HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, October 18, 2022

MIKATABA YA BILIONI 60.3 YA UJENZI NA UKARABATI WA VIVUKO YASAINIWA

 


Na Alfred S. Mgweno (TEMESA)

Serikali kupitia Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) imesaini mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 60.3 kwa ajili ya ujenzi wa vivuko vipya, ukarabati wa vivuko vinavyoendelea kutoa huduma ambavyo muda wake wa ukarabati umefikia pamoja na ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya vivuko kote nchini.

Hayo yamebainishwa leo wakati wa hafla fupi ya uwekaji wa msingi (Keel Laying) wa ujenzi wa kivuko kipya kitakachokuwa kinatoa huduma kati ya Kisorya Wilayani Bunda Mkoani Mara na Rugezi Wilayani Ukerewe Mkoani Mwanza, hafla iliyofanyika katika yadi ya Songoro iliyopo Ilemela Mkoani Mwanza.

Akizungumza wa kati wa hafla hiyo, Mgeni Rasmi, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Adam Malima amepongeza Wizara ya ujenzi na Uchukuzi pamoja na Wakala wa Ufundi na Umeme TEMESA kwa kuanza Ujenzi wa Kivuko hicho na kuwataka kuhakikisha kinakamilika kwa haraka na kwenda kutoa Huduma katika maeneo ya Kisorya na Rugezi.

“Nafurahi kusikia kuwa kazi ya ujenzi wa kivuko kipya cha Kisorya - Rugezi uko katika hatua za kuanza kujengwa kwa gharama za kitanzania jumla ya Shilingi Bilion 5 ikiwa imetolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania. Sina budi kuipongeza Serikali ya awamu ya sita kwa kutekeleza Ujenzi huu.” Alisema Mkuu wa Mkoa na kuongeza kuwa ujenzi wa kivuko kipya cha Kisorya – Rugezi utachochea na kuboresha huduma za usafiri kwa wananchi wa maeneo zitakapoenda kutoa huduma.

Naye Mtendaji Mkuu wa Wakala huo, Lazaro N. Kilahala, akisoma taarifa fupi ya ujenzi wa kivuko hicho amesema katika mwaka huu wa fedha Wakala unaendelea na Ujenzi wa vivuko vipya vitano ambavyo ni Kisorya - Rugezi, Bwiro – Bukondo, Nyakalilo – Kome, Ijinga – Kahangala na Mafia Nyamisati, “Mikataba yenye thamani ya Tshs 33.2 bilioni imeshasainiwa, Wakandarasi wameshalipwa malipo ya awali na kazi inaendelea, miradi mingine ni vivuko vya Buyagu-Mbalika na Magogoni-Kigamboni ambavyo viko katika hatua za manunuzi. ” Alisema Mtendaji Mkuu na kuongeza kuwa katika mwaka huu wa fedha Serikali inavifanyia ukarabati vivuko 14 vya MV. KAZI, MV. MISUNGWI, MV. MUSOMA, MV. SABASABA, MV. TANGA, MV. NYERERE, MV. KITUNDA, MV. KILOMBERO II, MV. RUHUHU, MV. OLD RUVUVU, MV. MAGOGONI, MV UJENZI, MV KOME II na MV MARA kwa gharama ya Tshs 22.99 bilioni na ukarabati wa miundombinu ya vivuko katika maeneo 11 kwa gharama ya Tshs 4.1 bilioni.

Mtendaji Mkuu ameishukuru Serikali ya Awamu ya sita chini ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha kifedha kutekeleza mradi huo na kuahidi kufanya kazi kwa weledi na jitihada kubwa ili kufikia malengo na matarajio ya Serikali na wanachi kwa ujumla. Kivuko hicho kitakapokamilika kitakuwa na uwezo wa kubeba abiria 800 na magari 22 swa na tani 170.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Adam Malima akichomelea chuma kuashiria kuanza kwa msingi wa ujenzi wa kivuko kipya (Keel Laying) kitakachotoa huduma kati ya Kisorya Wilayani Bunda Mkoani Mara na Rugezi Wilayani Ukerewe Mkoani Mwanza, kivuko hicho kitakapokamilika kitakuwa na uwezo wa kubeba abiria 800 na magari 22 sawa na tani 170. Kushoto ni Major Songoro, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Songoro Marine Transport, hafla hiyo fupi imefanyika katika yadi ya Songoro iliyopo Ilemela Mkoani Mwanza leo.
Major Songoro, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Songoro Marine Transport akimuonyesha Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Adam Malima michoro itakayotumika kwenye ujenzi wa kivuko kipya kitakachotoa huduma kati ya Kisorya Wilayani Bunda Mkoani Mara na Rugezi Wilayani Ukerewe Mkoani Mwanza, kivuko hicho kitakapokamilika kitakuwa na uwezo wa kubeba abiria 800 na magari 22 sawa na tani 170.
Wafanyakazi wa Kampuni ya Songoro Marine ya jijini Mwanza inayoanza ujenzi wa kivuko kipya kitakachotoa huduma kati ya Kisorya Wilayani Bunda Mkoani Mara na Rugezi Wilayani Ukerewe Mkoani Mwanza wakiwa katika picha ya Pamoja wakati wa hafla fupi ya kuweka msingi wa ujenzi wa kivuko hicho iliyofanyika katika yadi ya Songogo iliyoko Ilemela Mkoani Mwanza leo.
Major Songoro, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Songoro Marine Transport akimueleza jambo Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Adam Malima wakati wakikagua ukarabati unaoendelea wa vivuko vya MV. SABASABA na MV. MUSOMA leo mara baada ya kumaliza zoezi la kuweka msingi wa kivuko kipya kinachoanza kujengwa kitakachotoa huduma kati ya Kisorya Wilayani Bunda Mkoani Mara na Rugezi Wilayani Ukerewe Mkoani Mwanza, kivuko hicho kitakapokamilika kitakuwa na uwezo wa kubeba abiria 800 na magari 22 sawa na tani 170. Picha zote na Alfred Mgweno TEMESA 



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad