HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, August 30, 2017

NIPASHE, MWANANCHI WAPEWA ONYO NA SERIKALI.

Na: Neema Mathias-MAELEZO 
Serikali imevionya vyombo vya habari nchini hususan baadhi ya magazeti ambayo yamekuwa na mtindo wa kuandika habari pasi na kuzingatia maadili na weledi wa kitaaluma.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari leo katika ukumbi wa Idara ya Habari-MAELEZO jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu, Idara ya Habari –MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi alitahadharisha kuwa aina hiyo ya uandishi unaweza kuleta madhara kwa jamii.

Katika onyo hilo, Dkt. Abbasi ametolea mfano vichwa vya habari katika kurasa za kwanza za magazeti ya Nipashe na Mwananchi matoleo ya leo Jumatano Agosti 30, 2017 ambavyo alisema vimelenga katika kuwatia hofu wananchi, kuleta taharuki na kuashiria sintofahamu kati ya wananchi na Serikali.

Katika matoleo hayo ya leo Gazeti la Nipashe liliongozwa katika taarifa yenye kichwa cha habari “NI MATESO” na Gazeti la Mwananchi liliongozwa na habari yenye kichwa cha habari “Bomoabomoa Nyingine ya Kufa Mtu yaja Dar”.

Mkurugenzi Mkuu huyo na Msemaji Mkuu wa Serikali alifafanua kuwa wakati kichwa cha habari cha gazeti la Nipashe kililenga kuwatia hofu wananchi na kusababisha taharuki katika zoezi linalofanyika kisheria kichwa cha habari cha Mwananchi kinatoa taswira kama kwamba watakaobomolea nyumba zao kisheria wajiandae kwa vita na taharuki. 

“Zoezi linaloendelea linafuata sheria na taratibu kulingana na aina ya zoezi. Ziko nyumba ambazo zina amri za mahakama, wako waliopewa onyo la kuondoka katika maeneo ambayo ni hatarishi kama bonde la Msimbazi” alieleza Dk. Abbasi na kueleza kuwa katika kutekeleza zoezi hilo kama zimejitokeza karsoro hazina budi kurekebishwa.

Dk. Abbasi aliwaeleza waandishi wa habari waliohudhuria mkutano huo kuwa Serikali haina nia ya kuyachukulia hatua magazeti hayo lakini alitumia fursa hiyo kuyatahadharisha magazeti hayo na magazeti mengine pia yenye mtindo wa kuandika vichwa vya habari vinavyohukumu kuacha mtindo huo vinginevyo sheria itachukua mkondo wake.

“Waandishi wa habari tuna misingi yetu ya uandishi hivyo hatupaswi kuandika kichwa cha habari kinachohukumu ama kutia hofu kwa jamii, hivyo navipa onyo vyombo vinavyoandika vichwa vya habari vyenye maudhui kama hayo” Dkt. Abbasi alisisitiza.

Mkurugenzi Mkuu huyo na Msemaji Mkuu wa Serikali alivitaka vyombo vya habari kusimamia ukweli na kufanya uchambuzi ili kusaidia jamii badala ya kuandika mambo kwa sababu tu yametokea.

Alitolea mfano kuwa inashangaza kuona baaadhi ya vyombo vya habari vinashindwa kuona ukweli kuhusu hatari za watu wanaoishi maeneo hatarishi kama bonde la Msimbazi na kusubiri kuandika habari za misaada kwa watu hao wakati wa majanga.  

Kwa hivyo, alitumia fursa hiyo kuvikumbusha tena vyombo vya habari kuwa tasnia ya habari ni taaluma yenye misingi na maadili yanayopaswa kuzingatiwa na pale misingi na maadili hayo yatakapoendelea kukiukwa Serikali haitasita kuchukua hatua kali zaidi za kisheria kwa maslahi ya taaluma na jamii.
 Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari (MAELEZO) na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi (katikati) akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati akitoa onyo kwa magazeti ya Mwananchi na Nipashe kwa kuandika vichwa vya habari vinavyohukumu, kulia ni Mkurugenzi Msaidizi kitengo cha Habari,  Rodney Thadeus na kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi kitengo cha Usajili, Patrick Kipangula.
 Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari (MAELEZO) na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi (katikati) akionesha  waandishi wa habari (hawapo pichani) gazeti la Mwananchi lenye  kichwa cha habari kinachotoa hukumu, kulia ni Mkurugenzi Msaidizi kitengo cha Habari,  Rodney Thadeus na kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi kitengo cha Usajili, Patrick Kipangula.
Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari (MAELEZO) na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi (katikati) akionesha  waandishi wa habari (hawapo pichani) gazeti la Nipashe lenye  kichwa cha habari kinachotoa hukumu, kulia ni Mkurugenzi Msaidizi kitengo cha Habari,  Rodney Thadeus na kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi kitengo cha Usajili, Patrick Kipangula.

Picha na Eliphace Marwa - Maelezo

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad