HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, March 4, 2024

JAMII YASHAURIWA KUCHUNGUZA AFYA ZAO

 

Na Fauzia Mussa, Maelezo Zanzibar
RAIS wa Rotary club ya Zanzibar Stone Town ndg. Augustine Mwombeki ameishauri jamii kuwa na tabia ya kuchunguza afya mara kwa mara ili kugundua magonjwa nyemelezi na kupata tiba mapema.

Akizungumza na waandishi wa habari katika kambi ya uchunguzi na matibabu bure kwa wananchi wa makunduchi iliyofanyika Skuli ya Kiongoni Mkoa wa kusini Unguja amesema endapo jamii itaendeleza utamaduni huo itasaidia kugundua maradhi katika hatua za awali na kupatiwa matibabu kwa muda stahiki.

Amesema uwepo wa kambi za uchunguzi na matibu vijijini kunahamsisha na kushajihisha wananchi kujitokeza kuchunguza afya zao na kuishauri jamii kuchangamkia fursa za kambi hizo pale zinapotokezea.

Aidha alizitaka taasisi nyengine za Serikali na binafsi kushirikiana kujidhatiti kutoa huduma bora za afya kwa jamii ikiwa ni pamoja na kuungamkono kambi kama hizo ziweze kufanyika mara kwa mara vijijini kwani wamekuwa wazito kwenda Hospital na kuishia kutumia mitishamba jambo ambalo linahatarisha afya zao.

Amefafanua kuwa Kambi hiyo ni kwaajili ya kufanya uchunguzi wa maradhi mbalimbali kwa Watoto, Wazee na kina mama wapatao 1500 ambapo wamejipanga kutoa huduma tofauti zikiwemo uchunguzi wa magonjwa ya meno,macho,ngozi,masiki, koo na pua, HIV pamoja na magonjwa ya kina mama katika kijiji hicho.

Akizungumzia kuhusu taasisi hiyo alisema kuwa ni taasisi ya kimataifa yenye lengo la kusaidia na kutatua changamoto mbalimbali za kijamii ikiwemo huduma za afya.

Kwa upande wake daktari wa kutoka hospitali ya Tawakal Madvan Nestory Rwegasira aliihimiza jamii kuchangamkia fursa za kambi za uchunguzi na matibabu zinapotokezea kwani zinasaidia kujua magonjwa nyemelezi ambayo yatasababishwa nagonjwa makuu.

“unaweza ukawa unaumwa ila hujijui unatembea hata siku ukianguka maradhi yameshakuwa makubwa na ngumu kutibika”

Nao baadhi ya wananchi akiwemo Zulfat Muhaji Mkaazi wa Kiongoni na Ali Matata Haji Mkaazi wa Mtende wameishukuru taasisi hiyo kwa kuweka kambi ya uchunguzi na matibabu kijijini hapo jambo litalowasaidia kugundua hali za afya zao na kupatiwa matibabu.

wamesema jamii haina tabia ya kuchunguza afya zao kutokana na gharama ambapo wameishukuru taasisi hiyo kwa kuweka kambi hiyo na kuwataka wananchi wezao kujitokeza katika kambi kama hizo ili kupata fursa ya kujua afya zao na kupatiwa matibabu.

Hata hivyo wananchi hao wameziomba taasisi nyengine kujitokeza kuweka kambi kama hizo katika maeneo mengine ili wakaazi wa maeneo hayo wapate fursa ya kuchunguzwa afya zao.

Kambi ya uchunguzi na matibabu bure katika skuli ya kiongoni imeendeshwa na taasisi mbalimbali ikiwemo Rotary club Zanzibar stone town hospitali ya Ampola,skuli ya afya suza na home nursing care.

MAELEZO YA PICHA

Picha no.01:-Rais wa Rotary club ya Zanzibar Stone Town ndg. Augustine Mwombeki akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na zoezi la uendeshaji wa kambi ya uchunguzi na matibabu bure huko Skuli ya Kiongoni Makunduchi mkoa wa Kusini Unguja

PICHA NA FAUZIA MUSSA –MAELEZO ZANZIBAR



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad