Na Mwandishi Maalum – Chalinze, Pwani
Wananchi
437 wamefanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo na kisukari ambapo
asilimia 60 wamekutwa na tatizo la shinikizo la juu la damu (Presha) na
asilimia 20 ya waliokutwa na tatizo hilo tayari walishapata madhara ya
shinikizo la juu la damu ikiwa ni pamoja na moyo kutokufanya kazi vizuri
na kutanuka kwa misuli ya damu ya moyo.
Wananchi
wengine walikutwa na matatizo ya matundu kwenye moyo, mishipa ya damu
ya moyo kutokukaa katika mpangilio wake, matatizo kwenye vyumba vya moyo
na mishipa ya damu ya moyo kushindwa kupitisha damu vizuri.
Hayo
yamesemwa jana na daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) Peter Kisenge wakati wa kufanya tathimini ya
zoezi la upimaji wa magonjwa ya moyo na kisukari lililofanyika katika
hospitali ya Halmashauri ya Chalinze iliyopo Msoga wilayani Bagamoyo.
Dkt.
Kisenge ambaye pia ni mkuu wa kitengo cha mafunzo na utafiti wa Taasisi
hiyo alisema wagonjwa 27 walikutwa na matatizo ya moyo yaliyohitaji
uchunguzi na matibabu ya kibingwa na hivyo kupewa rufaa ya kwenda
kutibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete.
“Katika
upimaji huu tulifanya upimaji kwa watoto 22 ambapo watatu kati yao
walikutwa na matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo ambayo ni matundu na
mishipa ya damu ya moyo kutokuwa katika mpangilio wake wa kawaida,
watoto hawa tumewapa rufaa ya kuja kufanyiwa kufanyiwa uchunguzi zaidi
na kutibiwa katika Taasisi yetu”,.
“Zoezi
la upimaji limeenda vizuri mwitikio ni mkubwa wananchi wamekuja kwa
wingi na wamefurahia kupata matibabu kutoka kwa wataalamu wetu. Kwa kuwa
tatizo la shinikizo la juu la damu ni kubwa nawashauri wananchi waepuke
uvutaji wa sigara, unywaji wa pombe uliopitiliza na kutokula vyakula
vyenye mafuta mengi pia wazingatie lishe bora na ufanyaji wa mazoezi kwa
kufanya hivi wataepuka kupata magonjwa ya moyo”, alisema Dkt. Kisenge.
Dkt.
Kisenge alisema Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete inaunga mkono jitihada
za Serikali za kuhakikisha wananchi wanafikiwa na huduma za matibabu ya
kibingwa kwa kuwafuata wananchi mahali walipo kwa ajili ya kutoa huduma
za upimaji wa magonjwa ya moyo na kisukari bila malipo yoyote yale kwa
kufanya hivi wananchi wengi wataweza kufikiwa na huduma za matibabu ya
kibingwa ya magonjwa hayo kwa haraka zaidi.
Naye
Mganga mkuu wa Halmashauri ya Chalinze Dkt. Allen Mlekwa aliwashukuru
wataalamu waliotoa huduma za upimaji na matibabu kwa wananchi na kusema
upimaji huo ulihusisha madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa JKCI
pamoja na wenzao wa Hospitali ya Msoga.
Dkt.
Mlekwa alisema waliokutwa na matatizo ya moyo wengine walikuwa na
kliniki katika hospitali mbalimbali na walikuwa wanatumia dawa lakini
waliacha kutokana na sababu mbalimbali na baada ya kufanyiwa vipimo vya
moyo wamekutwa mioyo yao imetanuka na wengine wamekutwa na ugonjwa sugu
wa kisukari. Baadhi yao hawakuwa wanafahamu kabisa kuwa na tatizo la
moyo na hivyo waliwaanzishia dawa za kutumia.
“Kuwepo
kwa zoezi hili la upimaji kumetufanya tufahamu kunatatizo kubwa la watu
wenye matatizo ya moyo na kisukari hivyo basi nasi tumejipanga
kuboresha kliniki yetu ya moyo na kisukari iliyopo katika Hospitali ya
Msoga kwa siku ya alhamisi ili wagonjwa waliokuwa wanakwenda kutibiwa
Hospitali za Tumbi, Amana, Mwananyamala na Muhimbili waje kutibiwa
hapa”,.
“Kwa
kuwa tuna mashine za kupima vipimo vya kuangalia jinsi moyo unavyofanya
kazi (Echocardiography – ECHO) na kuchunguza mfumo wa umeme wa moyo
(Electrocardiography - ECG) tutawafanyia wagonjwa wenye shida ya moyo
vipimo hivi hapa hapa na kama tutawakuta na matatizo makubwa tutawarufaa
kwenda kutibiwa katika Hospitali kubwa zaidi”,.
“Wananchi
wengine wametoka kilomita zaidi ya 100 karibu kabisa na Tanga na
Mvumero wamekuja hapa kwa ajili ya kufuata huduma hii ya upimaji,
tutajipanga ili tuweze kufanya mobile kliniki za kwenda kutoa huduma za
upimaji katika vituo vya afya vya Msata, Kibindu, Lugoba na Miono kwa
kufanya hivi wananchi wengi watafikiwa na huduma za matibabu ya moyo na
kisukari”, alisema Dkt. Mlekwa.
Kwa
upande wa wananchi waliopata huduma hiyo walishukuru kwa huduma ya
uchunguzi na matibabu ya bila malipo waliyoipata na kusema
imewapunguzia gharama ya kusafiri na kuwafuata wataalamu Dar es Salaam
pamoja na kulipia matibabu hayo.
Fredrin
Ikumbera mkazi wa Lugoba alisema alipima vipimo na kukutwa moyo uko
sawa lakini amekutwa na shida ya presha amepewada dawa za kutumia pamoja
na ushauri wa lishe bora na kuambiwa apunguze matumizi ya vyakula vya
wanga pamoja kupunguza kunywa pombe kwani ni hatari kwa afya ya moyo
wake.
“Nilikuwa
ninawasiwasi kuhusu moyo wangu kwani mazingira niliyokuwa naishi
hayakuwa salama. Ninawasihi wananchi wenzangu kutumia nafasi za upimaji
pindi zinapotokea kwa kwenda kupima afya zao pia kwa upande wa Serikali
iendelee kuhakikisha wananchi walioko vijijini wanapata huduma za
matibabu ya kibingwa kwani kutokana na mazingira yao ni vigumu kufikiwa
na huduma hizi”, alisema Ikumbera.
Afisa kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Aliston Jovin
akiwagawia vipeperushi vinavyoelezea huduma za matibabu zinazotolewa na
JKCI wananchi waliofika katika Hospitali ya Halmashauri ya Chalinze
iliyopo Msoga kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo
uliofanywa na wataalam wa moyo kutoka JKCI katika Halmashauri hiyo
iliyopo wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.Afisa
Uuguzi kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Rahabu Tamba
akimpima urefu na uzito mwananchi aliyefika katika Hospitali ya
Halmshauri ya Chalinze iliyopo Msoga wilayani Bagamoyo kwa ajili ya
kufanya uchunguzi wa magonjwa ya moyo uliokua ukifanywa na wataalam wa
moyo kutoka JKCI kwa wananchi wa Chalinze. Daktari
kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Magreth Ng’ondya
akimuelezea mwananchi umuhimu wa kutumia dawa za shinikizo la damu
wakati wa upimaji wa magonjwa ya moyo, kisukari na shinikizo la damu
uliofanywa na wataalam wa moyo kutoka taasisi hiyo kwa wananchi wa
Chalinze kwa siku mbili na kumalizika jana katika Hospitali ya
Halmashauri ya Chalinze iliyopo msoga Wilayani Bagamoyo.
Daktari kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Janeth Mmari akisoma majibu ya vipimo vilivyofanywa na mwananchi wa Chalinze baada ya kufanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo na kisukari wakati wa upimaji uliyofanywa na wataalam wa moyo kutoka JKCI kwa wananchi wa Halmashauri ya Chalinze iliyopo wilayani Bagamoyo.
Mkuu wa Kitengo cha Mafunzo na Tafiti kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kiwetwe (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimpima mwananchi wa Halmashauri ya Chalinze kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echo-Cardiograph) wakati wa upimaji uliofanywa na wataalam wa moyo kutoka JKCI kwa wananchi hao siku mbili katika Hospitali ya halmashauri hiyo iliyopo Msoga wilayani Bagamoyo.Wataalam wa moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa upimaji maalum uliofanyika kwa siku mbili kwa wananchi wa Chalinze kuchunguza magonjwa ya moyo, kisukari na shinikizo la damu katika Hospitali ya Halmashauri ya Chalinze iliyopo msoga wilayani Bagamoyo. Picha na JKCI
Daktari kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Janeth Mmari akisoma majibu ya vipimo vilivyofanywa na mwananchi wa Chalinze baada ya kufanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo na kisukari wakati wa upimaji uliyofanywa na wataalam wa moyo kutoka JKCI kwa wananchi wa Halmashauri ya Chalinze iliyopo wilayani Bagamoyo.
Mkuu wa Kitengo cha Mafunzo na Tafiti kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kiwetwe (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimpima mwananchi wa Halmashauri ya Chalinze kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echo-Cardiograph) wakati wa upimaji uliofanywa na wataalam wa moyo kutoka JKCI kwa wananchi hao siku mbili katika Hospitali ya halmashauri hiyo iliyopo Msoga wilayani Bagamoyo.Wataalam wa moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa upimaji maalum uliofanyika kwa siku mbili kwa wananchi wa Chalinze kuchunguza magonjwa ya moyo, kisukari na shinikizo la damu katika Hospitali ya Halmashauri ya Chalinze iliyopo msoga wilayani Bagamoyo. Picha na JKCI
No comments:
Post a Comment