HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, August 22, 2017

Viwanda 42 Zaidi Kuunganishwa Mfumo wa Gesi

Naibu Waziri wa Nishati na Madini Dk. Medard Kalemani

Na Said Ameir-MAELEZO
Serikali imesema kuwa viwanda vingine 42 vitaunganishwa na mfumo wa matumizi wa matunizi ya gesi asilia katika kipindi cha miaka miwili ili kuongeza tija tofauti viwanda 37 vya sasa ambavyo tayari vinatumia gesi hiyo.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini Dk. Medard Kalemani aliiambia Kamati ya Fedha ya Bunge jana kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa changamoto zinazokwaza zoezi la kuvipatia viwanda nishati hiyo zinatatuliwa haraka.
“Tuna gesi ya kutosha futi za ujazo trilioni 57.25 ambapo hadi sasa tunatumia wastani wa futi za ujazo milioni 70 ikiwa ni kama asilimia kumi tu hivi” alieleza Waziri Kalemani
Kwa hivyo alisema azma ya Serikali ni kuona viwanda vinatumia gesi katika uzalishaji na kubanisha kuwa Tanzania inaongoza kwa kuwa na nishati hiyo katika Afrika Mashariki. 
Waziri Kalemani aliieleza kamati hiyo kuwa hivi sasa wateja wakubwa wa gesi hiyo ni viwanda lakini Serikali ipo mbioni kutekeleza mkakati wa kusambaza gesi hiyo kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.
Katika maelezo yake kwa kamati hiyo ambayo ilitembelea kituo cha kupokelea gesi asilia huko Kinyerezi na miradi ya uzalishaji umeme kwa kutumia gesi hiyo ya Kinyerezi I na Kinyerezi II, Naibu Waziri  huyo alidokeza kuwa Serikali ina mpango wa kuanzisha kiwanda cha kusindika gesi asilia ili iweze kusafirishwa nchi za nje.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha ya Bunge Hawa Ghasia ameitaka TPDC kutayarisha mpango maalum kwa kuainisha na kutenga maeneo maalum ambayo yatawekewa miundombinu ya gesi ili uwekezaji wa viwanda uzingatie ramani hiyo.
“Tungetengeneza kanda maalum tukaziandaa kwa ajili ya viwanda kwa kuziwekea miundombinu ya gesi tofauti na sasa ambapo serikali inalazimika kuvifuata viwanda viliko kuvipelekea nishati hiyo” alishauri Mwenyekiti huyo.
Akizungumza  wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti huyo alieleza kuwa shirika hilo lina nafasi ya pekee katika kuifanya Tanzania kufikia lengo lake la kuwa nchi ya viwanda kama itatekeleza vyema miradi ya matumizi ya gesi viwandani.
Aliueleza uongozi wa TPDC na waandishi wa habari walioambatana katika ziara hiyo kuwa madhumuni ya ziara ya kamati yake katika miradi hiyo ni kuangalia utayari wa shirika hilo katika kuchangia maendeleo ya uchumi wa viwanda bila ya vikwazo.
Mwenyekiti huyo alieleza kuwa kamati yake imeridhika na kazi inayofanyika hadi sasa na kueleza matumiani ya kamati yake kuwa miradi ya Kinyerezi I na Kinyerezi II itamalizika kwa wakati na kufikia malengo yaliyowekwa. 
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TPDC Mhandisi Kapulya Musomba mpango wa shirika lake sasa ni kutekeleza programu yake ya kusambza gesi nchi nzima kwa kuanzia na mikoa ya Arusha, Mbeya, Mwanza na Tanga.
Alisema shirika lake lipo tayari kukipatia kiwanda au mwekezaji nishati hiyo katika sehemu yeyote ambayo bomba la gesi hiyo limepita na kwamba ingependeza kuona Tanzania ina viwanda vingi ili gesi yote iweze kutumika humu nchini pasi na kusafirishwa nchi za nje. 
Mapema akijibu maswali kutoka kwa wajumbe wa Kamati hiyo, Mhandisi Musomba alisema shirika lake linatumia mifumo miwili ya usalama wa bomba lenye urefu wa kilomita 551 linalosafirisha gesi kutoka Mtwara hadi eneo hilo.
Aliitaja kuwa ni mfumo unaojitegemea wa bomba hilo ambapo zinapotokea hitilafu hujizima na wataalamu hufuatilia kuelewa hitilafu iliopo na mfumo wa pili ni ulinzi shirikishi ambao wanawatumia wananchi kulinda bomba hilo.
Mbali na viwanda 37 kuunganishwa katika mfumo wa matumizi ya gesi, shirika hilo pia limeziunganisha familia 70 katika mfumo wa matumizi ya gesi hiyo katika maeneo ya Mikocheni jijini Dar es salaam.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad