HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, November 14, 2023

Mkurugenzi Mkuu wa VETA Afanya Ziara Ofisi za VETA Kanda ya Kati na Chuo cha VETA Dodoma

 

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Dkt. Prosper Mgaya akizungumza wakati wa ziara yake katika Ofisi za VETA Kanda ya Kati na Chuo cha VETA Dodoma.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Dkt. Prosper Mgaya akiwa katika Chuo cha VETA Dodoma na Ofisi ya   VETA  Kanda ya Kati.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) Dkt. Prosper Mgaya akipata maelezo kutoka kwa Mwalimu Neema Mihambo wa Chuo cha VETA Dodoma alipotembelea karakana ya Ukataji na Uchakataji Nyama chuoni hapo.

Picha ya pamoja ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Dkt. Prosper Mgaya  katika Ofisi za VETA Kanda ya Kati na Chuo cha VETA Dodoma

 
*Aainisha mikakati kuboresha utoaji mafunzo kwenye vyuo vya VETA
 
MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Dkt. Prosper Mgaya amefanya ziara katika Ofisi za VETA Kanda ya Kati na Chuo cha VETA Dodoma ambapo ametembelea karakana kujionea shughuli za mafunzo na kufanya mazungumzo na Menejimenti ya Kanda na Chuo.
 
Akizungumza wakati wa ziara hiyo leo tarehe 13 Novemba, 2023, Dkt. Mgaya  ameainisha mikakati mbalimbali ya kuboresha utoaji mafunzo ya ufundi stadi nchini ili kuwanufaisha wananchi wengi zaidi na kuwawezesha kuendesha shughuli za kiuchumi kwa ufanisi.
 
Mikakati hiyo ni pamoja na kuongeza ubunifu kwenye kuandaa kozi za muda mfupi zinazojibu mahitaji halisi ya jamii, kuboresha vifaa vya utoaji mafunzo vinavyokidhi ukuaji wa teknolojia na kuhakikisha ubiasharishaji wa vifaa vya kiubunifu vinavyozalishwa kwenye vyuo vya VETA.
 
“Ni lazima tuongeze ubunifu katika kuandaa kozi za muda mfupi kujibu changamoto zinazowakabili wananchi kwenye shughuli zao za kiuchumi…tunafanya vizuri sana kwenye eneo la ubunifu lakini changamoto ni namna ya kuhakikisha ubunifu huo unaingia sokoni hivyo tunahitaji kuweka nguvu katika suala hili,”amesema
 
Dkt. Mgaya ameeleza pia umuhimu wa kupata ithibati za kimataifa kwenye mafunzo yanayotolewa ili kuwezesha wahitimu wa VETA kutambulika kwenye soko la ajira kimataifa na kusisitiza nia yake ya kuwezesha walimu kupata mafunzo na ujuzi ndani na nje ya nchi.
 
Aidha, Dkt Mgaya ameeleza kuridhishwa na maandalizi yanayofanywa na Kanda ya Kati kwa ajili kuanza kutoa mafunzo kwenye vyuo vipya vya ufundi stadi vya Wilaya yanayotarajia kuanza kutolewa mwezi Januari, 2024 na kumuagiza Mkurugenzi wa Kanda hiyo kushirikisha viongozi wa Wilaya husika katika maandalizi ya kozi zitakazotolewa kwenye vyuo hivyo.
 
Ameelekeza chuo cha VETA Dodoma kuandaa kozi za aina mbalimbali zinazokidhi mahitaji ya jamii na kuzitangaza ili wananchi wazifahamu na kujitokeza kujiunga na kozi hizo ili waweze kujipatia ujuzi wa kuendesha shughuli zao za kiuchumi.

Dkt Mgaya amesema mikakati hiyo itachangia kufanikisha malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwapatia watanzania ujuzi utakaokuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na kwamba VETA inategemewa kufanikisha malengo hayo.
 
Awali, Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Kati, Ndg. John Mwanja  aliwasilisha taarifa ya kanda hiyo inayohusisha mikoa ya Dodoma, Singida na Manyara ambapo amesema Kanda yake imejipanga vyema katika kuhakikisha vyuo vilivyopo kwenye kanda yake vinatoa mafunzo bora na kufikia wananchi wengi zaidi.
 
Mkuu wa Chuo cha VETA Dodoma, Ndg.Stanslaus Ntibara, amesema hadi sasa, chuo chake kina jumla ya wanafunzi 4350 ambapo 650 ni wa kozi za muda mrefu na 3700 ni wa kozi za muda mfupi ikiwa ni ongezeko la asilimia 30 kutoka mwaka 2022.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad