HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, November 21, 2016

fursa ya uwepo wa meli za mizigo na abiria katika ziwa Nyasa itahimarisha uchumi wa wananchi wa Mikoa ya Njombe, Mbeya na Ruvuma

 Muonekano wa Meli za Mv. Njombe na Mv.Ruvuma ambazo ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 99, meli hizo zipo katika hatua za majaribio kabla ya kuanza kutoa huduma.
 Mkurugenzi wa Kampuni ya Songoro Marine Transport Bw. Salehe Songoro akimuonesha Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani (katikati) ripoti ya ukaguzi wa ujenzi wa meli mbili za mizigo katika bandari ya Itungi ziwa Nyasa.
 Kaimu Meneja  wa bandari ya Itungi na Kiwira Eng. Juma Kisavara (wa kwanza kushoto) akifafanua jambo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani (katikati) kuhusu namna ya kuondoa mchanga katika kingo za ziwa Nyasa ili kuwezesha meli zinazotengenezwa kuingizwa katika maji kwa urahisi.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akikagua Meli ya Mv. Njombe ambayo ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 99.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akipanda juu ya Meli ya Mv. Ruvuma ambayo ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 99 ili kuona mfumo wa injini unavyofanya kazi.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akikagua mfumo wa uendeshaji wa Meli ya Mv. Njombe ambao ujenzi wake umekamilika kwa asilimia 99.
Meneja wa Wakala wa barabara Mkoa wa Mbeya Eng. Paul Lyakurwa akifafanua jambo kwa  Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani alipokagua ujenzi wa barabara ya Kikusya-Ipinda hadi Matema KM 34.6 ambayo inajengwa kwa kiwango cha lami.Picha na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano


Imeelezwa kuwa uchumi wa wananchi wa Mikoa ya Njombe, Mbeya na Ruvuma utaimarika kwa kasi kama watatumia vizuri fursa ya uwepo wa meli za mizigo na abiria katika ziwa Nyasa.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani amesema kukamilika kwa meli mbili za mizigo za Mv. Njombe na Mv. Ruvuma na ujenzi wa meli ya abiria ya Mv. Mbeya ni fursa mpya ya kiuchumi kwa wakazi wa mikoa hiyo.

“Tumejipanga kuhakikisha tunafungua ukanda huu wa nyanda za juu kusini kiuchumi hivyo ni jukumu la wananchi kuchangamkia fursa za kibiashara zinazoweza kusafirishwa ndani na nje ya nchi ili kukuza uchumi”.amesema Eng. Ngonyani.

Naibu Waziri Ngonyani ameelezea kuridhishwa kwake na hatua ya ujenzi wa meli za Mv.Njombe na Ruvuma ambao umefikia asilimia tisini na tisa na kusisitiza kuwa Serikali itaendelea kuwaamini makandarasi wazawa wanaofanya kazi kwa ubunifu, uadilifu na uaminifu ili kutoa fursa nyingi za ajira kwa watanzania.

Kaimu Meneja wa bandari ya Itungi na Kiwira Eng. Juma Kisavara amemhakikishia Naibu Waziri Ngonyani kuwa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) imejipanga kuhaikikisha bandari zote kumi na tano zilizopo katika ziwa Nyasa kwa upande wa Tanzania zinafufuliwa na kutumika kupakia na kushusha mizigi ikiwemo vifaa vya ujenzi, makaa ya mawe,mbolea na mazao ambayo yana soko ndani na nchi za jirani.

Eng. Kisavara amemhakishia Naibu wa Ujenzi kuwa tayari wametafuta soko la kutosha la kusafirisha mizigo hivyo kuiomba Serikali kuendelea na kasi ya ujenzi wa meli nyingine zitakazotumika katika ziwa Nyasa.

Zaidi ya shilingi bilioni 11 zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa Meli ya Mv.Ruvuma na Mv. Njombe zinazojengwa na kampuni ya Songoro Marine Transport ya hapa nchini na meli hizo zinatarajiwa kukabidhiwa kwa Serikali mwezi Januari mwakani.

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Ngonyani amekagua ujenzi wa barabara ya Kikusya-Ipinda hadi Matema KM 34.6 wilayani Kyela inayojengwa kwa kiwango cha lami na kusisitiza kuwa Serikali italipa fedha kwa mkandarasi anayejenga barabara hiyo ili kuiwezesha kukamilika kwa muda uliopangwa.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad