Ofisi ya afya wilaya ya Makete mkoani Njombe imekusudia
kununua kamera kwa ajili ya kupigia picha za baadhi ya watu wanaojisaidia ovyo
mitaani kwa lengo la kuwadhibiti na kuwachukulia sheria watu wa namna hiyo
ikiwemo kuwafikisha mahakamani
Kauli hiyo imetolewa leo katika ukumbi wa halmashauri ya
wilaya ya Makete na Afisa afya wilaya hiyo Bw. Boniphace Sanga katika kikao
kilichowahusisha mkuu wa polisi Makete, Afisa biashara, afisa afya pamoja na
wamiliki na wahudumu wa baa na vilabu vya pombe za kienyeji
Bw. Sanga amesema ofisi yake imefikia hatua hiyo baada ya
kuona vitendo vya kujisaidia hovyo hasa maeneo ya baa na vilabu yanakithiri
licha ya adhabu mbalimbali kuchukuliwa dhidi yao, na wengine kudai kuwa
wanaonewa na ofisi yake, hivyo wameamua kununua kamera ambazo wakiwapiga picha
watu hao picha moja wanawapelekea wenyewe na nyingine wanaihifadhi na kuitumia
kama ushahidi mahakamani
Amesisitiza wamiliki na wahudumu hao kuhakikisha wanatunza
usafi wa maeneo yao ya biashara kwa kuweka vyombo vya kuhifadhi taka na
kuhakikisha wanapokwenda kuzitupa dampo vyombo hivyo wanarudi navyo, na kuwepo
kwa maji moto ya kuoshea glasi ama vikombe vya kupimia pombe za kienyeji
Ameongeza vitu vingine wanavyotakiwa kuvifanya kuwa ni kuvaa
sare sketi nyeusi, blauzi nyeupe na kofia ama kilemba na wanaume suruali
nyeusi, shati nyeupe na kofia pamoja na kufunga taa za mwanga mkubwa kwenye
maeneo ya giza ya nyumba zote za biashara za vileo kwani wateja wakishakunywa
pombe hupenda kwenda jirani kwenye maeneo yenye giza na kujisaidia hapo
“Hayo ni maagizo tafadhali yazingatiwe la sivyo
tutawanyang’anya leseni za kufanyia biashara, mteja akiona kagiza kadogo tuu
hapo hapo anajisaidia na matokeo yake athari za mikojo ama vinyesi vinawaathiri
watu wote” alisema Sanga
Kwa upande wake mkuu wa polisi wilaya ya Makete (OCD) SP
Peter Kaiza amewataka wahudumu hao kuzingatia muda wa kufunga na kufungua
nyumba za kuuzia vileo na kusisitiza kuwa hakuna mtu yeyoteakiwemo yeye ambaye
upo juu ya sheria.
Amesema kumekuwa na utaratibu ambao unafanywa na baadhi ya
maafisa wakubwa wa serikali ambao kwa wadhifa wao ama vyeo vyao huwafuata
wahudumu wa vilabu ama baa na kuwataka kufungua kabla ya muda halali kwa
kisingizio kwamba hakuna atakayekuuliza, hivyo kuwataka wakatae na kuwataka
wawaambie waje muda wa kufungua ukifika
SP Kaiza amesema hali hiyo kwa hivi sasa haitafumbiwa macho
na wao kama jeshi la polisi wataanza kuwakamata wote wanaokiuka masharti ya
leseni zao na kuwafikisha mahakamani ili waadhibiwe kwa mujibu wa sheria
“Hakuna hata mmoja aliyepo juu ya sheria, na endapo
tutakukamata umewahi kufungua ama umechelewa kufunga kwa kisingizio cha
kuwahofia wateja wako kuwa ni watu wakubwa hapa, tutakumata na kukufikisha
mahakamani, na kumbuka hakuna atakayekutetea na waliokudanganya watakuacha
utaabike peke yako” alisema Kaiza
Naye Afisa biashara Bw. Edonia Mahenge amesema ni marufuku
kuchangaya pombe za kienyeji na za viwandani na kuziuza katika chumba kimoja na
kama mtu anataka kufanya hivyo anatakiwa kutenga mabanda mawili kwa kuwa hizo
ni biashara nyingi tofauti
Amesema hayo kufuatia ombi lililotolewa na mmoja ya mmiliki
wa kilabu cha pombe za kienyeji katika kitongoji cha Dombwela Bw. Harun ambaye
amesema wanaomba kuruhisiwa kuuza vileo vyote kwa pamoja kwa kuwa hawana mitaji
ya kutosha kupanga mabanda mawili, hali iliyopingwa na SP Kaiza na kusisitizwa
na afisa biashara kuwa hiyo haiwezekani
Afisa biashara huyo amesema maagizo hayo yaliyotolewa katika
kikao hicho yatatumika wilaya nzima hivyo wafanyabiashara hao wanatakiwa
kuyazingatia na kutekeleza maagizo hayo.
Imeandikwa na Edwin Moshi, Makete
No comments:
Post a Comment