Wakazi wa Makete mjini wilayani Makete mkoani Njombe wameonesha mfano wa kuigwa na nchi nzima baada ya kutii agizo la serikali liliowataka kubomboa nyumba zilizopo kandokando mwa barabara ndani ya kipindi cha mwezi mmoja
Zoezi hili la kubomoa nyumba hizo lilitakiwa kufanywa ndani ya kipindi cha mwezi mmoja ili kupisha ujenzi wa barabara ya lami Makete mjini kama ilivyoahidiwa na serikali
Mtandao huu ulishuhudia zoezi la kubomoa nyumba hizo likitekelezwa kwa zaidi ya asilimia 95 huku wananchi hao wakiitaka serikali kuharakisha kujenga barabara hiyo kwa wakati kwa kuwa wameahidiwa kwa muda mrefu
"Sisi tunapenda maendeleo ya wilaya yetu ndio maana unaona tunabomoa bila usumbufu, lakini isiwe tunabomoa halafu ujenzi unakuja kuanza miaka ijayo huko mbele huu utakuwa ni uonevu wa hali ya juu kwa kweli" alisema mfanyabiashara mmoja aliyejitambulisha kwa jina moja la Chaula
Wabomoaji hao wameendelea kubomoa nyumba zao kwa umakini na kuchukua baadhi ya vifaa kama tofali, milango, madirisha na mbao ili waweze kwenda kuvitumia kwenye maeneo mengine waliyoyapata
Kwa mujibu wa tangazo la TANROADS mkoa wa Njombe, zoezi la kubomoa kwa hiari limemalizika na kwa yeyote ambaye hatakuwa ametii amri hiyo, bomoa bomoa ya serikali itapita ili kuondoa jengo hilo(na www.edwinmoshi.com)

No comments:
Post a Comment