HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, September 1, 2022

HAFLA YA UTIAJI WA SAINI KATI YA KIST NA ICDL YAFANA ZANZIBAR

 Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Mh.Ali Abdulgulam Hussein amesema ipo haja kwa kila mfanyakazi na wananchi wote kwa ujumla kupatiwa mafunzo ya matumizi sahihi ya kompyuta na uelewa wa mambo ya kidigitali ili waweze kukuza ufanisi katika kazi zao.


Alisema hayo wakati alipohudhuria katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano ya pamoja baina ya Taasisi ya Karume ya Sayansi na Teknolojia(KIST) na Taasisi ya Kimataifa inayoshughulikia utoaji wa Vyeti vya Kompyuta (ICDL), yaliyofanyika katika ukumbi wa Dkt.Idrissa Muslim Hija, Mbweni Zanzibar.

Alisema endapo watumishi wa umma watapatiwa mafunzo ya kina ya matumizi ya mifumo ya kidigitali wataweza kuendana na wakati wa sasa, na kuondoa tatizo la uelewa mdogo wa vitu mbalimbali vilivyomo katika kompyuta na mitandao.

“Nimegundua kuwa bado watu wengi wanauelewa mdogo katika masuala ya kidigitali hasa katika matumizi ya kompyuta katika kazi mbalimbali, waliowengi wanafahamu vitu vichache, vingi hawavifahamu, ambavyo ni muhimu kuvijuwa katika kazi zao” alisema Naibu Waziri.

Hivyo, alitumia fursa hiyo kuushauri uongozi wa Taasisi ya Karume kuhakikisha wanaihamasisha jamii ili ipate mwamko kuhusu umuhimu wa kupatiwa mafunzo hayo, pamoja na kuishauri serikali kuweka mafunzo hayo kwa kila mfanyakazi ili kuboresha utendaji kazini.

Aidha aliupongeza uongozi wa Taasisi ya Karume na Taasisi ya ICDL kwa kufanikisha hatua hiyo muhimu ya kuifanya Taasisi ya Karume kuwa ni kituo cha kutolea mafunzo hayo ambayo yana faida kubwa kwa Zanzibar.

Nae Mkurugenzi wa Taasisis ya Karume ya Sayansi na Teknolojia (KIST), Dkt. Mahmoud Abdulwahab alisema fursa hiyo ni fursa kubwa ambayo Zanzibar tumeipata kwani itawawezesha wananchi na wafanyakazi kupata ujuzi wa hali ya juu na kunufaika katika matumizi ya mambo ya kidigitali.

Alisema kuwa,mambo mengi yaliyomazuri yanaweza kutokea mara tu watakapoanza rasmi kutoa mafunzo hayo, ikiwemo kuwafanya wafanyakazi kuwa wataalamu wa hali ya juu katika matumizi ya kompyuta na hatimae kuwafanya wawe wafanyakazi mahiri na wenye kujuwa mambo mengi.

Aidha alisema Taasisi ya Karume itachukua jitihada mbalimbali za kuhakikisha jamii inapata mwamko kuhusu umuhimu wa ICDL ili wote wanufaike.

Kwa upande wake mwakilishi wa ICDL Afrika, Bw.Peter Maina Taasisi hiyo ipo tayari kufanyakazi na Taasisi ya Karume katika masuala ya mbalimbali ya Kidigitali ili wananchi waweze kunufaika kitaifa na kimataifa.

Alisema mafunzo hayo yatawafanya wananchi kupata ujuzi wa hali ya juu katika masuala ya matumizi ya Kompyuta na hatimae kuongeza uzalishaji, kuweza kuajiriwa na kuajirika popote watakaopenda duniani kwani vyeti watakavyovipata vitakuwa vinatambulika duniani kote.
Mwakilishi wa Taasisi ya Kimataifa ya utoaji wa Vyeti vya Kompyuta (ICDL) Peter Maina wa pili (kushoto), akitia Saini hati za mashirikiano ya kuanzisha Kituo cha kutoa mafunzo na kutoa Vyeti vya Kompyuta vinavyotambulika Kimataifa kwa kushirikiana na Taasisi ya Karume ya Sayansi na Teknolojia Zanzibar (KIST), (wakati kati) ni Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mhe, Ali Abdulgulam Hussein akishuhudia utiaji wa Saini , wa tatu ni Mwanasheria wa Taasisi ya Karume Lutta Mwadini, hafla hiyo imefanyika katika Ukumbi wa Mkutano wa Dkt. Idrisa Muslim Hijja wa Taasisi ya Karume Mbweni Zanzibar .
Mkurugenzi wa Taasisi ya Karume ya Sayansi na Teknolojia Zanzibar (KIST), Dkt. Mahmoud Abdulwahab (kulia) wakikabidhiana hati za mashirikiano ya kuanzisha Kituo cha kutoa mafunzo na kutoa Vyeti vya Kompyuta vinavyotambulika Kimataifa, kushoto ni Mwakilishi wa Taasisi ya Kimataifa ya utoaji wa Vyeti vya Kompyuta (ICDL) Peter Maina, na (wakati kati) ni Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mhe, Ali Abdulgulam Hussein, hafla iliyofanyika Ukumbi wa Mkutano wa Dkt. Idrisa Muslim Hijja wa Taasisi ya Karume Mbweni Zanzibar .
Mkurugenzi wa Taasisi ya Karume ya Sayansi na Teknolojia Zanzibar (KIST), Dkt. Mahmoud Abdulwahab (kulia) akitia Saini hati za mashirikiano ya kuanzisha Kituo cha kutoa mafunzo na kutoa Vyeti vya Kompyuta vinavyotambulika Kimataifa kwa kushirikiana na Taasisi ya Kimataifa ya utoaji wa Vyeti vya Kompyuta (ICDL), (wakati kati) ni Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mhe, Ali Abdulgulam Hussein akishuhudia utiaji wa Saini , wa pili kulia kwa Mkurugenzi ni Mwanasheria wa Taasisi ya Karume Lutta Mwadini, hafla hiyo imefanyika katika Ukumbi wa Mkutano wa Dkt. Idrisa Muslim Hijja wa Taasisi ya Karume Mbweni Zanzibar .
NA MARYAM KIDIKO – KIST.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad