaidi wa kuhudumia umma,” alisema Kindamba.
Akielezea mustakabali wa ajira za wafanyakazi wa kampuni hiyo baada ya mabadiliko hayo, Kindamba amesema ajira zao ikiwa ni pamoja na mali na miuondombinu viko salama.

Kindamba amesema huduma zinazotolewa na TTCL yaani simu za mezani, simu za kiganjani, data na TTCL PESA zinaendelea kutolewa kwa ufanisi mkubwa na kuongeza kuwa huduma za Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano (NICTBB) na Kituo mahiri cha kutunzia kumbukumbu (National Data Centre) pia zinaendelea kutolewa kama kawaida na kwa weledi wa hali ya juu.
“Kilichobadilika ni sheria ya kampuni ya simu Tanzania ambayo sasa ni shirika la mawasiliano Tanzania ambapo mapendekezo haya yanasubiri idhini ya mheshimiwa rais ili kuwa sheria kamili,” amehitimisha Kindamba.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad