HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, May 29, 2022

MWANA FA ANOGESHA USIKU WA MKESHA WA MWENGE

 

Na Mashala Mhando, Muheza
MBUNGE wa jimbo la Muheza, Hamis Mwinjuma maarufu MwanaFA, jana alinogesha usiku wa mkesha wa Mwenge wa Uhuru kwa kuimba nyimbo zake mbalimbali zilizompa umaarufu kwenye muziki wa Bongo Fleva.

Mbunge huyo ambaye alikonga nyoyo za vijana na watu wengine waliokuwa kwenye mkesha huo uliohidhuriwa na viongozi mbalimbali wa wilaya baada ya kumaliza mbio zake katika wilaya hiyo.
Nyimbo alizoimba na kuwaacha hoi, mamia ya watu waliojazana kwenye uwanja wa Jitegemee mjini hapa ni pamoja na wimbo 'Kwa Mungu hakuna majungu, wee Endelee tu' na 'Asante kwa Kuja'.

Nyingine ambazo hapan'shaka zilivuya hisia za watu waliojazana kwenye uwanja huo ni pamoja na wimbo 'Binadamu Kukunja Goti' alioamshirikisha AY, 'Mfalme' alioimba na G Nako pamoja na wimbo mpya wa 'Gwiji Remix'.
Watu waliohudhuria mkesha huo, walisema amekomaa katika nyanja ya siasa pamoja na majukumu yake ya kuimba muziki.

"Kiukweli acha niwe mnafki, mbunge wetu anaupiga mwingi, bungeni anawasha moto kwa hoja zake za kisiasa kututetea wana-Muheza na leo hii ametupa burudani ya kutosha kabisa, hongera zake," alisema Ramadhani Sebwijo mkazi wa Kicheba Muheza.

Naye John Mdami mkazi wa Kerenge Muheza alisema kitendo cha mbunge wao kutoa burudani kunogesha mkesha wa Mwenge, kimesaidia kuongeza alama katika shamra shamra za mwenge huo.

"Hakika tumepata Mbunge, hapa ametupa burudani ya kufa mtu, juzi nimemsikia bungeni akichangia mjadala wa Wizara ya Ardhi, Nyumba Maendeleo ya Makazi, alitutetea sana kuhusu mashamba ya chai yaliyotelekezwa akaiomba serikali itupe tupate maeneo ya kulima," alisema Mdami na kuongeza,
"Tumechagua mbunge anayekidhi mahitaji yetu ya burudani, kisiasa na kijamii,".

Mkuu wa wilaya Halima Bulembo aliwakumbusha wananchi waliofika kwenye mkesha huo, kuhakikisha wanajitokeza kwa wingi katika zoezi la sensa ya watu na makazi itakayofanyika Agosti 23 mwaka huu.

"Pamoja na burudani mnayoipata kutoka kwa mbunge wenu msisahau ujumbe uliotolea na Kiongozi wa mbio za Mwenge mwaka huu Sahil Geraruma, mjitokeze kwenye sensa," alisema mkuu huyo wa wilaya.

Mwenge ulipitia na kuweka mawe ya msingi na kuzindua miradi ipatayo minane kwenye wilaya hiyo yenye thamani ya shilingi bilioni 1.7

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad