HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, September 1, 2022

MSIWAFICHE WATOTO WANAOSTAHILI CHANJO YA POLIO- RC SENDIGA

 Na. OMM Rukwa

MKUU wa Mkoa wa Rukwa Queen Sendiga ametoa wito kwa wananchi kutowaficha ndani watoto wanaostahili kupewa chanjo ya polio ili kuwakinga na ugonjwa wa ulemavu.

Ametoa agizo hilo leo (01.09.2022) wakati akizindua kampeni ya tatu ya utoaji chanjo ya polio Kwa watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano iliyofanyika kimkoa katika Kituo cha Afya Mazwi kilichopo Manispaa ya Sumbawanga.

Sendiga aliongeza kusema chanjo ya polio inayotolewa ni salama na kuwa serikali imejipanga kuhakikisha watoto wanakuwa na afya njema.

" Wito wangu ni kwa akina mama na akina baba kujitokeza na kushiriki kutoa taarifa za watoto wanaostahili kupata chanjo ili wataalam wa afya wawafikie huko majumbani na kuwapa chanjo ya polio" alisema Sendiga.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga Sebastian Waryuba alisema Wilaya yake imejipanga kuhakikisha watoto wote wanaostahili wanafikiwa majumbani ndani ya siku nne za kampeni hii ya polio.

Waryuba alisema katika kampeni hii ya awamu tatu Halmashauri ya Manispaa imelenga kuchanja watoto 51,919 na Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga itachanja watoto 83,573.

Kwa mujibu wa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Dkt. Ibrahim Isaack alisema kampeni hii ya tatu Mkoa umelenga kutoa chanjo ya Polio kwa watoto 276,320 kuanzia tarehe 01 hadi 04 Septemba 2022.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad