HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, September 14, 2022

Benki ya CRDB yazindua kampeni maalum ya Bima ya Vyombo vya Moto ‘Kuwa Shua’

 
Kaimu Mkurugenzi wa Wateja wadogo na wakati, Bonaventure Paul (wapili kushoto), Mkuu wa Kitengo cha Bima wa Benki ya CRDB, Moureen Majaliwa (kushoto), Meneja Uendeshaji Huduma za Bima Benki ya CRDB, Tumaini Frank, na Meneja Mauzo Orxy, Fredy Mcharo kwa pamoja wakibonyeza kitufe kuashiria uzinduzi rasmi wa Kampeni ya Elimu ya Bima ya Vyombo vya Moto iliyopewa jina la “Kuwa Shua” iliyofanyika katika Gereji ya MacAuto Sinza, Jijini Dar es salaam mapema leo 14 Septemba 2022. 
Mkuu wa Kitengo cha Bima wa Benki ya CRDB, Moureen Majaliwa akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya Elimu ya Bima ya Vyombo vya Moto iliyopewa jina la “Kuwa Shua”, iliyofanyika katika Gereji ya MacAuto Sinza, Jijini Dar es salaam mapema leo 14 Septemba 2022. Wengine pichani ni Meneja Uendeshaji Huduma za Bima Benki ya CRDB, Tumaini Frank (kushoto, na Meneja Mauzo Orexy, Fredy Mcharo.

==========   =========   ===========

Benki ya CRDB leo imezindua kampeni maalum ya elimu ya bima ya vyombo vya moto iliyopewa jina la ‘Kuwa Shua’ katika hafla  ulifanyika katika gereji ya MacAuto iliyopo Sinza Jijini Dar es salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari Mkuu wa Kitengo cha Bima Benki ya CRDB, Moureen Majaliwa amesema lengo la kampeni hiyo ni kuhamasisha wamiliki wa vyombo vya moto kukatia vyombo vyao bima ili kujikinga dhidi ya majanga.

Majaliwa alisema pamoja na kuwa bima ya vyombo vya moto ni moja ya bima zinazotumika kwa kiasi kikubwa bado wamiliki wengi wa vyombo vya moto nchini hawana elimu ya kutosha kuhusu bima, jambo linalopelekea wengi kupuuzia.

“Katika kipindi cha kampeni maafisa wetu wa Benki watakuwa wakitembelea wateja kuwapa elimu ya bima za vyombo vya moto, lakini pia tutakuwa tukitoa zawadi kwa wateja watakaokata bima kupitia Benki ya CRDB,” alisema Majaliwa.

Akielezea kuhusu zawadi kwa wateja Majaliwa alisema wamiliki wa vyombo vya moto watakaolipia bima kubwa ya ‘comprehensive’ watarudishiwa asilimia 5 ya kiasi cha bima (kabla ya VAT) kama mafuta kupitia vituo vya Oryx nchi nzima.
“Baada ya kulipia bima, aidha kupitia tawi la Benki, CRDB Wakala, au SimBanking, mbali ya mteja kupokea ujumbe wa sera yake ya bima, vilevile atapokea ujumbe wenye nambari ya zawadi ambayo ataitumia kujaza mafuta katika vituo vya Oryx,” aliongezea.

Taratibu za usalama zinaonyesha ni sharti la lazima kwa vyombo vya moto kuwa na bima kabla ya kuruhusiwa kuingia barabarani. Majaliwa anasema jamii inapaswa kuchukulia kwa umuhimu huduma hiya ya bima kujikinga na majanga ya ajali za barabarani.

Majaliwa alisema kampeni hiyo pia inalenga katika kusaidia malengo ya Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha ya kuongeza ujumuishi wa Watanzania katika huduma za bima kufikia asilimia 50 ifikapo mwaka 2030.
Katika kuhakikisha kuwa kampeni hiyo inakuwa na mafanikio, Benki ya CRDB imeandaa Tamasha la Elimu ya Bima ya Vyombo vya Moto litakalofanyika Viwanja vya Posta, Kijitonyama, siku ya  Jumamosi tarehe 17 Septemba 2022.

Tamasha hilo linakusudia kuwaleta pamoja wadau mbalimbali wa vyombo vya moto; kampuni za bima, gereji, maduka ya vifaa, na Mamlaka ya Usimamizi wa Bima (TIRA), Msuluhishi wa Migogoro ya Bima, na Jeshi la Polisi.
Meneja Uendeshaji Huduma za Bima Benki ya CRDB, Tumaini Frank aliwakaribisha wamiliki wa vyombo vya moto kushiriki katika tamasha hilo ili kupata elimu, lakini pia kukutana na watoa huduma mbalimbali.

“Katika tamasha hilo pia kampuni za bima zitakuwa zikishughulikia madai ya wateja, hivyo hii ni nafasi muhimu kwa wale ambao wanamadai ambayo bado hayajafanyiwa kazi.” alisema Tumani.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad