HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, August 30, 2022

Waziri Dkt. Ashatu amewaasa wakulima kuacha kilimo cha Mazoea na kuanza kilimobiashara

Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Dkt.Ashatu Kijaji akizungmza leo Agosti 30, 2022 wakati wa mkutano wa maandalizi ya Mkutano mkuu utakaofanyika Nchini Rwanda wa wadau wa kilimo na biashara Septemba 5-9,2022.
Makamu wa Rais wa Alliance for a Green Revolution in Africa (AGRA), Apollos Nwafor akizungumza wakati wa mkutano wa wadau wa kilimobiashara jijini Dar es Salaam leo Agosti 30, 2022.

KUELEKEA Mkutano wa Afrika wa masuala ya Kilimobiashara utakaofanyika nchini Rwanda Septemba 5-9,2022 Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Dkt.Ashatu Kijaji amewaasa wakulima kuacha kilimo cha Mazoea na kuanza kilimobiashara.

Ameyasema hayo wakati wa kufungua mkutano Uwekezaji katika kilimobiashara ulifanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) Dar es Salaam jijini Dar es Salaam leo Agosti 30,2022.

"Kilimo ni ajira, kilimo ndiko watanzania wengi wanakoajiriwa na ndiko ambako fursa nyingi zilizopo sasa za uwekezaji wa kilimo.

Tanzania tunamaeneo mengi ya kilimo tulime, tuuze na tuihudumie Afrika na dunia kwa mazao kutoka Tanzania." Amesema Dkt. Ashatu

Amesema serikali imeanza kuwaandaa wawekezaji katika sekta ya kilimo na biashara ili kujiandaa na biashara za mazao ya kilimo.

Amesema Serikali imewekeza fedha nyingi za kwenda kujenga miundombinu ya umwagiliaji katika maeneo mbalimbali ili vijana wa kitanzania waweze kulima kilimo cha kibiashara.

Akizungumzia kuhusiana na usalama wa Chakula Dkt. Ashatu amesema kuwa watanzania tunatakiwa kuhakikisha nchi inakuwa na usalama wa chakula pamoja na dunia kwa kuwepo na chakula kingi kutoka hapa nchini.

Kwa upande wa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), John Mnali amesema TIC wanawahamasisha wawekezaji kutoka nchi mbalimbali kuja kuwekeza nchini katika Sekta ya kilimo kwani Tanzania ina ardhi ya kutosha.

Amesema kuwa watanzania wanatakiwa kuongeza thamani ya mazao ya Uvuvi na mbegu za Mafuta na mazao ya bustani na matunda.

Licha ya hayo Mnali amewakaribisha wawekezaji kuja kuongeza thamani ya Mazao ya kilimo hapa nchini.

Mkurugenzi wa Sera na Mipango kutoka Wizara ya Kilimo, Obadia Nyagilo amesema wizara hiyo inahakikisha inaweka mifumo katika uzalishaji wa mazao ya chakula na mazao ambayo yanahitajika zaidi.

Akitolea mfano wa mazao ambayo yanahitajika zaidi amesema ni Alizeti na Parachichi ambayo yanaweza kuzalisha Mafuta.

Hata hivyo Nyagilo amewahamasisha watanzania kuwekeza kwenye kilimo cha Alizeti ili kuwahikisha mahitaji ya mafuta kula yanayohitajika nchini yanakwisha na kupunguza kuagiza kutoka nje ya nchi.

Nyagilo amesema kuwa wizara wanaendelea kufungua masoko ili kuhakikisha kwamba soko la Parachichi linakuwa kubwa.

"Mikakati yetu ni kuhakikisha kuwa zao la Parachichi linatangaza Tanzania Zaidi, kwa Upande wa Alizeti tunahakikisha kwamba kilimo cha alizeti kinaongezeka ili kupunguza upungufu wa mafuta kula nchini na kuacha kuagiza nchi nyingine."Amesema Nyagilo

Mkutano Mkuu Utakaofanyika nchini Rwanda Septemba 5-9, 2022 utajumuisha wawekezaji na taasisi za fedha kutoka nchi mbalimbali za Afrika kwa lengo la kutafuta wawekezaji wengi waweze kuwekeza katika nchi mbalimbali za Afrika kwenye Sekta ya kilimo na biashara pamoja na kuongeza thamani ya mazao ya kilimo na uvuvi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad