HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, December 7, 2022

Serikali yaahidi kushughulikia changamoto za wamiliki wa malori nchini

 

 


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam,


SERIKALI Kupitia Wizara yaUjenzi na Uchukuzi imekubali ombi la Chama Cha Wamiliki wa Malori Madogo na ya kati (TAMSTOA) juu ya kodi kubwa katika kichwa na Trela na kodi hizo kuwa mzigo mkubwa kwa wasafirishaji hapa nchini na kupunguza chachu ya uwekezaji katik sekta husika.

Akizungumza kwenye mkutano wa mwaka wa chama hicho jijini Dar es Salaam jana, Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Atupele Mwakibete alisema kwamba serikali kupitia wizara hiyo itaingalia kodi hiyo na kuja na mapendekezo sahihi katika swala la hilo ili kuendelea kuwa pamoja na wadau wa sekta ya usafirishaji na kuchochea maendeleo ya nchini.

“kwa niaba ya serikali tumepokea changamoto ya kodi kwenye sekta hii ya usafirishaji (provisional tax) na nitalipeleka kwa mheshimiwa waziri na tuone ni kwa namna ipi tunaweza kusaidiana hili kupunguza haya malalamiko na hatimaye kuchochea chachu ya ukuaji wa sekta hii muhimu katika kukuza uchumi wa nchini na kuongeza ajira kwa watanzania,” alisema Mwakibete

Aliongeza kwamba kwamba wizara kwa kushirikiana na TAMSTOA na wadau wengine kwenye sekta ya usafirishaji kwa kiasi kikubwa wameweza kupunguza malalamiko mengi ikiwa pamoja na migomo ya mara kwa mara kwa madereva wa malori hapa nchini ambapo serikali ilikuwa inapata hasara kubwa.

“nachukua nafasi hii kuwaomba madereva wa malori hapa nchini kuendelea kuchapa kazi na endapo kuna matatizo yoyote basi wachukue njia za kisheria na za kiutaratibu kwa kuihusisha serikali na chama cha wamiliki wa malori ili kuhakikisha matatizo yao yanafanyiwa kazi kwa njia ya mazungumzo,” alifafanua Naibu Waziri.

Naibu Waziri Mwakibete alisema kwamba baadhi ya matatizo ya muda mrefu kama vile foleni katika mpaka wa Tunduma ambapo ilikuwa ni kero ya muda mrefu kwa madereva na wadau wengine wa usafirishaji sasa limepatiwa suluhisho baada ya serikali kuongeza scanner ili kuharakisha taratibu za kinyaraka pale mpakani.

Kwa upande wa changamoto ya maeneo ya maegesho ya malori kutoka dar es salaam mpaka Tunduma serikali ipo katika hatua za mwisho uanza mchakato na kupata uzabuni wa kujenga eneo la maegesho ya malori ili kuondoa atha kubwa wanaokuwa wanapata wamiliki , mawakala na madereva wa malori hayo.

Awali, Mwenyekiti wa TAMSTOA , Chuki Shabani alisema kwamba wamiliki wa malori nchini wanapitia changamoto nyingi kwenye sekta hiyo ya usafirishaji ikiwemo faini za Mamlaka ya Usafiri wa nchini kavu (LATRA) na kuomba serikali kupitia wizara kuangalia namna nzuri ya kuendelea kufanya kazi kwa pamoja ili kusukuma gurudumu la maendeleo kwa maslahi mapana ya nchini.

“Ni matarajio yetu ombi letu kupitia kwa wizara ya Ujenzi na Uchukuzi wa kuangali upya kodi katika sekta ya usafirishaji litafanyiwa kazi ili wamiliki wa malori waendelee kutoa huduma hii hapa nchini na nchini za jirani na kuchochea uchumi wa nchini na kuongeza kipato cha serikali,” aliongeza Shabani.

Mwenyekiti wa chama hicho aliendelea kusisitiza kwamba pamoja na mafanikio yaliyopatikana kama vile kuondoa migomo ya madereva na kuboresha huduma za mpakani pale Tunduma ila bado tatizo la usalama wa madereva katika nchini za jirani hasa Zambia na Congo kwa sababu matukio ya utekaji wa madereva na malori bado yanaendelea na kuiomba serikali kuendelea kushirikiana na majirani zetu ili kuweza kutatua changamoto hiyo.

Aliongeza kwamba chama hicho kilianzishwa rasmi 24/4/2014 kikiwa na wanachama 40 na hadi kufikia mwaka huu kina takribani ya wanachama 700 nchini nzima na wanatarajia kuendelea ksuhirikiana na mamlaka zote za serikali ili kuboresha sekta ya usafirishaji hapa nchini.

Naye mmoja wa wadau wa sekta hiyo, Salman Karmali ambaye ni Mkurugenzi wa Masoko wa kampuni ya GF Trucks , alisema kwamba kampuni imejikita kuendelea kutoa huduma ya mauzo ya malori ya kisasa hapa nchini na kuendelea kuwa mdau muhimu katika sekta hii nyeti kwa uchumi wa nchini.

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi,Atupele  Mwakibete (katikati) akijadiliana jambo na Makamu  Mwenyekiti chama cha wamiliki wa malori (TAMSTOA) Mgendela Gama wakati wa mkutano mkuu wa Tatu wa Chama cha wamiliki wa maloli nchini uliofanyika jijini Dar es salam jana.Kulia ni Mwenyekiti  wa chama hicho, Chuki Shaban.


Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi,Atupele  Mwakibete (katikati)na Mwenyekiti chama cha wamiliki wa malori (TAMSTOA) Chuki Shaban (kulia) pamoja na Makamu  mwenyekiti wa wa TAMSTOA , Mgendela Gama wakipiga makofi wakati wa ufunguzi wa mkutano  mkuu wa tatu wa chama cha wamiliki wa malori nchini uliofanyika jijini Dar es salaam jana.






No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad