HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, December 7, 2016

SERIKALI YAOMBWA KUWAPATIA BIMA YA AFYA WALEMAVU WA NGOZI

Muweka hazina wa Chama cha Watu wenye Ualbino Tanzania, Abdilah Omari  akiwa pamoja Leonard Gasper anayesumbuliwa na tatizo la kansa na kumpatia msaada wa kiasi cha fedha milioni moja kwa ajili ya matibabu.


Na Anthony John,Globu ya Jamii.


CHAMA cha watu wenye ualbino Tanzania (TAS) kimetoa wito kwa Serikali kuwapatia bima ya Afya watu wenye ulemavu wa ngozi ili kuweza kuwasaidia pale wanapokuwa na matatizo ya kiafya.

Akiongea  na waandishi wa habari leo Jijini Dar es salaam katika Ofisi ya chama hicho iliyopo hospitali ya Ocean Road, Muweka hazina Abdilah Omary amesema watu wenye ualbino hasa waliopo vijijini wanapata changamoto kubwa ya upatikanaji wa matibabu hasa pale wanapo sumbuliwa na magonjwa mbali mbali.

 Abdilah ametoa wito kwa jamii na familia zenye watu wenye ualbino kuwapa malezi yanayoendana na hali yao tofauti na Jamii nyingi kwa hivi sasa wanawalazimisha watu wenye ualbino kufanya kazi ngumu kama kuchunga ngo'mbe na kulima.

Wakati huo huo wajumbe wa chama cha watu wenye ualbino Tanzania wamemchangia kiasi cha sh.milioni moja Leonard Gaspar mwenye ulemavu wa ngozi Mkazi wa Morogoro Matombo anayesumbuliwa na kansa ya ngozi.

Hata hivyo Leonard  amewashukuru wajumbe wa chama hicho kwa mchango huo huku akiomba jamii na wadau mbalimbali kuwapa msaada pale wanapoweza ili apate mtaji wakumsaidia katika maisha ya kila siku na matibabu.

Chama hicho cha watu wenye ualbino Tanzania wametoa wito kwa jamii kumsaidia kijana Leonard anaye sumbuliwa na tatizo la kansa ya ngozi kwa muda mrefu.

Hata Hivyo Abdilah ameomba Jamii ya watanzania watakaoguswa na tatizo alilonalo Leonard wanaweza kutoa michango yao kwa kuwasiliana na Ofisi za Chama Cha Watu Wenye Ualbino kilichopo Katika Hospital ya Ocean Road.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad