HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, September 11, 2017

Serikali Kuajiri Maafisa Ugani Katika Kila Kata Nchini

Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Mhe. William Ole Nasha

Na Beatrice Lyimo- MAELEZO DODOMA
Serikali  imepanga kuongeza idadi ya Maafisa Ugani wenye ujuzi katika kila Kata na Kijiji ili kuleta mapinduzi ya kilimo Nchini.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Mhe. William Ole Nasha wakati akijibu swali lililohusu mkakati wa Serikali wa kuhakikisha inafanya mapinduzi ya kilimo kwa kuwa na wataalamu wa kutosha, leo Bungeni mjini Dodoma.

Naibu Waziri huyo amesema kuwa Serikali inatambua kuwa Sekta ya Kilimo ni muhimu na ndiyo yenye kuajiri watanzania wengi hivyo mapinduzi ya kilimo yatachangiwa na uwepo wa wataalam wa kutosha wenye taaluma na ujuzi stahiki ili waweze kushauri matumizi ya teknolojia na kanuni bora za kilimo.

" Hadi kufikia mwaka 2016/2017 Serikali imeajiri maafisa ugani 8,756 sawa na asilimia 43 ya mahitaji ya maafisa ugani 20,374 katika ngazi ya Kijiji, Kata na Wilaya" amefafanua Naibu Waziri Ole Nasha.

Aidha, Naibu Waziri Ole Nasha aliongeza kuwa Serikali inaendelea kuboresha na kuwezesha vituo vya kilimo na vituo vya Rasilimali za kilimo za kata (WARCs) kwa ajili ya kufundishia teknolojia mbalimbali za kilimo.

Vilevile alisema kuwa Serikali itaendelea kutoa ushauri wa kitaalam na kuandaa miongozo na mafunzo ya huduma za ugani, ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa kazi za Ugani na kuboresha usambazaji wa teknolojia za kilimo bora kwa wakulima nchini.

Mbali na hayo Serikali inaendelea kusomesha vijana na kuwaajiri kulingana na upatikanaji wa rasilimali fedha.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad