HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, October 19, 2022

TAASISI YA UONGOZI INATOA MAFUNZO YANAYOWAJENGEA UWEZO VIONGOZI KIUTENDAJI ILI KUIMARISHA UTAWALA BORA NCHINI

 

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (katikati) akifafanua jambo alipotembelea Maktaba ya Taasisi ya UONGOZI jijini Dar es Salaam, kabla ya kuzindua Awamu ya Tatu ya Programu ya Mafunzo kwa Viongozi. Kushoto kwake ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya UONGOZI, Bw. Kadari Singo.

Na. Veronica E. Mwafisi-Dar es Salaam
NAIBU Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema mafunzo ya kuwajengea uwezo kiutendaji viongozi katika Utumishi wa Umma na sekta binafsi yanayotolewa na Taasisi ya UONGOZI, yamelenga kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita za kuimarisha Utawala Bora nchini.

Mhe. Ndejembi amesema hayo jijini Dar es Salaam akiwa katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere, wakati akizindua Awamu ya Tatu ya Programu ya Mafunzo kwa Viongozi yanayotolewa na Taasisi ya UONGOZI.

Mhe. Ndejembi amesema, program zote za mafunzo zinazotolewa kwa viongozi kupitia Taasisi ya UONGOZI zimelenga kuimarisha uwezo na kuwaongezea ufanisi kiutendaji kwenye maeneo yao ya kazi.

“Programu hizi za mafunzo kwa viongozi zinazoandaliwa na Taasisi ya UONGOZI zinalenga kuimarisha uwezo wa viongozi katika kufanya maamuzi ya kimkakati, kuongoza rasilimaliwatu na kujenga sifa binafsi za kiongozi,” Mhe. Ndejembi amesema.

Ameongeza kuwa, mafunzo hayo yanayotolewa kwa viongozi kupitia Taasisi ya UONGOZI ni muhimu katika kuimarisha utawala bora utakaokuwa ni chachu ya kuleta maendeleo endelevu nchini.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka washiriki wa mafunzo hayo, kuyazingatia mafunzo kikamilifu ili kupata elimu na ujuzi utakaowaongezea ufanisi kiutendaji na kuleta mabadiliko chanya katika maeneo yao ya kazi pindi watakapohitimu.

Sanjali na hilo, Mhe. Ndejembi amesema mafunzo hayo yameandaliwa katika viwango vya kimataifa ili kuwajenga viongozi kifikra na kimtazamo, kwa kuwapatia uelewa mpana katika masuala ya uongozi na hatimaye kuwa na mchango katika maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Afya Plus, Dkt. Pastory Sekule amesema, baada ya kuhitimu mafunzo hayo anatarajia kupata uzoefu mkubwa zaidi utakaomuwezesha kusimamia rasilimali pamoja na kusimamia mabadiliko kwa kuwaongoza watumishi alionao katika eneo lake la kazi.

Jumla ya washiriki 68 kutoka katika taasisi za umma na sekta binafsi wanashiriki mafunzo hayo ya Awamu ya Tatu ya Program ya Mafunzo kwa Viongozi yanayotolewa na Taasisi ya UONGOZI kwa kushirikiana na Serikali ya Finland pamoja na Umoja wa Mataifa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad