HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, August 14, 2017

TUFANYE HAYA KULETA MAPINDUZI YA SOKA TANZANIA.



Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii.


Soka la nchi yetu linaenda 'halijojo' halina mtiririko wenye mwendelezo makini.Tangu kuanzishwa kwa Taifa hili ni Mara moja tu nchi yetu ilishiriki michuano mikubwa kwa ngazi ya Afrika yaani Afcon.



Ilikua mwaka 1980 ambao tulinyanyaswa sana katika uwanja wa Sululele pale Nigeria. Sululele ndio mtaa aliozaliwa msanii nguli wa Nigeria Wizkid,na anatanbulika kama mfalme wa Sululele.

Vizazi Vingi vimepita tangu mwaka 1980 hadi sasa. Na imekua kama ni suala la kawaida kila nyakati zimekuwa zikilalamikiwa. Na nyakati zikipita waliolalamikiwa kwa viwango vyao nao wanawalalamikia wale wanaocheza kwa wakati ambao waliolalamikiwa hawachezi.

Imekua kama mbio za 'relay' kila mlalamikiwa muda ukimwacha nae husubili wa kumlalamikia. Leo twaweza kuwa na kiwango kizuri tikaridhisha mashabiki lakini kesho tunakuwa kawaida.

TUFANYE HAYA KUNUSURU SOKA LETU.

Katika masuala ya utafiti kuna jambo linaitwa kukusanya taarifa za jambo la utafiti.Pia unatakiwa kufanya mapitio ya maandishi ili kujua tatizo uchunguzalo kama limewahi kuchunguzwa. Baada ya kuchunguza unatazama kufanikiwa au kutofanikiwa kwa utafiti huo.

Katika soka tinapaswa kutumia utafiti wa wenzetu walioporomoka kisoka na wakarudi vyema. Iko mifano mingi lakini tuwatazame Wajerumani na Wabelgiji.

Katika nchi ya Ujerumani baada ya kufanya vibaya katika michuano ya Ulaya mwaka 2000 walirudi katika vitalu 'grassroots' vya soka.

Wataalamu elfu moja walisambazwa nchi nzima kutafuta vipaji vya soka. Wataalamu hao wenye elimu ya ukocha waliingia miji mbali na maeneo ya chini kabisa kufanya kazi hiyo.

Maamuzi ya kuingia vitaluni kusaka vipaji ilitokana na jicho lao kuona hawana ubabe tena Ulaya.Maeneo ya Gelsenkirchen, Bremen, Colony, Munich,Hamburg, Wolfsburg, Frankfurt,Stuttgart yalifikiwa na wataalamu hao.

Uhai wa Ujerumani ulibaki katika vilabu vyao ambapo Mwaka 2001 Bayern Munich walichukua kikombe cha ubingwa wa Ulaya. Mwaka uliofuata klabu ya Bayer Leverkusen walicheza fainali dhidi ya Rael Madrid. Mwaka 2002 wakapoteza fainali dhidi ya Brazili pale Yokohama.

Nyakati hizo zote vijana kumi na mbili toka kwa wataalamu elfu moja walikua wamesambazwa katika vituo vya soka vya vilabu vyote. Ilikua ni mkakati ambao Chama cha soka na wanachama wake yaani vilabu vilikubaliana katika harakati hizo hivyo walilea vijana hao.

Mwaka 2006 walirejea kombe la dunia na kupata kichapo toka kwa Italia katika Nusu fainali palepale nyumbani kwao. Wajerumani walitawanywa akili na magoli ya Simeon Perotta na Alessandro Del Piero.

Wakiwa na vipaji katika vitalu wakaanza kuvichimoa mwaka 2008 katika Euro waliyokuja kupoteza fainali dhidi ya Hispania. Ilikua ni mwanga kwao Kwani 2010 wakavitoa vipaji hivyo na kuvitumia kombe la dunia pale Afrika kusini.

Ilikuwa ni kizazi cha akina Mesut Ozil,Thomas Muller,Manuel Nueur,Jerome Boateng,Sam Khedira,Matt Hummels, na wengineo. Hawa ndo ambao walipatikana vitaluni mwaka 2000.

Matunda ya vitalu vya mwaka 2000 vilikuja kuleta katika fainali ya kombe la dunia 2014.Huu unaitwa uthubutu. 

Ubelgiji nao kwa miaka ya hivi karibuni tumewaona wakibembea sana katika nafasi ya kwanza ya viwango vya soka. Mwaka 2013 na 2014 ilikua viwango vikitolewa basi Ubelgiji inaongoza.

Haikua kazi rahisi kwao lakini walichokifanya hakina tofauti na majirani zao wajerumani. Wao ubelgiji waliwatawanya makocha wakasome ukocha nje ya Ubelgiji. Hivyo wataalamu hao walisambaa Ujerumani na Uholanzi na wakarudi na maarifa ya kutosha nyumbani.

Makocha wale ndio waliosambazwa katika vilabu kama wasaidizi na wengine timu za taifa za vijana. Maarifa waliyoyatumia kwa vipaji vyao yalikuwa yanaleta matunda. 

