HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, July 14, 2016

GST yatoa ufafanuzi kuhusu Tetemeko la Ardhi lililotokea mkoani Dodoma

Na Samwel Mtuwa, GST

Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) imetoa  taarifa kwa wananchi kuhusu tetemeko la ardhi lililotokea tarehe  13 Julai, 2016, majira ya saa 12:01:15 alfajiri , likiwa na ukubwa wa kipimo cha Ritcher 5.1.

Kitovu cha tetemeko hilo kilitokea umbali wa kilomita 11 Mashariki mwa mji wa Haneti ambao upo umbali wa kilomita 79 Kaskazini Mashariki mwa mji wa Dodoma.

Akizungumza na MEM Bulletin ofisini kwake, Mtalaam wa Matetemeko katika Idara ya Jiolojia, GST, Gabriel Mbogoni, alisema kuwa eneo hilo lipo katika ukanda wa Bonde la Ufa la Afrika Mashariki, maeneo hayo  hukumbwa na matukio ya matetemeko ya ardhi mara kwa mara.

Akifafanua kuhusu chanzo cha tetemeko, Mbogoni alisema kuwa  hiyo ni kutokana  na tabaka la miamba katika maeneo hayo kuwa na  kina kidogo ikilinganishwa na maeneo ambayo yako nje ya ukanda wa Bonde la Ufa.

“Hali hii husababisha matabaka ya miamba katika ukanda huo kuwa katika hali ya fukuto jingi la joto na kusigana kwa miamba ambapo husababisha miamba hiyo kukatika, hali ambayo hufanya ardhi itikisike,” alisema Mbogoni.

Alisema kuwa kiutalaam hali hiyo husababisha miamba hiyo kukatika na kusababisha mtikisiko wa ardhi ambao ndio huitwa tetemeko la ardhi. Akieleza kuhusu madhara ya tetemeko hilo, Mbogoni alisema kuwa mpaka muda wa mchana wa siku ambayo tetemeko lilitokea, hakukuwa na taarifa yoyote ya madhara  kwa wananchi, majengo au miundombinu  iliyotolewa kutokana na tetemeko hilo.

Alifafanua kuwa eneo la Haneti kijiografia lipo katika ukanda wa Bonde la Ufa, maeneo ambayo yana mipasuko mingi ya miamba. Alisema kiutalaam mawimbi ya tetemeko la ardhi yana tabia ya kusafiri umbali mrefu katika mwendo wa kasi alitolea mfano  mawimbi ya  P na S yanaweza kusafiri umbali wa kilomita 8-13 kwa sekunde.

Akizungumzia kuhusu tahadhari, Mbogoni alisema kuwa, wananchi wanaposikia hali ya kutokea kwa Tetemeko la Ardhi  wanapaswa kuchukua tahadhari ya kukaa mbali na miti, nguzo za umeme na nyumba ndefu kama vile maghorofa, na pindi wanapokuwa ndani ya nyumba wanashauriwa kukaa katika kona za ukuta wa nyumba  ili kujizuia na madhara.

Moja ya majukumu ya GST ni kufanya uchunguzi juu ya matetemeko, maporomoko, mipasuko ya ardhi katika eneo zima la nchi, kwa sasa GST ina vituo tisa ya kurekodi taarifa zote  za matetemeko katika mikoa mbalimbali  ya nchi kama vile Dodoma, Arusha, Babati, Singida, Geita, Kibaya, Kondoa , Mbeya na Mtwara.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad