HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, October 11, 2017

SHIRIKA LA SAVE THE CHILDREN LAFANYA KONGAMANO LA WATOTO MKOA WA SHINYANGA


Kuelekea kilele cha siku ya mtoto wa kike ambayo hufanyika kila tarehe 11 Oktoba,Shirika la kimataifa la Save The Children limefanya kongamano la watoto mkoa wa Shinyanga kwa kuwakutanisha watoto kutoka maeneo mbalimbali mkoani humo kwa lengo la kuzungumzia masuala yanayohusu watoto wa kike.



Mgeni rasmi katika kongamano hilo lililofanyika leo Oktoba 10,2017 katika ukumbi wa ofisi ya mkuu wa mkoa wa Shinyanga,alikuwa Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Josephine Matiro.


Kauli mbiu ya Kongamano hilo ni “Tokomeza mimba za utotoni tufikie uchumi wa viwanda.


Wakizungumza katika kongamano hilo watoto hao waliiomba serikali kutenga bajeti yenye kumjenga mtoto huku wakiitaka serikali kuwachukulia hatua viongozi na watumishi wa serikali wanaoendekeza rushwa na kuwanyima haki watoto kwenye vyombo vya dola.
"Bado kuna changamoto ya wazazi,walezi,viongozi na jamii kwa ujumla katika kuwanyima haki watoto,wengine wamekuwa wakishirikiana na watu wanaonyanyasa watoto kumaliza kesi kienyeji matokeo yake vitendo vya watoto kupewa mimba vinazidi kujitokeza",walieleza watoto hao.
Aidha watoto hao walisisitiza elimu iendelee kutolewa kwa jamii kuhusu haki za watoto na wale wanaobainika kuwapa mimba watoto basi wachukuliwe hatua kali ili liwe funzo kwa watu wengine.
Hata hivyo watoto hao waliwanyoshea vidole waendesha bodaboda kwamba wamekuwa mstari wa mbele kushawishi watoto wa kike wanaosoma katika shule mbalimbali kwa kuwapa lifti na kuwanunulia chips kisha kuwapatia ujauzito.
Akifungua Kongamano hilo,Matiro aliwataka watoto wa kiume kuwa mstari wa mbele kuwahamasisha watoto wa kike kutoshawishiwa ili waweze kutimiza ndoto zao.
Katika hatua nyingine mkuu huyo wa wilaya aliwataka watoto wanaofanyiwa vitendo vya kikatili kuwa tayari kutoa ushirikiano ili wahusika waweze kuchukuliwa hatua za kisheria.
“Ili tushinde vita ya mimba za utotoni ni lazima watoto wasimame imara,waseme ukweli, kukataa kurubuniwa,lakini pia wazazi tuache tabia ya kumaliza kesi za watoto kienyeji kwani mnawanyima haki watoto wetu”,alieleza Matiro.
“Kesi nyingi zinashindwa kuendelea kutokana na baadhi ya watoto(waathirika) kutokuwa tayari kusema ukweli,inaumiza sana mtoto amebakwa na kupewa mimba lakini akiwa mahakamani anasema hamjui aliyembaka matokeo yake kesi inashindwa kuendelea”,aliongeza Matiro.
Hata hivyo aliwataka wazazi na walezi wa watoto na jamii kwa ujumla kuhakikisha wanawalinda watoto
Naye Mratibu wa Ulinzi wa mtoto na usimamizi wa haki za watoto kutoka Shirika la Save The Children Alex Enock alisema watoto walioshiriki katika kongamano hilo wanatoka kwenye maeneo ambako shirika la Save the Children linatekeleza mradi wa Ulinzi wa mtoto na usimamizi wa haki za mtoto.
"Tumewakutanisha watoto kutoka manispaa ya Shinyanga,Shinyanga Vijijini,Kishapu na Mji wa Kahama kwa lengo la kuzungumza na kujadili masuala mbalimbali yanayohusu watoto hasa watoto wa kike",alieleza Enock.
Hata hivyo alisema bado watoto wengi wa kike wameonekana kuwa chanzo cha mapato wanapoozeshwa lakini pia watoto wa kike hawapati muda wa kupumzika wala kucheza wanaporudi majumbani ukilinganisha na watoto wa kiume.
Kwa upande wake Afisa Maendeleo ya Jamii mkoa wa Shinyanga,Glory Mbia alisema mkoa wa Shinyanga unashika nafasi ya tano kwa mimba za utotoni kwa asilimia 34 ambapo mkoa wa kwanza ni Katavi (45% ,Dodoma (43%),Tabora (39%) na Mara (37%).
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza wakati wa kongamano la watoto wa kike leo Jumanne Oktoba 10,2017 katika ukumbi wa ofisi ya mkuu wa mkoa wa Shinyanga.Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog Watoto wakimsikiliza mkuu wa wilaya Mkuu wa wilaya ya Shinyanga akizungumza katika kongamano hilo ambapo aliwasisitiza watoto wa kike kujiamini na kutokubali kurubuniwa
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza katika kongamano hilo
Watoto wakimsikiliza mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Josephine Matiro Mtoto Victoria Deogratius kutoka manispaa ya Shinyanga akielezea kuhusu changamoto zinazowakabili watoto wa kike kuwa ni pamoja na wazazi kutokuwa na elimu kuhusu haki za watoto
Mratibu wa Ulinzi wa mtoto na usimamizi wa haki za watoto kutoka Shirika la Save The Children Alex Enock akielezea lengo la kongamano hilo la watoto wa kike Watoto wakiwa ukumbini
Mratibu wa Ulinzi wa mtoto na usimamizi wa haki za watoto kutoka Shirika la Save The Children Alex Enock akizungumza katika kongamano hilo
Afisa Maendeleo ya Jamii mkoa wa Shinyanga,Glory Mbia akizungumza katika kongamano
Kulia ni Meneja wa Shirika la Save the Children mkoa wa Shinyanga Benety Malima na mdau wa haki za watoto wakiangalia kitu muhimu kwenye kitabu wakati wa kongamano hilo
Watoto wakiwasilisha mada kuhusu changamoto wanazokabiliana nazo watoto wa kike
Wadau wa watoto wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea ukumbini
Venny Raymond kutoka shirika la Promising World For Women and Children na Afisa Mradi wa kutokomeza mimba za utotoni kutoka shirika la Young Women Leadership Veronica Massawe wakiwa ukumbini wakati wa kongamano hilo
Wadau wakiwa ukumbini
Watoto wakiwasilisha mada kuhusu masuala ya watoto ambapo walisema watoto wana nafasi kubwa katika kuhakikisha Tanzania inakuwa nchi ya viwanda
Uwasilishaji mada ukiendelea ambapo mtoto huyo alieleza kuhusu changamoto wanazokabiliana ikiwemo umbali kutoka nyumbani hadi shuleni ambapo njia wanakutana na vishawishi mbalimbali ikiwemo ya waendesha bodaboda
Watoto wakicheza mchezo wa igizo kuhusu masuala ndoa za utotoni
Antonio Alfred akichangia hoja wakati wa kongamano hilo
Mtoto akichangia hoja wakati wa kongamano hilo
Afisa Maendeleo ya Jamii manispaa ya Shinyanga,Sifa Amon akizungumza katika kongamano hilo. 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa haki za watoto na watoto
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa haki za watoto na watoto 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa haki za watoto na watoto
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa haki za watoto na watoto 
Picha ya pamoja
Watoto wakiwa katika picha ya pamoja

Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad