HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, June 15, 2022

MAHERA AHIMIZA WATANZANIA KUHESABIWA

 

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Dkt. Wilson Mahera Charles.

WATANZANIA wametakiwa kuwa tayari kushiriki kikamilifu zoezi la kuhesabiwa wakati wa sensa ya watu na makazi itakayofanyika tarehe 23 agosti, 2022, nchini kote.

Wito huo umetolewa jana na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Dkt. Wilson Mahera Charles ofisini kwake jijini Dodoma.

Amesema zoezi la Sensa ya watu na makazi ni muhimu kwa maendeleo ya nchi kwani hata Tume ya Taifa ya Uchaguzi hutegemea takwimu za sensa kukadiria idadi ya wapiga kura wapya watakaoandikishwa pamoja na waliopoteza sifa za kuandikishwa kama vile waliofariki.

“Kimsingi wapiga kura au shughuli za uchaguzi kwa ujumla zina uhusiano mkubwa na takwimu zitokanazo na sensa, kwani katika sensa ndipo Tume inaweza kubainisha idadi ya watu itakayowaandikisha katika daftari la kudumu la mpiga kura,”amesema Dkt. Mahera na kuongeza:

“Nawahimiza watanzania kujitokeza kuhesabiwa kwenye sensa ya watu na makazi mwaka huu na kila mmoja kumhamasisha mwenzake kuhesabiwa.”


Dkt Mahera amesisitiza kuwa ili Tume iweze kufanya shughuli zake vizuri ni lazima ipate takwimu sahihi za watu, makazi na kutambua makundi maalum ambayo ni ya wanawake, wazee, vijana na watu wenye ulemavu.

Mkurugenzi wa Uchaguzi ameongeza kuwa kutokana na sensa ya mwaka huu kufanyika kwa kutumia teknolojia ya kisasa ambayo itawezesha kutambua idadi ya majengo ya umma na makazi ya watu, Tume inatarajia kutumia takwimu hizo, kuweka vituo vya uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura.

“Sensa ya mwaka huu itafanyika kidijiti na itaweza kubainisha idadi ya majengo ya umma ambayo sisi huyatumia kuweka vituo vya kujiandikisha, lakini pia itatusaidia pia kuweka vituo hivyo kwa mujibu wa anuani za makazi ambazo pia sensa inakwenda kuzitambua rasmi,” amesema Dkt Mahera.

Pia Dkt Mahera amesema Tume imekua ikipanga mipango yake kwa takwimu kuanzia ngazi ya kata lakini sasa kwa kuwa sensa inakwenda kuweka kumbukumbu hadi ngazi ya kitongoji, Tume itaweza kupanga mipango yake kwa urahisi zaidi na matumizi ya teknolojia katika uchaguzi yataongezeka.

Sensa ya watu na makazi hufanyika kila baada ya miaka 10 na mara ya mwisho Sensa hiyo ilifanyika mwaka 2012 ambapo watanzania milioni 44,929 walihesabiwa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad