Kama mwandishi na mmiliki wa blog kama hii ya BC [mahali ambapo vipaji huibuliwa na majina kutambulishwa] mojawapo ya majukumu yangu ya kawaida kila siku au kila wiki ni pamoja na kupokea kazi mbalimbali za wasanii. Mara nyingi,kazi hizo zinakuwa bado hazijasikika katika masikio ya wapenzi na mashabiki wa muziki. Hivyo basi,ni jukumu langu pia kuzisikiliza nyimbo hizo, kuzifafanua na kuzielewa ili kupata maudhui yanayofaa katika kuitambulisha nyimbo na msanii mwenyewe.
Kuna wanaochipukia na kuna wanaoanza safari ndefu ya kuelekea kwenye umaarufu au kujikimu na maisha. Kuna wanaokuwa wanarejea baada ya mapumziko na tafakuri na kuna ambao wanakuwa wameogopa kwamba wanaanza kusahauliwa na hivyo wanajifaragua kurejea kilingeni.
Hivi sasa, kila jua linapozama,maelfu ya vijana wanajisogeza vitandani mwao kupumzisha mwili na akili huku ndoto zao zikilenga kwenye “kutoka” kwa maana ya kuwa msanii superstar ajaye. Kazi ya kuwaza ni kazi.Kazi ya kufanya kinachotakiwa kufanyika ili kutimiza lengo au malengo ni kazi zaidi.
Sanaa inalipa. Sanaa ni kazi. Sina takwimu halisi lakini bila shaka tunakubaliana kwamba sanaa inatoa ajira kwa maelfu [kama sio mamilioni] ya vijana nchini mwetu.Na ni kweli kwamba ingelipa zaidi endapo taratibu na sheria mbalimbali [ambazo zipo] zingetumika vyema. Kuna wanaofaidi Jasho la hawa vijana na ndio maana kuna “mgando” katika utekelezaji wa sheria hizo. Hii ni mada ambayo natumaini kuifanyia kazi zaidi katika siku za usoni.


No comments:
Post a Comment