HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, September 20, 2023

DC MATINYI AZINDUA RASMI ZOEZI LA ARDHI CLINIC

 Na Joanita Joseph -TMC

MKUU wa wilaya ya Temeke Mheshimiwa Mobhare Matinyi ametoa wito kwa wakazi wa Temeke kujitokeza kwa wingi kwa ajili kuboresha usalama wa milki za ardhi zao ikiwemo kugawiwa hati papo hapo.

Mhe. Matinyi ameyasema hayo leo Septemba 20, 2023 kwenye mkutano wa uzinduzi wa Ardhi Clinic, zoezi ambalo lipo chini ya Mradi wa uboreshaji usalama wa milki za ardhi (LTIP) unaofadhiliwa na Benki ya Dunia chini ya wizara ya ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi.

Mhe. Matinyi amemshukuru Mhe. Rais Daktari Samia Suluhu Hassan kwa kutafuta fedha kwa ajili ya kuboresha milki za ardhi nchini na kuwataka Wananchi kutumia fursa hiyo muhimu.

"Mheshimiwa Rais ametafuta fedha kwa ajili ya kuboresha milki za ardhi kwenye maeneo yetu, hivyo Wananchi tutambue umuhimu na tujitokeze kwa wingi, jambo zuri huduma zote zinatolewa kielektronikia unapewa hati yako na rekodi zako zinahifadhiwa kidigitali " alisema DC Matinyi

Kwa upande wake msimamizi wa mradi Bi. Aisha Masanja amesema kuwa zoezi hilo litadumu kwa siku 25 na litapita kwenye mitaa mitano.

"Tumeanzia hapa Mbagala kuu mashariki, na tutakuwa hapa viwanja vya Zakhiem kuwahudumia wananchi kwa muda wa siku tano, na baada ya hapo zoezi hili litahamia kwenye mitaa mingine ambayo ni Buza, kisewe, Mwembebamia,na Mianzini" alisema Bi. Aisha

Mara baada ya Mkuu wa wilaya kuzindua rasmi zoezi hilo, alikabidhi kwa Wananchi hati milki zilizoshughulikiwa papo hapo.

Mradi wa uboreshaji usalama wa Milki za ardhi (LTIP) unalenga kutatua changamoto zote zinazokabili urasimishaji ardhi nchini ikiwemo kupanga na kupima maeneo yanayoyohitaji leseni za makazi na hati Miliki, kurahisisha gharama za upimaji, kutoa hati na leseni za makazi pamoja na kuboresha miundo mbinu ya ardhi kwa nchi nzima.
Mkuu wa wilaya ya Temeke Mhe. Mobhare Matinyi (kulia) akimkabidhi mkazi wa wilaya ya Temeke hati miliki ilishoghulikiwa kwenye zoezi la ardhi clinic (hati papo hapo).
Wakazi wa wilaya ya Temeke katika picha ya pamoja na Mkuu wa wilaya wakifurahia hati zao walizogawiwa katika zoezi la ardhi clinic (hati papohapo).

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad