Mkuu wa kitengo cha Uwezeshaji na Utawala Bora wa Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Danford Sango akitoa neno la ukaribisho kwa washiriki wa warsha ya siku tatu ya uwezeshaji wa maandiko bora ya utoaji ruzuku iliyoandaliwa na ESRF kwa ufadhili wa Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Maendeleo (IDRC) kupitia Taasisi ya Kimataifa ya Wanazuoni (Think Tank Initiatives-TTI) na kumalizika mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.
Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF) imewezesha warsha ya siku 3 kuwajengea uwezo watafiti wa ndani waweze kuandika andiko bora la kuombea fedha kwa ajili ya tafiti.
Warsha hiyo iliyofadhiliwa na Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Maendeleo (International Development Research Centre-IDRC) kupitia Jukwaa la Wanazuoni Wabobezi (Think Tank Initiatives), ilifanyika makao makuu ya ESRF, Dar es salaam.
Akizungumza Jijini hapa, Mtalaamu Mwandamizi wa Programu ya Think Tank Initiatives anayeshughulikia Sera za Uchumi, Dkt. John Okidi kutoka (IDRC), amesema kwamba watafiti kutoka nchini za Senegali, Tanzania, Uganda, Ghana na Kenya walikutana kwa siku tatu kujadili na kubadilishana mawazo namna ya kujenga uwezo katika kuandika maandiko thabiti ya kuomba fedha kutoka mashirika mbalimbali ya kimataifa.
Alisema kuna umuhimu wa kufanya andiko linaloeleweka ili kuweza kushawishi watoa ruzuku kutoa fedha za utafiti ili kuharakisha mapinduzi ya viwanda nchini.
“Watafiti lazima wawe mstari wa mbele katika kushawishi wanasiasa na viongozi kutegemea zaidi tafiti katika kuleta matokeo chanya kwa wananchi na kusukuma umuhimu wa kutumia tafiti katika kufanya maamuzi kwenye ngazi zote za maamuzi,” aliongeza Dkt. Okidi
Alisisitiza umuhimu wa utafiti katika utungwaji wa sera za maendeleo ya kiuchumi hususani katika kipindi hiki ambacho Tanzania inafanya mageuzi makubwa ya kuingia kwenye uchumi wa viwanda.
No comments:
Post a Comment