Na Mwandishi Wetu, Kondoa
BAADA ya baadhi ya vyombo vya habari kutangaza kuwepo mgogoro kati ya
wananchi na serikali katika Pori tengefu la Mkungunero wilayani Kondoa
mkoa wa Dodoma, mkuu wa wilaya hiyo amejitokeza na kudai taarifa hizo
hazina ukweli.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Mkuu wa Wilaya
ya Kondoa Bibi Sezaria Makota, alisema habari zilizosambazwa kuhusiana
na wananchi kunyanyaswa katika pori la Mkungunero zinazungumzia
matukio ya zamani ambayo kimsingi yameshapatiwa ufumbuzi na serikali.
“Katika taarifa zilizotolewa kwenye vyombvo vya habari imeelezwa kuwa
viongozi na wanakijiji katika Kijiji cha Kisondoko na Kata ya KK kuwa
wananyanyaswa na kuna wasichana walisema wamebakwa lakini nakanusha
taarifa hizi si za kweli, wafanyakazi wa pori la Mkongonero
wanajiheshimu na wanafanya kazi kwa nidhamu,” alisema Bi. Makota na
kuongeza:
“Nilipofika Kondoa mwaka jana (2016) nilisikia hayo malalamiko lakini
nilipofuatilia nikabaini si kweli, viongozi wa kamati ya ulinzi na
usalama waliitisha mkutano kuwahoji wanakijiji wanaosema
walinyanyashwa, kupigwa na kubakwa, kulikuwepo na madaktari
waliowafanyia vipimo lakini hakuna aliyeonekana amebakwa.”
Katika maelezo yake Bi. Makota aliweka wazi kuwa ni kweli wanahabari
walifika ofisini kwake kumhoji kuhusiana na manyanyaso wanayofanyiwa
wakazi wa Kijiji cha Kisondoko, wakafanya mahojiano pia na meneja wa
poro hilo, lakini taarifa zao hazikutolewa kwenye vyombo vya habari
bali zimetolewa za upande mmoja kinyume na maadili ya uandishi wa
habari.
“Waandishi wa habari walimuhoji meneja wa pori la akiba la Mkongonero
na wakanihoji mimi lakini mbona tuliyozungumza hawakuyatoa kwenye
vyombo vya habari,” alihoji Bi. Makota na kuongeza:
“Njilimuuliza (mwandishi ambaye hata hivyo hakumtaja jina) umekuta
wananchi wangapi wameumizwa, wangapi wamenyanyaswa au kubakwa, akasema
amehoji tu wananchi kwa ujumla. Nikamwambia arudi akawahoji
walioumizwa na waliobakwa lakini hadi sasa hajarejea.”
Akizungumzia ziara ya Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhandisi
Ramo Makani, Bi. Makota alisema Agosti 8, 2016 naibu waziri huyo
alipotembelea wilaya yake wananchi waliibua suala hilo la manyanyaso
lakini walipotakiwa kujitokeza waliofanyiwa vitendo hivyo hakuna
aliyejitokeza kutoa ushuhuda.
Hata hivyo, mkuu huyo wa wilaya alikiri matatizo hayo kutokea lakini
ilikua masuala ya zamani ambayo tayari yameshapatiwa ufumbuzi, hata
viongozi wa kijiji hicho walikiri kuwa wananchi walikua wakikumbukia
mambo yaliyotokea zamani si kwa wakati huu.
“Kijiji cha Kisondoko ni miongoni mwa vijiji vilivyoanzishwa ndani ya
pori hili tengefu, lakini wananchi wanaishi vizuri na tayari
wameshatambua mipaka yao. Lakini wapo wananchi wanaotaka kujaribu
kuvuka mipaka na hao ndio wanaozusha habari hizi zisizo na ukweli, kwa
nafasi yangu nitahakikisha sheria inafuatwa na kulinda mipaka kwa
mujibu wa taratibu za uhifadhi,” alisisitiza Bi. Makota.
Tangu kuanzishwa kwa poro tengefu la Mkungunero wilayani humo
kumekuwepo na mvutano kati ya askari wa pori hilo na wananhi kutokana
na madai kuwa wananchi wanataka kuingilia mipata ya pori, hata hivyo
viongozi kwa muda mrefu wamekuwa wakifuatilia kwa karibu mgogoro huo
na unaonyesha kuwa na tija.
Mwisho
Wednesday, August 23, 2017
Hakuna mgogoro wowote pori Tengefu la Mkungunero-DC Kondoa
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment