HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, September 1, 2017

KAMISHNA WA MADINI ASHIRIKI ZOEZI LA UKAGUZI WA DHAHABU INAYOSAFIRISHWA NJE YA NCHI

Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka (katikati) na timu yake, wakiondoka ndani ya eneo la Mtambo/kiwanda cha kuchakata dhahabu katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM), baada ya kushiriki zoezi la uhakiki na ufungaji wa dhahabu inayosafirishwa nje ya nchi. Pamoja nao ni maafisa wa GGM. 

Na Veronica Simba – Geita

Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka, ameshuhudia na kushiriki katika zoezi la kuhakiki na kufunga madini ya dhahabu katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM), kabla ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi.

Kamishna Mchwampaka alishiriki zoezi hilo hivi karibuni, akiwa katika ziara ya kazi mkoani Geita kukagua shughuli mbalimbali za sekta ya madini. 

Zoezi la uhakiki na ufungaji wa dhahabu inayosafirishwa, hufanyika katika chumba maalum kijulikanacho kama gold room kilichopo mgodini na hushirikisha maafisa mbalimbali wa Serikali kutoka Jeshi la Polisi, Wizara ya Nishati na Madini na Mamlaka ya Mapato Tanzania pamoja na maafisa wa Mgodi.

Akizungumzia lengo la maafisa wa Serikali kutoka sekta husika kushiriki katika zoezi hilo; Kamishna Mchwampaka alieleza kuwa ni kwa Serikali kujiridhisha na thamani ya dhahabu inayosafirishwa ili kuhakikisha inapata mapato stahiki na kuepusha udanganyifu wowote unaoweza kujitokeza.

“Katika hili, tuko imara na makini. Ni lazima tuhakikishe kuwa Serikali inapata mapato stahiki kulingana na dhahabu inayosafirishwa. Ndiyo maana unaona maafisa wetu kutoka sekta zote muhimu wanashiriki kikamilifu katika zoezi hili.”

Aliwataka watanzania kuondoa hofu na kuiamini Serikali ya Awamu ya Tano inayowaongoza kuwa iko makini na imejipanga kusimamia kikamilifu maslahi ya wananchi.

Kamishna wa Madini yuko katika ziara ya kazi Kanda ya Ziwa kukagua shughuli mbalimbali za sekta husika.


Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka (mwenye koti), akihakiki uzito wa Mkuo wa Dhahabu, katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM) kabla ya kufungwa na kusafirishwa nje ya nchi. Wengine pichani ni baadhi ya maafisa wa Serikali na GGM.
Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka (mwenye koti-kulia), akishuhudia Mkuo wa Dhahabu wenye uzito wa kilogramu 26, ukiwekwa ndani ya mfuko maalum kabla ya kufungwa kwa ajili ya kusafirishwa nje ya nchi. Wengine pichani ni baadhi ya maafisa wa Serikali na GGM.
Afisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Anuari Fadhili akiweka ‘seal’ maalum ya Serikali kwenye Kasha lenye Mkuo wa Dhahabu baada ya ukaguzi katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM), kabla ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi. Wanaoshuhudia ni Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka (katikati) na maafisa wengine wa Serikali na GGM.
Kamishna wa Madini Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka (katikati),  akitoa maelekezo kwa maafisa wa Serikali pamoja na wale wa Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM), kuhusu zoezi la uhakiki na ufungaji dhahabu inayosafirishwa nje ya nchi.

Kasha lenye Mkuo wa Dhahabu katika Mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM), lililohakikiwa na kufungwa tayari kwa kusafirishwa nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad