HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, February 23, 2023

Pesapal yahimiza matumizi ya teknolojia sekta ya Utalii

  
Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda Zanzibar, Omar Said Shaban (katikati), akipata maelezo kutoka kwa Meneja Mkazi wa Pesapal, Bupe Mwakalundwa (wa pili kulia) na Meneja Mkuu wa Pesapal Emmy Rono (watatu kulia) jinsi ya kufanya malipo kupitia mfumo wa Pesapal badala ya fedha taslimu wakati wa kongamano lililowakutanisha wadau wa sekta ya utalii Mjini Zanzibar. Kushoto ni Meneja Biashara Pesapal, Abdul Hatibu Mwamba na wa pili kushoto ni Meneja Biashara Pesapal Zanzibar, Sufii Yussufu.
 
=========     ========    ========

Na Mwandishi Wetu

Kampuni kinara wa huduma za malipo ya Pesapal imewataka wadau wa shughuli za utalii na  ukarimu nchini kuzichangamkia na kuzitumia teknolojia za kisasa kujikwamua na mathira ya janga la Uviko-19 na kuiimarisha upya sekta hiyo muhimu ya utalii.

Maafisa waandamizi wa Pesapal walitoa rai hiyo jana huku Zanzibar kwenye mkutano shirikishi wa kwanza na wadau wa setka mzima ya utalii na ukarimu.

Mkutano huo ulihudhuriwa pia na mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ambao waliipongeza kampuni hiyo kwa kuchagiza matumizi ya huduma za kidijitali kwenye utalii na kusisitiza umuhimu wa usalama wa mifumo ya malipo.
Katika hotuba yake, Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda, Bw Omar Said Shaaban, alisema ubunifu wa kiteknolojia na uwekezaji unaofanywa na Pesapal unaendana na ajenda ya kidijitali ya serikali.

Kiongozi huyo alibainisha kuwa wanaunga mkono kinachofanywa na kampuni hiyo kwenye shughuli za ukarimu kwani jitihada hizo zinaunga mkono mikakati na maono ya serikali ya kujenga uchumi wa kisasa ambao utategemea sana mafanikio ya sekta ya utalii.

"Teknolojia na shughuli za utalii na ukarimu ni pande mbili za sarafu moja. Wadau wa utalii wanapaswa kukumbatia teknolojia za kidijitali ili waweze kukabiliana na ubunifu unaofanyika katika sekta hii na kuweza kuyamudu mahitaji mapya ya soko, ambayo yanabadilika kwa kasi sana,” Waziri Shaaban alisisitiza.

Naye Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Bw Ali Suleimani Ameir, aliwasihi wawekezaji wa teknolojia za kisasa kuhakikisha huduma zao zinasaidia kukuza mapato ya serikali badala ya kuwa vyanzo kwa kupotea kwake.
Bw Ameir alisema serikali za muungano na Zanzibar zimeruhusu matumizi ya mifumo ya kidijitali kwa lengo la kurahisisha shughuli mbalimbali za kiuchumi zikiwemo zile za kifedha hususani malipo na miamala mingine.

Aidha, aliwataka washiriki wa mkutano huo wa Pesapal kuangalia njia na uwezekano wa kupanua huduma za malipo ya kidijitali na kuimarisha matumizi yake huko Zanzibar na Tanzania nzima kwa ujumla.

Mkutano wa jana ulihusu zaidi kuangalia njia ambazo teknolojia mpya zinaweza kusaidia kuimarisha uendeshaji na kuwa na vyanzo vipya na mbadala vya mapato.  

Wataalamu wa Pesapal walitumia fursa hiyo kuwaonyesha na kuwahimiza wadau wa utalii umuhimu wa teknolojia katika mipango yao ya kukuza biashara na mikakati ya kuondokana na mathira ya Uviko.

Meneja wa Pesapal Tanzania, Bi Bupe Mwakalunda, alisema kampuni hiyo ina ushirikiano wa kimkakati na mashirika ya kimataifa kusaidia kutoa suluhisho bunifu za kuimarisha huduma za utalii na ukarimu mara baada ya kupungua sana kwa janga hilo lililoikumba dunia nzima.

“Uundaji wa mifumo ya teknolojia inayoruhusu ubunifu wa haraka, kukuza faida na kuongeza ufanisi itakuwa ni kipaumbele muhimu cha kujikwamua kutoka kwenye janga ja Uviko-19 na kufikia ustahimilivu wa kidijitali,” Bi  Mwakalenda alibainisha.

“Ili kufanikisha jambo hili, tumeshirikiana na Oracle Hospitality ili kutoa suluhisho za kiteknolojia na kusaidia ushirikishwaji wa miundombinu inayoweza kunyumbulika kutoa huduma thabiti na maalumu kwa ajili ya wadau wa kisekta,” aliongeza.

Kongamano hilo la kwanza la “Adopt & Thrive” liliwajumuisha washiriki mbalimbali kutoka katika biashara za hoteli, migahawa, kumbi za starehe na waongoza watalii.

Pesapal na Oracle ni washirika wa karibu wa kuihudumia tasnia ya kusafiri na ukarimu  nchini kupitia utaalamu na suluhisho za teknolojia mahiri ili kurahisisha na kuboresha huduma kwa watalii na wateja wengine kwa ujumla.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad