HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, April 5, 2023

TAHADHARI YATOLEWA MATUMIZIA MAJI YA MSUKA

 Na Rahma Khamis Maelezo Zanzibar 5/4/2023

WIZARA ya Afya Zanzibar imewataka wananchi kuacha kutumia maji ya chemchem yanayodaiwa kuwa tiba kwa maradhi mbalimbal ili kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza katika jamii.

Akitoa taarifa ya tahadhari kwa Waandishi wa Habari kuhusiana na maji hayo huko Ofisini kwake Mnazimmoja Waziri wa Afya Zanzibar Mhe,Nassor Ahmed Mazrui amesema kuwa maji hayo si salama na hayafai kwa matumizi ya viumbe hai.

Amesema kuwa hivi karibuni kupitia mitandao ya kijamii kumekuwa kukisambaa taarifa ya kuwepo kwa chemchem ya maji katika shehia ya Msuka Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba, ambayo wanadai kuwa maji hayo ukinywa yanaweza kutibu magonjwa mbalimbali.

Aidha amesema kutokana na hali hiyo kumepelekea kujitokeza watu mbalimbali kutoka Pemba na nje ya hapo kuchukua maji hayo kwa kutumia vyombo mbalimbali ikiwemo madumu na chupa ambapo Wizara baada ya kusikia hivyo ilipeleka watalamu kuchukua sampuli ya maji hayo na kuyafanyia uchunguzi.

Amefahamisha kuwa uchunguzi umebaini maji hayo sio salama na hayafai kwa matumizi ya binadam kutokana na kuwa na idadi kubwa ya vimelea kati ya 220 hadi 1800 kwa kila lita moja ya ujazo wa maji, kiasi ambacho kinasababisha maradhi ya kuharisha nas vidonda vya tumbo.

Pia amesema katika uchunguzi huo kumeonekana uwepo wa kloraid kiasi cha miligram1490hadi 2059 kwa kila lita moja ya maji kiwango ambacho ni kikubwa kwa matumizi ya Binadamu.

Waziri Mazrui alifafanua kuwa kwa kawaida maji ya kunywa yanatakiwa yawe na kiasi cha chumvi kiwango 0 ambapo katika uchunguzi maji hayo yamebainika kuwa na Ukali wa chumvi kati ya 2.8 na 3.8 ambacho ni zaidi ya kiwango kilichokubalika kwa matumizi ya kunywa.

Aidha amefahamisha kuwa kutokana na matokeo hayo katika maji kunmeonesha kuwa maji hayo yamechafuliwa na kinyesi cha viumbe hai na kuwa na kiwango kikubwa cha kemikali ambacho sio salama katika mwili wa binadamu.

Waziri Mazrui amewataka Wananchi waliotumia maji hayo kujitokeza katika vituo vya Afya kwa Ajili ya Uchunguzi zaidi.

"Ikiwa kutajitokeza matatizo yoyote kwa mtu amabae katumia maji hayo na amehisi mabadiliko katika mwili wake basi afike Hospitali mapema na sisi tutamfanyia uchunguzi na kumpatia tiba bila ya gharama yeyote," alisema Waziri.

Akitoa ufafanuzi wa kitaalamu Mkemia Mkuu wa Serikali Dokt, Farid Mzee Mpatani amesema ili maji yawe salama lazima kuangalia ubora wa nadharia ,kemikali za maji na vijidudu ambavyo vimo ndani maji ili kuhakikisha kuwa yapo salama kwa matumizi ya binadamu.
:Waziri wa Afya Zanzibar Mhe. Nassor Ahmed Mazrui akizungumza na Waandishi wa Habari wakati alipokua akitoa Taarifa ya tahadhari kwa umma kuhusu maji ya chemchem yanayodaiwa kuwa ni tiba yaliyopo pembezoni mwa Bahari Shehia ya Msuka Mashariki Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba, huko Afisini kwake Mnazimmoja Mjini Unguja.April 05 , 2023.Mkemia Mkuu wa Serikali Dkt.farid Mzee Mpatani Akitoa ufafanuzi wa kitaalamu kwa Waandishi wa Habari kuhusiana na maji ya chemechem yaliyopo pembezoni mwa Bahari,Shehia ya Msuka Mashariki Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba wakati wa Mkutano na Waandishi hao uliolenga tahadhari juu ya maji hayo yanayodaiwa kuwa ni tiba, hafla iliyofanyika huko Wizara ya Afya Mnazimmoja Mjini Unguja . April 05 , 2023.
PICHA NA FAUZIA MUSSA –MAELEZO ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad