HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, August 16, 2017

TTCL 4G LTE sasa yatua mkoani Iringa

Kampuni ya Simu Tanzania TTCL imezindua huduma ya teknolojia mpya ya 4G LTE mkoani Iringa ili kuongeza kasi ya maendeleo na kuimarisha mawasiliano katika mkoa huo.

Hafla hiyo ya uzinduzi ilihudhuriwa na Mgeni Rasmi, Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Asia Abdallah aliyemuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza, Mkuu wa Wilaya Iringa, Richard Kasesera, Afisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Waziri Kindamba, Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa na Meneja wa TTCL –Iringa, Mhandisi Ekael Manase.

Akizindua huduma hiyo Mgeni rasmi alisema Mkoa wa Iringa ni maarufu kwa mazao ya kilimo na biashara hivyo huduma hiyo itawanufaisha wananchi kuwasiliana na kupeana taarifa kuhusu shughuli mbalimbali za maendeleo.

Aidha amesema kuanzishwa kwa huduma hiyo mkoani humo ni fursa nyingine kwa wananchi kwani itatoa mchango mkubwa katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, usafiri, biashara, utalii, huduma za jamii na sekta nyingine mbalimbali.

“Natumia fursa hii kutoa rai kwa Wana Iringa na Wananchi kwa ujumla kutumia TTCL kwani ni Mtandao wa wenye huduma bora na tozo nafuu, zenye kukidhi mahitaji ya Makundi yote katika jamii” Alisema Mkuu wa Wilaya ya Kilolo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dc Asia Abdallah.

Aidha, mgeni rasmi amewataka Wakazi wa Iringa kuziona fursa za kibiashara zinazotolewa na TTCL kama vile kuwa Wakala wa kuuza vocha, wakala wa TTCL PESA na huduma mbalimbali zitolewazo na kampuni hii ili waweze kujipatia kipato.

Katika hatua nyingine alitoa changamoto kwa TTCL kupanua wigo wa huduma zake ili kuyafikia maeneo ya vijijini ambako zinafanyika shughuli nyingi za kiuchumi hasa Kilimo na biashara ambavyo vinahitaji sana Mawasiliano ya uhakika.

Naye, Afisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Waziri Kindamba aliwataka wananchi kutumia huduma za TTCKL ambazo zimeboreshwa zaidi ili kukidhi mahitaji ya wateja wetu.

“Uzinduzi wa huduma hiyo, ni utekelezaji wa mpango mkakati ambao TTCL imejiwekea kwa kusambaza huduma za mawasiliano bora nchini kote. Uzinduzi wa huduma ya 4G, ni miongoni mwa hatua za utekelezaji wa mpango mkakati huo, ambao unaongeza idadi ya mikoa iliyofikiwa kuwa 15 kati yake 13 ya Tanzania Bara na miwili ya Tanzania visiwani ”amesema Bw. Waziri Kindamba.

Aidha, Afisa Mtendaji Mkuu aliwahakikishia wananchi kuwa TTCL imejipanga vyema katika kuhakikisha inatoa huduma bora ya mawasiliano ya simu ya Mkononi, mezani na huduma bira ya Intaneti.
Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Asia Abdallah kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa Iringa, Amina Masenza (wa tatu kulia), akiwa ameshika bango sambamba na Afisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Waziri Kindamba (wa pili kushoto) pamoja na Mbunge wa Iringa Mjini, Mchunaji Peter Msingwa (kushoto), wakiashiria uzinduzi wa huduma ya TTCL 4G mkoani Iringa na kushuhudiwa na Mkuu wa Wilaya Iringa, Richard Kasesera (wa pili kulia) pamoja na Meneja wa TTCL Mkoa wa Iringa, Mhandisi Ekael Manase.
Afisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Waziri Kindamba (katikati) akimuonesha matumizi ya Simu ya Mezani isiyotumia waya, Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Asia Juma Abdallah katika uzinduzi wa huduma ya 4G mkoani Iringa.
Afisa Mtendaji Mkuu Bw.Waziri Kindamba akimuonesha Mbunge wa Iringa Mjini, Mchunaji Peter Msingwa jinsi huduma ya 4G ilivyobora na spidi kubwa ya Intaneti, katika hafla ya uzinduzi wa 4G Iringa.
Afisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Waziri Kindamba akihutubia kwenye hafla ua uzinduzi wa huduma ya TTCL 4G Mkoani Iringa.

Afisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Waziri Kindamba (wa pili kushoto) akimuonyesha Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Asia Juma Abdallah namna huduma hiyo inavyofanya kazi wakati wa huduma ya 4G mkoani Iringa. Wengine pichani toka kushoto ni Mbunge wa Iringa Mjini, Mchunaji Peter Msingwa, Mkuu wa Wilaya Iringa, Richard Kasesera (wa pili kulia) pamoja na Meneja wa TTCL Mkoa wa Iringa, Mhandisi Ekael Manase.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad