HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, July 6, 2022

MIGONGANO YA JAMII YA WAFUGAJI KWENYE CHANJO YA UVIKO-19 NA DAWA ZA ASILI

 Na Joseph Lyimo

MARA nyingi baadhi ya jamii ya wafugaji wa Wilaya ya Kiteto na Simanjiro Mkoani Manyara, pindi wakiugua huwa wanatumia dawa mbalimbali za asili ikiwemo Loduwa na Ndimwai katika kupata tiba.

Mwaka 2020 maambukizi ya UVIKO-19 yalipoingia nchini jamii ya wafugaji iligawanyika katika kushiriki kupata chanjo ya UVIKO-19 ili kupambana na virusi hivyo, huku wengine wakitumia dawa za asili na wengine wakishiriki kupata chanjo hiyo.

Hata hivyo, kutokana na elimu kuwafikia wengi wao na Serikali kujenga zahanati, vituo vya afya na hospitali karibu na makazi yao, hivi sasa wengi wao wanapata huduma za afya za kitaalamu.

Mkazi wa kata ya Orkesumet Wilayani Simanjiro, Elias Mollel anasema kwamba mara baada ya UVIKO-19 kuwa tishio, jamii mbalimbali za kifugaji, ziligawanyika katika kupata chanjo na kuendelea kutumia dawa za asili.

Mollel anaeleza kuwa awali baadhi ya jamii ya wafugaji walikuwa wanatumia dawa za asili na kuhofia kupata chanjo ya UVIKO-19 iliyokuwa inatolewa na wataalam wa afya ila baada ya kuona hakuna mabadiliko chanya na watu wanakufa wakaanza kuchanjwa.

“Ulipita upepo fulani hapa Orkesumet na watu wakawa wanakufa kwa UVIKO-19 ikabidi watu wachanje na wengi wao waliopata maambukizo hawakufa kutokana na chanjo kuwasaidia hivyo wakaiamini chanjo hiyo,” anasema.

Mkazi wa kijiji cha Loondrekes, Kata ya Kitwai, Wilayani Simanjiro, Michael Loishiye anasema awali kulikuwa na dhana potofu kwa jamii ya wafugaji kulishwa maneno potofu kuwa chanjo ya UVIKO-19 ina madhara hivyo watumie dawa za asili katika kujikinga.

“Mara baada ya kutokea vifo kwa baadhi ya waliokuwa viongozi maarufu kwenye wilaya ya Simanjiro kufa kutokana na tatizo hilo la kupumua ikawabidi wafugaji wabadili dhana potofu waliyokuwa nayo awali na kukubali kuchanjwa,” anasema Loishiye.

Mmoja kati ya viongozi wa kimila wa jamii ya wafugaji wa Wilaya ya Kiteto, Laigwanani Alaice Olengitambi anasema japokuwa wafugaji walikuwa wanatumia dawa za asili suala la kuchanja walilijadili baada ya kupata muongozo wa wataalam wa afya hivyo wao hawakupinga chanjo.

“Tulikuwa tunawaeleza kuwa wataalam wa afya wametupa elimu juu ya chanjo ya UVIKO-19 kuwa haina madhara na itakuwa inatolewa kwa hiyari hivyo jamii yenyewe itaamua kama watachanja au wataacha na kuendelea kupata dawa za asili ili kujikinga na UVIKO-19,” anasema Laigwanani Olengitambi.

Anasema suala hilo lilibaki kwenye mgawanyiko kwani baadhi yao walikuwa wanapata chanjo ya UVIKO-19 na wengine wakaendelea na dawa za asili ila hakuna kundi lilikuwa linatangaza kwani ni hiyari ya mtu kuchanja.

Mchungaji John Saning’o wa Kanisa la Kilakuno akizungumzia juu ya jamii ya wafugaji kupata chanjo ya UVIKO-19 anaeleza kuwa yeye anahudumu kwenye makanisa 37 ya eneo hilo na alikuwa akiwaeleza waumini wa makanisa hayo kuwa chanjo ni hiyari.

Mchungaji Saning’o anaongeza kwamba wao ni wachungaji wanaotoa elimu ya kiroho na elimu ya kimwili kwa kutangaza mambo ya Mungu na mambo ya serikali kwa waumini wao.

Anasema waliwaeleza waumini kuwa Kanisa halibagui kwani kupata chango ya UVIKO-19 ni hiyari hivyo atakayepata chanjo ni sawa na atakayegoma kuchanja ni suala binafsi kwani wenyewe hawaangali hayo.

“Muumini akikubali kuchanjwa hatafukuzwa wala kutengwa kanisani na asiyepata chanjo hatatengwa hivyo hakutakuwepo utaratibu wa kumuuliza muumini endapo amepatiwa chanjo au laa,” anaeleza Mchungaji Saning’o.

Mganga mkuu wa halmashauri ya Wilaya ya Kiteto, Dk Malkiadi Mbota anasema kuwa hivi sasa jamii ya wafugaji wa eneo hilo wamepata elimu na wanashiriki kupata chanjo ya UVIKO-19 kwenye vituo vilivyowekwa.

“Mwitiko kwa jamii ya wafugaji kupata chanjo ya UVIKO-19 hivi sasa ni mkubwa kwani awali walidhani ni bora watumie dawa za asili ila elimu ilipowafikia na wakaona hakuna madhara kwenye chanjo hivyo wanashiriki kuchanja kwa sasa,” anasema Dk Mbota.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad