HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, December 21, 2011

Wananchi walalamikia serikali kuhusiana na hifadhi ya Tarangire kuvamia ardhi yao

Na Mery Ayo,Arusha.

WANANCHI wa kijiji cha Kimotorok wilayani Simanjiro mkoani Manyara wameilalamikia serikali kuhusiana na hifadhi ya Taifa ya Tarangire kuvamia ardhi ya kijiji hicho kwa lengo la kupanua hifadhi hiyo.. 

Ambapo hifadhi hiyo imekuwa ikivamia eneo hilo la kijiji bila kutoa taarifa zozote kwa uongozi wa kijiji hicho hali ambayo imekuwa ikiwaletea madhara makubwa kwa kukosa mahitaji yao muhimu huku mgogoro huo bado unaendelea . 

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti wa halmashauri ya kijiji hicho, Daniel Melau wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na hatua hiyo ya hifadhi hiyo kuwaondoa wafugaji kwa nguvu kwenye ardhi yao wakidai kuwa wanapanua hifadhi hiyo. 

Aidha aliongeza kuwa hifadhi ya Taifa ya Ruaha imepanuliwa kutoka kilometa za mraba 10,300 hadi kilometa za mraba 20,226 , ambapo hifadhi ya Taifa ya ziwa Manyara nayo imepanuliwa kutoka kilometa za mraba 330 hadi kilometa za mradi 648.7 ,ambapo katika upanuzi huu vijiji vilivyo jirani na hifadhi vimekuwa vikipoteza ardhi na mali nyingi. 

Alisema kuwa, katika hatua hiyo TANAPA imekuwa ikihamisha mipaka iliyowekwa kisheria huku ikichoma moto na kuteketeza nyumba za wananchi wa kijiji hicho hali ambayo imekuwa ikileta mtafaruku mkubwa katika jamii hiyo. Alifafanua kuwa, mnamo tarehe novemba 18 mwaka huu , TANAPA iliwapiga wanakijiji watano na kumlazimisha kijana aitwaye Isaya Nabana kula gamba la nyoka . 

'Tunafahamu kuwa Tanapa ina mpango unaojulikana kwa jina la ujirani Mwema , ila tabia hii ya kuvamia mipaka kinyume cha sheria inakinzana na maana nzima ya ujirani mwema ,ni jirani gani mwema anachoma moto nyumba ya jirani mwenzake na kuhamisha mipaka pamoja na kuvuruga amani katika jamii?'aliuliza Melau. 

Hata hivyo Melau , alimtaka Rais Kikwete awafukuze kazi haraka Waziri wa maliasili na utalii , Ezekiel Maige , pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa TANAPA, Alan Kijazi kwa kuzidi kuzorotesha mahusiano kati ya serikali ya Rais Kikwete na vijiji vinavyopakana na hifadhi za Taifa kama vile kijiji cha Kimotorok. 

Aidha aliitaka hifadhi hiyo, izuie wanyamapori wasikanyage katika ardhi ya kijiji cha Kimotorok ,kwani mifugo ya wananchi inapoingia hifadhini TANAPA hukamatwa , hali ambayo hifadhi hiyo imekuwa ikijichukulia sheria mkononi huku ikifahamu fika kuwa muda mwingi kwa mwaka maelfu ya wanyamapori wapo vijijini , ikiwa ni pamoja na kijiji cha Kimotorok lakini wao wamekuwa hawawakamati . 

Naye Mkurugenzi wa TANAPA Alan Kijazi akizungumza kwa njia ya simu kuhusiana na swala hilo alisema kuwa, wao wanachofanya sio upanuzi wa hifadhi bali ni uhakiki wa mipaka ambao inafanywa na Wizara ya Ardhi na maendeleo ya makazi . Alisema kuwa,TANAPA wao wanawawezesha tu katika kufanikisha zoezi hilo ambalo linafanywa na wataalamu kutoka wizara husika ambao mwisho wa siku watakuja na majibu sahihi kuhusiana na mipaka ilipo.

'Wanavyodai kuwa tumevamia eneo lao kwaupnuzi wa hifadhi sio kweli, nafikiri hapa wananchi tu ndio hawajaelewa tunachofanya na wakumbuke kuwa hifadhi sio mali ya TANAPA bali ni chombo cha serkali na sisi ni wasimamizi tu'alisema Kijazi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad