HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, May 12, 2023

MAREKANI YAWEKEZA MILIONI 12 KATIKA BIASHARA YA KILIMO YA VIJANA TANZANIA

 

SERIKALI ya Marekani imetoa dola milioni 12 (TZS 28 bilioni) kusaidia vijana wa Kitanzania katika kuanzisha, kuendesha na kuwekeza katika biashara ya kilimo bara na Zanzibar. Tangazo hilo lilitolewa na Balozi wa Marekani nchini Dkt. Michael A. Battle na Mkurugenzi Mkazi wa USAID/Tanzania Bi. V. Kate Somvongsiri katika hafla za uzinduzi wa Mradi wa Feed the Future - Uimarishaji Sekta Binafsi Zanzibar na Dodoma.

"Kwa zaidi ya miongo sita, Marekani imethamini ushirikiano wake na Tanzania," alisema Balozi Battle wakati wa uzinduzi wa PSSA mjini Zanzibar Mei 5. "Kupitia ushirikiano wetu Serikali ya Marekani inaendelea kujitolea kutengeneza ajira, kuboresha upatikanaji wa fedha. , na ushauri wa kuweka mazingira wezeshi ya wajasiriamali na sekta binafsi kuwekeza na kustawi katika mustakabali wa Tanzania.”

Mbali na kuwasaidia vijana wa Tanzania kupata mikopo ya biashara, ujuzi, na masoko, PSSA pia itahakikisha usimamizi wa haki na usawa wa kanuni za biashara za serikali ili kusaidia wajasiriamali wadogo. Ikilenga maeneo ya SAGCOT bara ikiwemo Iringa, Mbeya, Morogoro, na Unguja na Pemba Zanzibar, PSSA itatoa ruzuku za ushindani kwa vyama, mashirika na makampuni ya sekta binafsi yanayofanya kazi kuboresha mazingira wezeshi ya biashara na kupanua fursa za uchumi kwa vijana. Kwa ujumla, PSSA inalenga kufikia vijana 30,000, kuimarisha huduma za biashara kwa makampuni 6,000 yanayoongozwa na vijana, kutoa huduma za kifedha kwa zaidi ya vijana 3,000, na kuanzisha sera mpya 10 ili kuchochea fursa za kiuchumi kwa vijana na kuwezesha upanuzi katika masoko mapya.

Katika uzinduzi wa mradi wa PSSA mjini Dodoma, Mkurugenzi Mkazi wa USAID/Tanzania Bi. Kate Somvongsiri alisema, “Mradi wa Uimarishaji wa Sekta Binafsi wa Feed the Future Tanzania unatoa kipaumbele kwa kuwekeza kwa vijana. Kwa kufanya kazi pamoja na vyama vya sekta binafsi ikishirikiana na Mpango wa Wizara ya Kilimo wa Kujenga Taifa Bora la Kesho, tutaunga mkono utekelezaji wa sera zinazowasaidia vijana kuondokana na vikwazo vya kuwawezesha kiuchumi. PSSA inaweza tu kufikia malengo haya kwa ushirikiano na serikali ya Tanzania na washirika wa sekta binafsi kote nchini.”

Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Kilimo, Dk. Hussein Omari, katika hafla hiyo mjini Dodoma alisema, “Naona fursa za ushirikiano kati ya PSSA na Mpango wetu wa Kujenga Taifa Bora la Kesho: Mpango wa Vijana wa Kilimo Biashara. Serikali ya Tanzania imejizatiti kikamilifu kufanya kazi na mradi huu kusaidia vijana katika sekta binafsi na kukuza uwekezaji wa ndani na kimataifa.”
Kwa taarifa zaidi wasiliana na Ofisi ya Mawasiliano Ubalozi wa Marekani Tanzania kupitia barua pepe: DPO@state.gov.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad