Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) ni Taasisi ya
Udhibiti wa huduma za sekta mtambuka iliyoundwa kwa Sheria EWURA, Sura
ya 414 ya Sheria za Tanzania.
Shughuli kuu za Mamlaka ni pamoja na
kudhibiti sekta za Nishati na Maji Tanzania Bara. EWURA ina wajibu wa
kuzidhibiti sekta hizi kiufundi na kiuchumi. Sekta ndogo zinazothibitiwa na
Mamlaka ni Petroli, Gesi Asilia, Umeme na Maji na Usafi wa Mazingira.
Moja ya majukumu makuu ya EWURA ni kutoa, kudurusu na kufuta eseni za
huduma mbalimbali inazozidhibiti ikiwemo leseni za Makandari wa Umeme
na wote wanaojihusisha na shughuli za utandazi na ufungaji umeme kwa
ngazi/ madaraja mbalimbali.
Mfano wa leseni ya kufunga umeme iliyotolewa na EWURA
Kwa mujibu wa kifungu cha 8(1) cha Sheria ya Umeme ya mwaka 2008, kazi
za ufungaji umeme ni shughuli inayohitaji leseni ya EWURA. Kwa
mantiki hiyo, ni kosa la jinai kuendesha shughuli za ufungaji umeme
bila kuwa na leseni halali iliyotolewa na Mamlaka ya Udhibiti wa
Huduma za Nishati na Maji (EWURA).
Hivyo basi, mtu yeyote
atakayepatikana na hatia ya kuendesha shughuli hizo bila leseni, atatozwa
faini ya shilingi za Kitanzania milioni tano, au kifungo cha miaka mitano au
adhabu zote kwa pamoja.
Katika utekelezaji wa jukumu hili, Mamlaka imebaini kupitia kaguzi
mbalimbali zinazofanywa mara kwa mara, kuwepo kwa mafundi wengi wasio
na leseni za EWURA, na wengine wanaendelea kutumia leseni mfu
zilizokuwa zikitolewa na Wizara ya Nishati na Madini, ambazo hawajazihuisha
hadi leo.
Aidha imebainika pia kuwa, upo udanganyifu unaofanyika kati ya
wenye leseni na wasio na leseni kwa kuwagongea mihuri kazi zao au
kushirikiana na wafanyakazi wa TANESCO wasio waaminifu, hata kama
inaonekana dhahiri kuna udanganyifu katika nyaraka husika.
Kwa mantiki hiyo, wito unatolewa kwa watanzania kuwa na desturi ya
kutumia mafundi umeme waliosajiliwa na wenye leseni halali zilizotolewa na
EWURA ili kuhakikisha usalama wao pamoja na wa mali zao; ikizingatiwa
kuwa wapo mafundi umeme wengi hapa nchini wasiosajiliwa na wanaofanya
kazi za umeme bila usimamizi, na wengine ni vishoka; hivyo kazi nyingi
zinafanywa chini ya viwango, na pengine kuweza kutokea ajali za moto muda
mfupi tu baada ya kutumia huduma zilizotolewa na mafundi hao.
Ni muhimu wanachi kutambua kuwa wanapaswa kutumia mafundi wenye
leseni kufanya shughuli za kufunga umeme katika makazi na nyumba zao ili
kuweza kupunguza madhara, ajali au majanga ya moto yatokanayo na
umeme; kuweza kupata fidia stahili ya bima inapotokea ajali ya moto
uliosababishwa na umeme; kujiridhisha kuwa mafundi na/au kampuni za
kusambaza umeme katika eneo husika zinazingatia viwango vya ubora
vilivyothibitishwa na TBS na kuwa wanaofanya kazi kwa mujibu wa Sheria na
kanuni za ufungaji umeme.
Kwa kutumia mafundi umeme wenye leseni, ni rahisi kufanya ufuatiliaji wa
aliyefungia umeme katika makazi endapo kutatokea tatizo lolote kutokana na
huduma iliyotolewa; na ni njia ya kushirikiana na Serikali katika kupiga vita
mafundi umeme wanaofanya kazi bila kua na leseni wala kufuata taratibu
wanaotambulika maarufu kwa jina la “VISHOKA” ambao wamekua
wakiwarubuni watu bila kujua.
Vilevile, ni jambo jema kujihusisha na mtu anayetambuliwa na Serikali kuliko
yule asiyefahamika vyema kuhusu uwezo wake katika kuendesha shughuli za
ufungaji umeme; na ni rahisi kupata mtaalam sahihi mwenye leseni yenye
daraja sawia na ukubwa na aina ya kazi inayotakiwa kufanywa; ikiwemo
kugundua hatari inayoweza kujitokeza mbeleni katika mfumo wako wa
umeme kabla haujaleta madhara na hatimaye kushugulikiwa mapema ili
kuimarisha usalama wa watu pamoja na mali.
Kiuchumi, hupunguza gharama ya kazi kwa kutumia mafundi waliosajiliwa
kwa kuwa gharama za vifaa vitakavyotumika kufunga umeme vitakadiriwa
kwa usahihi na ni rahisi kupata mtaalam sahihi mwenye leseni yenye daraja
sawia na aina ya kazi itakayofanywa.
Zipo athari nyingi zinazoweza kujitokeza kutokana na kuendelea kutumia
mafundi umeme wasiosajiliwa na wasio na leseni ambazo ni pamoja na
matumizi ya vifaa visivyokidhi viwango ambavyo mara nyingi husababisha
ajali za moto; na fundi asiye na elimu na ujuzi stahiki hawezi kutambua kwa
urahisi, hivyo kupelekea athari kubwa.
Vilevile kwa sababu ya kupunguza
gharama fundi asiye na ujuzi stahiki hutumia vifaa visivyokidhi kwa kuwa
labda bei yake ni ndogo na hali inazidi kuwa mbaya kwa aliyefungiwa
umeme.
Athari nyingine ni kutokuwa na mfumo mzuri wa kuweka kumbukumbu
kupitia usajili/Udhibiti, hatimaye mafundi hawawajibiki inapotokea ajali
inayosadikiwa kutokana na umeme, kwani ni vigumu kuwapata kwa kua
aidha hawana ajira ya kudumu au mahali (ofisi) pa kudumu.
Pia, kutumia mafundi wasiosajiliwa husababish kukosekana kwa utaratibu wa
kukagua miundombinu ya umeme katika majengo yetu; hatimaye ajali
kutokea baada ya miaka mingi kutokana na uchakavu wa mifumo ya umeme.
Vilevile kumekua na kasumba ya kulituhumu sShirika la Umeme nchini
TANESCO pale inapotokea moto uliotokana na hitilafu ya umeme ingawa
inawezekana siyo chanzo cha moto huo, kwani tatizo la umeme (electric
fault) inaweza kutokana na tatizo la kiufundi, matumizi ya vifaa visivyo na
ubora na matumizi yasiyofaa ya umeme.
Ili kuleta nidhamu katika tasnia ya utandazaji wa mifumo ya umeme,
Mamlaka inawataka mafundi wote wa umeme kuwa na leseni zinazotolewa
na EWURA, ambazo zimeboreshwa kulingana na mazingira ya sasa ya
teknolojia.
Aidha, Makampuni ya umeme yanatakiwa kuajiri mafundi wenye leseni au
kuwasaidia mafundi wao kuwa na leseni, siyo kuwa na leseni moja tu kwa
Msimamizi halafu wengine wote wasiwe nayo, ili tu waendelee kufanya kazi
kwao; kwa kuwa siyo rahisi msimamizi kufuatilia ubora wa kazi katika hatua
zote za utandazi wa umeme, maana nyaya huwa zimefunikwa na mabomba
au udongo au insulation, na athari za kazi mbaya zinaweza kutokea miaka
kadhaa baada ya kazi kufanyika.
Vilevile, Makampuni yanayotoa huduma za utandazi wa umeme yanapaswa
kuwaendeleza kiujuzi wafanyakazi mahala pa kazi na kuwasaidia
wanapohitaji kusoma ili kupata daraja za juu zaidi za utaalam ikiwa ni
pamoja na kuhakiki vyeti vya wafanyakazi wao kwani imebainika kuwa
baadhi ya waombaji wa leseni hutumia vyeti vilivyogushiwa vya elimu ya
ufundi (VETA), jambo ambalo ni kosa la jinai kutumia nyaraka zisizo halali.
Ni vyema pia vyuo vilivyoenea maeneo mengi nchini vitoe elimu ya viwango
vinayokubalika katika soko, hasa katika kipindi hiki ambacho kuna ongezeko
kubwa la majengo ya makazi, biashara na viwanda. Na kwa upande wa
mafundi wasiopata ajira za kudumu wajiunge katika vikundi
vinavyotambulika kisheria ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi bila kuvunja
sheria.
Njia bora ya udhibiti ni kwa kujidhibiti mwenyewe, hivyo kwa yeyote
anayehitaji kupata huduma za kufungiwa umeme katika makazi yake
yampasa kutumia mafundi wenye leseni ili aweze kuepuka hatari nyingi na
madhara yanayoambatana na mifumo ya umeme isiyo salama.
Ili kutekeleza majukumu na wajibu wake kwa uwazi na katika namna yenye
manufaa kwa wote, EWURA inafuata sera za Kisekta, Sheria kuu na miongozo
na kanuni mbalimbali zinazotolewa na Mamlaka. Sera na Sheria
zinazosimamia utekelezaji wa majukumu ya EWURA ni pamoja na: Sera ya
Taifa ya Nishati (2015), Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati
na Maji (2001), Sheria ya Umeme (2008), Sheria ya Petroli (2015), Sheria ya
DAWASA sura ya 273, Sheria ya Maji safi na Usafi wa Mazingira (2009);
pamoja na miongozo na kanuni mbalimbali zilizondaliwa na Mamlaka katika
kusimamia utekelezaji wa majukumu yake.
Nyingine ni Sheria zinazoanzisha Taasisi ambazo zinasimamia na kuratibu
utoaji wa huduma kwa kuzingatia viwango vilivyowekwa ambazo ni Mamlaka
ya Usimamizi wa Usalama mahali pa kazi (OSHA), Shirika la Viwango
Tanzania (TBS) na Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira (NEMC).
No comments:
Post a Comment