Wabelgiji pia waliamua kuwatumia Walimu wa shule kupewa mafunzo ya uamuzi wa soka. Imani yao ilikuwa kumfundisha mwalimu wa shule ni rahisi na atashikilia maadili.Mbinu hii imeigwa na hata Cameron. Wanawatumia waamuzi ambao kwa asilimia kubwa ni wenye maadili mazuri.Hoja ya maadili inakuja kwa lengo la kutotaka kutokea kwa masuala ya rushwa. Pia inashauriwa lazima mwamuzi awe na shughuli inayomwingizia kipato.

Mikakati hiyo ilikuja kuwaleta akina Romelu Lukaku Bolingoli,Eden na Thorgan Hazard,Radja Nainggolani, Christian Benteke,Vincent Kompany na wengineo.


TUNAIGA LIPI ILI KUFANIKIWA KAMA TAIFA.

Shirikisho kwa kushirikiana na serikali pamoja na wadau tunapaswa kuiga haya.Kwanza tukubali kuanza upya sio vibaya katika kutaka kufikia malengo.

Tunatakiwa kuiga mfumo wa Ubelgiji kwa waamuzi hivyo chama cha soka kwa kushirikiana na Chama cha waamuzi na serikali kupitia idara ya maendeleo ya michezo iliyo chini ya Yusuph Omary Sengi wachuke walimu na kuwapa mafunzo.

Walimu hawa watakuja kutuelea matunda kutokana na kuwa na maadili ya kiutumishi ambayo wameyaapia katika utendaji wao. Kufanya hivyo kutatuletea waamuzi ambao hawatalalamikiwa kama ilivyo sasa.

Pili tunatakiwa kushirikiana na serikali pamoja na vyama vya soka vya Mkoa kufanya haya. Serikali ya Mkoa ielekeze chama cha soka kupitia kwa maafisa michezo kutafuta maeneo ambayo watajenga vituo vya soka kutokana na mapato ya chama husika. Mfano katika mapato ya michezo kile kinachwa katika klabu kitumike kujengea vituo kwa kutafuta hata msaada kwa wadau ili kufanikisha.

Baada ya kupatikana kwa vituo hivyo vitafutwe vipaji kwa kufanyiwa mchujo na baadae wale wanaofanikiwa waweze kulipiwa na wazazi wao karo ya kulelewa kisoka katika vituo. Na hata kama wako wanaosoma basi watahamishiwa shule katika maeneo ya jirani na kituo.

Upatikanaji na namana ya kutunza vipaji hivyo ni tofauti na ilivyokua kwa Taifa stars Maboresho. Baada ya hapo timu ya taifa ya vijana itapatikana kwa urahisi kama Mkurugenzi wa michezo atafanya kazi bega kwa begani na wasimamizi wa vituo hivyo.

Kufanyika kwa mashindano ya vituo vya soka ni moja ya sehemu ya kujua vipaji vilivyopo katika vituo. Kama sio kutilia mkazo kwa kuwasaidia vijana kufanikiwa kupata hata timu za kuchezea. Kuwatelekeza wakiwa hawajui wapi kwa kwenda ni kitu kibaya ambacho kimezoeleka kufanyika kwetu.

Kama tutakuwa watu tunaolipuuzia soka la vijana haitashangaza Somalia wanashiriki Afcon sisi tukiendelea na singeli zetu.Kujidhatiti ni jambo bora sana ambalo tunalikosa na tunahitaji kupata mafanikio ya zaidi ya sasa kwa vijana wetu.

Kwa upende wa uongozi wa shirikisho uwe wa Sera ya kusaidia wachezaji wanaopata vilabu nje ya nchi. Mfano suala la Abdi banda lingeweza kutatuliwa haraka na shirikisho kwa kusaidia kumwandikia barua Banda huku ikiambatanishwa na nakala ya mkataba wa Simba ambao ulikuwa Tff ili kuwajulisha klabu ya Baroka fc kuwa yuko huru.

Shirikisho la soka la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo liliwahi kuingia katika mtindo huu. Ilikua ni kutaka kuwasukuma wachezaji wakacheze soka nje ya Kongo. Harakati hizo ndizo tulizokuja kuwaona wachezaji kama Romana LuaLua aliyekipiga klabu kama Portsmouth. Hii ilikua baada ya kuona fedheha iliyowakuta Kongo baada ya kuweka rekodi katika vitabu vya michezo kuwa ni timu iliyowahi kufungwa goli nyingi kombe la dunia.

Harakati hizo za kuwatafutia vilabu nje ya Kongo ilikua baada ya rekodi ya kichapo cha goli Tisa kwa bila toka kwa Yugoslavia.Kama vichapo vikubwa tumeshafungwa sana kama timu ya Taifa. Kila Mdau anakumbuka kichapo toka kwa Algeria cha goli saba tukafananishwa na mataifa kama Djibouti.

Kuanza upya sio vibaya la msingi ni kutambua malengo yetu ni nini katika soka.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad