HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, November 17, 2017

MUHIMBILI YAADHIMISHA SIKU YA MTOTO NJITI DUNIANI

  Kaimu Mkuurugenzi wa Kinga katika Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Janneth Mghamba akizungumza kwenye maadhimisho ya mtoto Njiti Duniani ambayo huadhimishwa Novemba 17 kila mwaka. Kushoto ni Mkurugenzi wa Tiba Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dkt. Hedwiga Swai.
  Mkurugenzi wa Tiba Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dkt. Hedwiga Swai akizungumza na kinamama pamoja na wataalamu wengine wa afya katika siku ya mtoto njiti duniani. Kulia ni Kaimu Mkuurugenzi wa Kinga katika Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Janneth Mghamba, Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Afya ya Uzazi na Mtoto katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dkt. Felix Bundara na Kushoto ni Mkuu wa Idara ya Watoto, Dkt. Merry Charles.
 Baadhi ya kinamama wenye watoto njiti wakiwa kwenye maadhimisho hayo leo Muhimbili. 
 aktari Bingwa wa Watoto, Dkt Agustino Massawe akiweka saini kuthibitisha kuukoa maisha ya watoto njiti.

Serikali imesema imeweka mikakati endeleveu  ya kupunguza vifo vya watoto njiti kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya afya nchini.

Kauli hiyo imetolewa leo na Mkurugenzi wa Huduma za Kinga katika Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Neema Rusibamayila katika Siku ya Kimataifa ya Watoto Njiti ambayo huadhimishwa kila mwaka Novemba 17.

“Tanzania inakabiliwa na tatizo kubwa la vifo vya watoto wachanga chini ya mwezi mmoja hivyo kutokana na hali hii tunapaswa kudhibiti vifo kwa watoto wachanga,” alisema  Dkt. Rusibamayila.

Alisema takwimu zinaonyesha asilimia 13 hadi 17 ya watoto wote wanaozaliwa Tanzania ni njiti na kwamba kutokana na hali hiyo Serikali kupitia Wizara ya Afya, imekuwa ikiratibu progamu mbalimbali   za kupunguza  vifo vya watoto wachanga na wa chini ya miaka mitano.

Mkurugenzi huyo alisema moja ya program hizo ni kumsaidia mtoto kupumua baada ya kuzaliwa, kupanua huduma za watoto wachanga kwa kujenga wodi za watoto wachanga katika hospitali za manispaa na wilaya pamoja na kutoa mafunzo kwa wa hudumu wa afya jinsi ya ya kuhudumia watoto wachanga.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Profesa Lawrence Museru alisema kuwa hospitali hiyo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali inaendelea kutoa kutoa mafunzo ya muda mfupi na mrefu kwa wauguzi na madaktari wa kitengo cha watoto wachanga ili kuongeza ufanisi wa kazi.
“Pia tumeongeza wodi mpya ya watoto wachanga na kukarabati wodi ya za zamani ili kutoa huduma bora kwa watoto wengi zaidi. Sambamba na kuongeza wodi nyingine, pia tunatarajia kuzindua wodi maalumu ya watoto wachanga mahututi (NICU) katika maadhimisho haya. Ili kutapunguza msongamano wodini,” alisema Profesa Museru.

Profesa Museru alisema hospitali imepiga hatua kubwa katika kuboresha huduma kwa watoto wachanga kama vile kuongeza vifaa tiba katika kitengo cha watoto wachanga zikiwamo mashine za kusaidia watoto kupumua, dawa ya kukomaza mapafu kwa watoto njiti.

“Katika kuadhimisha siku hii muhimu kwa watoto, Hospitali ya Taifa Muhimbili inajivunia kuwa na wodi maalumu yenye wauguzi waliobobea kwenye kutoa huduma na mafunzo kwa kina mama wenye watoto njiti wenye uzito wa kuanzia gramu 500 kwa njia ya Kangaroo mother care. Nina imani kuwa wamama wote wanaolazwa wodi ya Kangaroo ni walimu na mabalozi wazuri kwa wa mama wenzao,” alisema Profesa Museru.

Profesa Museru Muhimbili imefanikiwa kwa asilimia kubwa kupunguza vifo vya watoto wachanga kutoka asilimia 19.8 mwaka 2015/2016 hadi asilimia 7.4 mwaka 2016/17.

“Idadiya watoto waliolazwa kwenye wodi ya Kangaroo walikuwa kati ya gramu 500 na kilo 1.5 na idadi kubwa ya watoto waliotunzwa katika wodi ya Kangaroo waliofanikiwa kutoka wodini na uzito wa kilo 1.6 hadi 1.7 ambayo ni sawa na asilimia 99.5 ya watoto wote waliolazwa wodi ya kangaroo.

Alisema changamoto ni upungufu wa vifaa tiba, gharama kubwa ya kununua dawa za kukomaza mapafu na idadi ndogo ya watoa huduma.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad