HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, February 21, 2013

UMOJA WA MATAIFA KUFANYA MAJARIBIO YA DRONES KATIKA OPERESHENI ZA KULINDA AMANI

 Balozi Ramadhani Mwinyi,Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa  Ubalozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, akizungumza wakati wa Mkutano wa Kamati Maalum inayohusika na  Operesheni za Ulinzi wa Amani C-34. Wakati wa mkutano huo  Mkuu wa Idara ya  Operesheni ya Ulinzi wa Amani ya Umoja wa Mataifa (DPKO), Bw. Herve Ladsous aliwataarifu  washiriki wa mkutano huo,  kwamba  Idara hiyo ilikuwa ikijielekeza katika matumizi ya teknolojia za kisasa ( Unmanned Aerial System ) maarufu kama Drones katika operesheni za kulinda amani na kwamba  teknolojia hiyo itafanyiwa  majaribio   katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ( DRC) 

Na Mwandishi Maalum

Wakati Idara ya Operesheni ya Ulinzi wa Amani ya Umoja wa Mataifa (DPKO) ikijielekeza katika matumizi ya teknolojiza za kisasa katika shughuli za ulinzi wa amani,  zikiwamo ndege zisizokuwa na rubani (Unmanned Aerial Systems ) maarufu kama Drones. Baadhi ya mataifa hasa yale yanayoendelea yanataka kuwapo kwa majadiliano zaidi  kuhusu  matumizi ya zana hizo.

Taarifa  ya  matumizi ya teknolojia za kisasa katika ulinzi wa amani,  imetolewa na Mkuu wa DPKO , Bw Herve Ladsous, wakati wa ufunguzi wa  mkutano wa Kamati  Maalumu inayohusika na masuala ya  operesheni za kulinda amani maarufu kama C-34.  Kamati hiyo maalumu ipo chini ya  Kamati ya Nne ya Baraza kuu la Umoja wa Mataifa. 

Katika taarifa yake, Bw Ladsous ameeleza kwamba uamuzi wa kutumia teknolojia za kisasa zikiwamo  unmanned aerial systems (UAS)  unalenga katika kuboresha utendaji kazi wa misheni za kulinda amani, kukusanya taarifa na kutoa tahadhari za awali na kubwa zaidi  kuokoa maisha ya walinzi wa amani dhidi ya hujuma mbalimbali.

 Katika  mwaka uliopitia (2012) walinzi wa amani 111 wakiwamo watanzania sita wamepoteza maisha kwa nyakati tofauti  kwa kushambuliwa wakati  wakitekeleza majukumu yao ya kuwalinda wananchi katika nchi zenye migogoro.

Akieleza zaidi kuhusu  mpango huo,  Bw. Ladsous amesema, zana hizo zitaanza kwa majaribio katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, kupitia misheni ya kutuliza amani   MONUSCO.

“Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, ametoa pendekezo la kutumika kwa majaribio teknolojia hii  katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya  Kongo. Tunafanya kazi kwa karibu na   Baraza Kuu la  Usalama , nchi  mwenyeji, na wadau wengine kuhakikisha kwamba walinzi wetu wa amani wanapata fursa ya kutumia teknolojia ya kisasa” akasema Mkuu wa DPKO.

Na kuongeza kwamba matumizi ya teknolojia   hizo ni muhimu  si katika kuwalinda walinzi wa amani bali pia kuzijengea uwezo na maarifa misheni hizo.

 Mkuu huyo wa DPKO akaeleza zaidi kwamba mchakato  umeanza wa kuomba ridhaa kwa nchi mwenyeji, kuzijulisha nchi jirani, mawasiliano na  nchi zinazotoa walinzi wa amani (TCC) na kuwauliza wauzaji wa zana hizo wale ambao wataonyesha nia.
Baadhi ya mataifa  yaliyoendelea   ingawa yanakili kwamba bado kuna hali ya sintofahamu na hofu kuhusiana na  suala hilo,yanaunga mkono matumizi  hayo  katika kile wanachoamini kutasaidia sana kupunguza  vifo vya walinzi wa amani.

Hata hivyo baadhi ya nchi zinazoendelea na ambazo zinachangia walinzi wa amani maarufu kama TCC,  zinasisitiza kwamba uamuzi wa matumizi ya zana hizo za kisasa ni lazima yajadiliwe  miongoni mwao .  Ikiwa ni  pamoja suala la    sheria  na sera za matumizi ya zana hizo,  raslimali fedha na teknolojia inayoambatana na zana hizo.

Mkutano huu wa Kamati Maalum ya operesheni za kulinda amani  licha ya kujadili suala zima la shughuli za ulinzi wa amani,  unajadili pamoja na mambo mengine changamoto mbalimbali zinazowakabili walinzi wa amani na   mfumo mzima wa utekelezaji wa operesheni hizo.

Baadhi yachangamoto zinazojadiliwa ni pamoja na  mkanganyiko wa dhamana wanayobeba walinzi wa amani ,  uhaba na ufinyu wa raslimali fedha  na vifaa,  dhana ya ulinzi wa raia,  ushirikishwaji  katika utoaji wa maamuzi   , ushiriki wa wanawake  hususani Polisi wanawake katika ulinzi wa amani na   mafunzo kwa walinzi hao wakiwamo  pia Polisi, Magereza na Raia.

Suala  la malipo kwa walinzi wa amani ni jambo ambalo pia limeendelea kutiliwa mkazo katika mkutano huu, na karibu wazungumuzaji wote  ikiwambo Tanzania  ambayo iliwakilishwa na Balozi Ramadhani Mwinyi,   Naibu  Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Matifa.

 Wazungumzaji wote   wametaka  na kusisitiza kwamba  ni matumaini yao   kuwa  mapendekezo yaliyotolewa na  Kundi la Washauri kuhusu  malipo ya walinzi wa amani pamoja na vifaa yatafanyiwa kazi ipasavyo wakati  Kamati ya Tano  ya baraza Kuu la Umoja wa Mataifa itakapokutana mwezi March mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad