HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, August 7, 2017

KATIBU MKUU NYAMHANGA AAGIZA UJENZI WA MIZANI BARABARA YA DODOMA – BABATI (KM 263).

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga, amewaagiza Mameneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Dodoma na Manyara kuhakikisha wanatafuta eneo la kujenga kituo cha mizani ili kudhibiti madereva wanaozidisha uzito katika barabara ya Dodoma- Babati (km 263), inayojengwa kwa kiwango cha lami.
Akizungumza katika eneo la Bonga, mkoani Manyara Eng. Nyamhanga, amesema kuwa barabara hiyo ambayo inatarajiwa kukamilika baadae mwezi huu inahitaji uwepo wa mizani kwa haraka ili kudhibiti  magari yanayozidisha uzito na kuharibu barabara. 

"Hakikisheni mnatafuta eneo la kujenga mizani ndani ya miezi miwilli ambapo wakandarasi bado wapo hapa ili iwe rahisi kwenu kumtumia mmoja wa wakandarasi hawa kuweza kujenga kituo hiki haraka, uwepo wa mizani hii utasaidia kudhibiti magari makubwa yanayozidisha uzito", amesema Katibu Mkuu Nyamhanga.
Aidha, Eng. Nyamhanga amewaagiza mameneja wote nchini kuchukua hatua kali za kisheria kwa watu wote wanaopitisha mifugo katika barabara ili kudhibiti uharibifu wa barabara.

Amewataka  madereva wote nchini kuendesha magari yao kwa tahadhari na kuzingatia alama za barabarani ili kudhibiti ajali zinazoepukika.
Katibu Mkuu Nyamhanga ametoa wito kwa wananchi wanaoishi kando ya barabara hiyo kuhakikisha wanatumia fursa ya kukamilika kwa barabara hiyo kwa ajili ya kuleta maendeleo katika maeneo yao ili kukuza uchumi kwa familia zao na Taifa kwa ujumla.
Amemataka  mkandarasi wa sehemu ya barabara ya Mela - Bonga (km88.8)  kuhakikisha anakamilisha kazi zilizobaki kwa wakati na kwa viwango vilivyo kwenye mkataba.
Katika hatua nyingine, Eng.Nyamhanga, ametembelea na kukagua barabara ya Mayamaya- Mela (km 99.35) kwa kiwango cha lami na daraja la Kelema lenye urefu wa mita 205 na kuridhishwa na ujenzi wake na kumtaka mkandarasi wa mradi huo kukabidhi mradi huo ifikapo mwezi Oktoba mwaka huu.
Kwa upande wake, Mhandisi Mshauri wa barabara ya Mayamaya- Mela (km 99.35), Leornado Licari,  amemhakikishia Katibu Mkuu huyo kumaliza mradi huo kwa wakati kwani kazi  zilizobaki kwa sasa ni ndogo kama kumaliza tabaka la mwisho la lami na uwekaji wa alama za barabarani.
Barabara ya Dodoma- Babati (km 263) ni sehemu ya barabara kuu ya kaskazini (Great North road), inayoanzia Capetown nchini Afrika Kusini hadi Cairo nchini Misri ambapo hapa nchini barabara hiyo inayopitia Tunduma mkoani Mbeya, hadi Namanga mkoani Arusha ina urefu wa kilomita 1500,hivyo kukamilika kwa sehemu ya barabara ya Dodoma – Babati (km 263), kunaiunganisha barabara yote kutoka Capetown hadi Cairo yenye  urefu wa kilomita 100000 kwa kiwango cha lami.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
 Mhandisi Mshauri wa barabara ya Mayamaya – Mela (km 99.35), Eng. Leornado Licari, akitoa maelezo ya mradi wa barabara hiyo kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga (wapili kushoto), alipofanya ukaguzi mkoani Dodoma.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga, akitoa maelekezo kwa mkandarasi wa kampuni ya CHICO anayejenga sehemu ya barabara ya Mayamaya – Mela (km 99.35), alipofanya ukaguzi mkoani Dodoma.
 Muonekano wa sehemu ya juu ya daraja la Kelema lenye urefu wa mita 205 linalounganisha wilaya ya Chemba na Kondoa mkoani Dodoma.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga, akikagua kingo za daraja la Kelema lenye urefu wa mita 205 linalounganisha wilaya ya Chemba na Kondoa mkoani Dodoma.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga (wapili kushoto), akiwa na wataalamu wanaosimamia ujenzi wa barabara ya Mayamaya – Mela (km 99.35), inayojengwa kwa kiwango cha lami mara baada ya kuikagua mkoani Dodoma. Wanne kushoto ni Mkurugenzi wa barabara Eng. Ven Ndyamukama.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga, akikagua sehemu ya barabara ya Mela – Bonga (km 88.8), inayojengwa kwa kiwango cha lami mkoani Manyara.
 Ujenzi wa barabara ya Dodoma – Babati kwa kiwango cha lami sehemu ya Mela – Bonga (km 88.8), ukiendelea.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga, akitoa maelekezo kwa Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Manyara, Eng. Bashiri Rwesingisa (kulia), na mkandarasi wa Kampuni ya China Railway Seventh Group Co. Ltd anayejenga sehemu ya Mela – Bonga (km 88.8), mkoani Dodoma.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad