Serikali mkoani Mwanza imeitaka jamii kote nchini kuwapeleka
watoto wanaoishi na maambukizi ya virusi vya ukimwi shule, badala
ya kuwanyanyapaa na baadhi kuwaficha ndani na kisha kufifisha
ndoto zao za maisha.
Akizungumza katika kambi ya siku tano mjini hapa, mganga mkuu
wa mkoa wa Mwanza Dk Leonard Subi kwenye ufunguzi wa kambi
hiyo iliyotayarishwa na taasisi isokuwa ya serikali ya ‘Ariel Glaser
Pediatric AIDS Healthcare Initiative (AGPAHI) na kuwakutanisha
watoto wanaoishi na maambukizi ya virusi vya Ukimwi kutoka
mikoa ya Tanga, Simiyu na Mara, Subi amehimiza umuhimu wa
malezi kwa watoto
“Naamini kila mtoto ana ndoto zake katika maisha lakini zaidi sana
katika kusoma na vipaji vingine endapo tu akisaidiwa kwa
kujengewa mazingira rafiki yakumwezesha kupata elimu bila
bugudha, alisema Subi na kuongeza “Kila mtoto ana haki ya kuishi,
apate afya bora”.
Naye , mkurugenzi mtendaji wa taasisi hiyo ya AGPAHI, Dr. Sekela
Mwakyusa, alisema jukumu la taasisi hiyo zaidi ni kutoa usaidizi
kwa vituo vya afya vilivyopo katika serikali kuu pamoja na serikali
za mitaa kwenye huduma za afya hususan katika maswala ya
HIV/UKIMWI, sambamba na huduma za afya ya uzazi kwa mama
na mtoto.
Mwakyusa alifafanua kuwa tangu taasisi hiyo ilipoanzishwa mwaka
2011, imekuwa ikifanya kazi katika mikoa miwili ya Shinyanga na
Simiyu. Lakini toka mwezi Oktoba mwaka 2017 taasisi imekuwa na
kutoa huduma katika mikoa sita ikiwemo Mwanza, Mara, Geita na
Tanga.
Amefafanua kwamba hadi kufikia mwezi Machi 2017 walikuwa
wamewafikia watu wenye maambukizi ya virusi vya ukimwi
wapatao 189,000 na kati ya hao 8,620 ni watoto wadogo ambao ndio
nguvu kazi ya taifa lijalo.
“Kwetu kama Taasisi ni kutoa huduma shirikishi zaidi na
kuhakikisha kwamba tunaondoa maambukizi ya virusi vya Ukimwi
kwa watoto na pia tunabaki na kizazi ambacho hakina UKIMWI.”
Alisema
Ameongeza kwamba tayari wamefikia asilimia tano ya watu wote
ambao wanawahudumia wakiwa ni watoto ingawaje lengo ni kufikia
angalau asilimia kumi ya watoto na hivyo wanafanya jitihada zote
kuweza kuwapata wale watoto kwenye vituo vya afya na pia kwenye
jamii.
Hata hivyo, AGPAHI inajukumu la kuwafuatilia afya za akina mama
wakiwa bado na uja uzito hadi wanapozaliwa kuhakikisha kwamba
wanapata huduma zote zinazostahili toka tu pale mama anapo pata
ujauzito.
“Wapo wale watoto ambao kwa bahati mbaya mama hakuweza
kutabulika kwamba ana matatizo na tunawakuta mara nyingi tukiwa
tumeenda kufanya kampeni za upimaji au kwenye vituo vya afya
wanakuja na tunawatambua.” alisema Mwakyusa.
Aidha alitoa wito kwa jamii kuwa na ushirikiano kwani asilimia
kubwa ya jamii hasa akina mama hawana nafasi ya kufanya
maamuzi kama vile kwenda kupata huduma za afya kwa wakati,
huku wakiahidi kuweka kambi ingine katika mkoa wa Kagera
itakayohusisha mikoa ya Mwanza, Geita na Shinyanga kwa lengo
lakuzidisha uelewa kwa jamii juu ya masuala ya afya katika miezi
ijayo.
No comments:
Post a Comment