HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, November 27, 2017

NAIBU WAZIRI WA NISHATI AAGIZA MKANDARASI WA REA KUHAKIKISHA UMEME UNAWAKA KATA YA KISIJU NA MKAMBA.

Naibu Waziri wa Nishati Subira Mgalu akimsikiliza Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi ambaye ni Mbunge wa Mkuranga Abdallah Ulega katika kata ya Kisiju  wakati wa ziara yake ya kukagua maendeleo ya mradi wa umeme wa vijijini REA kwenye Kata ya Kisiju na Mkamba na kuagiza Mkandarasi anayesimamia mradi huo kuhakikisha Ijumaa umeme unawaka kwenye vijiji hivyo.

Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii.

NAIBU Waziri wa Nishati Subira Mgalu ameagiza mkandarasi anayesimamia Mradi wa  umeme wa vijijini REA mkoa wa Pwani kufikia Ijumaa aweze kuhakikisha nyumba 14 za Kijiji cha Kisiju ziwe tayari zimeshaingia umeme pamoja mkandarasi kuweka transfoma zilizoharibika haraka sana kwenye Kijiji cha Kizapara Mkamba.

Akiwa ameambatana na Mbunge wa Mkuranga Abdallah Ulega, Naibu Waziri Wa Nishati ameyasema hayo mbele ya wananchi wa kata ya Kisiju na Mkamba na kuahidi kuwa ifikapo siku ya Ijumaa ataenda  kuhakikisha kama kweli nyumba hizo zitakuwa zimeshaingia umeme na kuwaka.

Naibu Waziri wa Nishati amemtaka mkandarasi ahakikishe transfoma hizo mpaka siku ya Ijumaa ziwe zimeshafungwa kuanzia kesho huku akiwaagiza Shirika La Umeme Nchini Tanesco pamoja na REA kuhakikisha matatizo hayo yanamalizika.
Naibu Waziri wa Nishati Subira Mgalu akizungumza na wanakijiji wa Kisiju wakati wa ziara yake ya ukaguzi wa miundo mbinu ya mradi wa umeme wa vijijini REA na kusikiliza changamoto mbalimbali za wananchi na kumuagiza mkandarasi kuhakikisha umeme unawaka kufikia siku ya ijumaa kwa kata ya Kisiju na Mkamba.

Subira amesema kuwa, umeme huo wa REA hatua ya tatu  takribani vijini 25 vya wilaya ya Mkuranga vimeingia kwenye mradi huo na kiujumla vitakuwa vijiji 43, na serikali imedhamiria kuanzia 2017 hadi 2021 vijiji vyote 7873 vyote viwe vimepelekewa umeme.

Mbunge wa Mkuranga Ulega, amesema wananchi wa baadhi ya vijiji vya Mkuranga walikwamisha mchakato wa kupatikana kwa umeme wa REA kwa kudai fidia ya maeneo yao yaliyotakiwa kupita mradi huo.

"Umeme wa REA ambao ni wenye gharama nafuu zaidi umekwamishwa kwa kipindi kirefu na wananchi wenyewe kwani wengi wao walikuwa wanadai fidia ya maeneo yaliyotakiwa kupita mradi huo," amesema Ulega.

Ulega amesema kuwa, mradi huo wenye manufaa makubwa kwa wananchi wavijijini ulikwamishwa na wao wenyewe kwa takribani miaka miwili na kufikia wengine kuamua kulipa fidia kwa wanakijiji waliokataa mradi huo kupita kwenye maeneo yao.

Naibu waziri wa Nishati aliweza kutembelea kijiji cha Kisiju na Mkamba na kujionea namna mradi wa REA ulipofikia pamoja na kusikiliza changamoto za wananchi katika kupata umeme huo.

Takribani Bilioni 469 kwa fedha za ndani na bilioni 30 kwa fedha za nje zimetengewa kwa ajili ya Wizara ya Nishati kuhakikisha umeme unafika katika Vijiji vyote na ifikapo June 2019 kwa awamu ya kwanza vijiji takribani 3559 vitakuwa vimeshapata umeme wa uhakika
 Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi na Mbunge wa Mkuranga Abdallah Ulega akisalimiana na wananchi wa kata ya Kisiju wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Nishati Subira Mgalu.
 Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi na Mbunge wa Mkranga Abdallah Ulega akizungumza na wanakijiji wa Kiparaza kata ya Mkamba wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Nishati Subira Mgalu ya ukaguzi wa mradi wa umeme vijijini REA kwenye kata za Kisiju na Mkamba.

Naibu waziri wa Nishati Subira Mgula akiwa ameambatana na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi na Mbunge wa Mkuranga Abdalaah Ulega wakati wa ziara ya ukaguzi wa miundo mbinu ya mradi wa umeme wa vijijini REA  katika kata za Kisiju na Mkamba. Picha zote na Emmanuel Masaka.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad