Na Mwandishi Wetu, Michuzi TV
WADAU
mbalimbali wakiwemo , viongozi na watu mashuhuri wamekutana kwenye
Kongamano maalumu ambalo limeandaliwa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa
lengo la kuenzi miaka 100 ya Mwalimu Julius Nyerere hasa katika
kutambua mchango wake katika masuala kadhaa yakiwemo ya kiuchumi.
Wakizungumza
wakati wa Kongamano hilo lililofanyika Ukumbi wa BoT ,wadau mbalimbali
wamepata nafasi ya kumuelezea Mwalim Nyerere na harakati zake katika
kukuza na kuimarisha uchumi wa Tanzania kupitia sekta ya fedha.
Gavana
wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Profesa Florens Luwoga pamoja na mambo
mengine ameeleza kwa kifupi sababu za kuandaa Kongamano hilo ambapo
amesema katika kufanikisha majadiliano katika kongamano hilo waliamua
kushirikiana na taasisi nyingine ikiwemo waandishi wa vitabu vya Mwalimu
Nyerere.
“Kwa sababu kwanza wakati Rais Samia Suluhu Hassan
anavizindua vitabu vya Mwalimu Nyerere kule Kibaha, hivi vitabu vilikuwa
havijatambulishwa na wananchi wengi walikuwa wanaona tu yale majuzuu
matatu lakini kwa kawaida unapoona majuzuu namna ile mtu wa kawaida
inampa uvuvi wa kununua asome
“Lakini ukivitambulisha wananchi
wanajua nini kilichomo na kuna nini kinaweza kupatikana kwenye hicho
kitabu, hivyo benki kuu imeona iandae huu mjadala katika moja ya kumuezi
Mwalimu Nyerere.
“Benki kuu kwa namna ya pekee imekuwa
ikihakikisha inamuenzi Mwalimu Nyerere kwanza kwa kuweka mfuko wa
ufadhili wa masomo kwa ajili ya kuendelea kutoa mafunzo kwa vijana ambao
wengi wana uwezo na wanaweza kuendelea kuihudumia nchi hii kupitia
Benki Kuu ya Tanzania au kupitia taasisi nyingine za umma.
“Kupitia
ufadhili huo vijana wetu wa kitanzania wanasoma fani mbalimbali
zikiwemo za kiuchumi, sayansi na fani nyingine .Hivyo kupitia kongamano
hili imekuwa nafasi nzuri kuujulisha umma kuhusu Mfuko wa Ufadhili wa
masomo wa Mwalimu Nyerere ambao uko hapa Benki Kuu, lakini kama ratiba
ilivyo litatolewa tamko hukusu mfuko huu,”amesema Gavana .
Ameongeza
wakati wanatambulisha vitabu vya aina ya pekee kwa jinsi
vinavyomuelezea Mwalimu Nyerere kwa nafasi yake kama Kiongozi na nini
alipitia na jinsi gani aliweza kuhakikisha nchi inaelekea kwenye malengo
ambayo Mwalimu alikuwa nayo.
Kuhusu mahusiano kati ya Mwalimu
Nyerere na BoT, Gavana Luwoga amesema huwezi kuizungumzia Benki Kuu ya
Tanzania bila Mwalimu kwa sababu kabla ya benki hiyo kuanzishwa masuala
yote yaliyohusu fedha yalikuwa chini ya Bodi ya Sarafu ya Afrika
Mashariki.
“Lakini baada ya kupata uhuru Mwalimu aliona umuhimu
wa kuhakikisha kuwa na Benki Kuu ya Tanzania ili Serikali iwe na uwezo
mkubwa wa kuendesha uchumi wake. Huwezi kuendesha uchumi bila kuwa na
Sera yako ya fedha na kutoa sarafu yako mwenyewe.
“Kwa hiyo
Mwalimu hata kabla ya Uhuru mazungumzo yalishaanzishwa kwamba tukipata
uhuru tuwe na Benki Kuu yetu .Utashi wa kiongozi unahitajika vinginevyo
unaweza kuwa na Benki Kuu ambayo haina uhuru wa kusaidia katika
kuimarisha ama kuwa na uchumi imara.
“Hivyo kuanzia mwaka 1965
wakati inaanzishwa Benki Kuu majukumu yake yalipewa kwa kushirikisha
uongozi wa nchi na baada ya pale kila sheria ilipobadilika ilikuwa ni
kuongeza majukumu na Serikali kuheshimu ule uhuru wa Benki Kuu.
“Ili
kuhakikisha uchumi unaimarika, sarafu yetu inaimarika, thamani ya
fedha, uhimilivu wa bei, riba na mambo yote hayo Benki Kuu inatakiwa
kuyatekeleza kwa weledi bila muingiliano mkubwa na Serikali.Hivyo huwezi
kuizungumzia Benki Kuu bila kuzungumzia maono ya kiongozi aliyeanzisha
benki hii,”amesisitiza.
Kwa upande wake Profesa Issa Shivjj
amesema uamuzi wa BoT kuandaa mdahalo kupitia Kongamano hilo la kuenzi
miaka 100 ya Mwalimu Nyerere ni mwanzo mzuri sana kwani huwezi
kutengenisha sekta ta fedha na mambo mengine ya hali ya nchi.
“Na
huwezi kutenganisha sekta ya fedha bila kujua histori , na kongamano la
leo ingawa limejikita katika historia ya Mwalimu lakini ni muhimu kwani
linafundisha mambo muhimu. Kama nilivyochangia kwenye mchango wangu
kuna mambo katika sekta ya fedha lazima tuyafahamu kwa mfano
tulipotaifisha benki wakati ule leo tunahitaji kujua ilivyotokea na
benki kutoka nje walivyopambana hadi wakasalimu amri.
Hata hivyo
amesema kuwa unaposoma vitabu vya Mwalimu Nyerere kwa sehemu kubwa
unaona wananchi na watu wa Tanzania walivyopambana wakiongozwa na
Mwalimu Nyerere , kwa hiyo mapambano bado yanaendelea.
“Kwa
upande wangu nawasihi vijana wasome hiyo historia ili wasione nchi
wanayoitaka itapatikana kama zawadi bali itapatikana kwa mapambano na
hii naaminisha sio watu wengi tutafaidika lakini lazima tupambane ili
vizazi vijavyo vifaidike kwa kuwa na nchi wanayoitaka,”amesema
Gavana
wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Prof. Florens Luoga akitazama na
kununua baadhi machapisho ya vitabu mbalimbali vya Mwalimu Nyerere baada
ya kufungua Kongamano la Kumbukizi ya Miaka 100 ya Kuzaliwa Hayati Baba
wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere katika mtazamo wa kiuchumi pamoja na
uchambuzi wa vitabu lililofanyika kwenye ukumbi wa benki hiyo jana Mei
5,2022 jijini Dar es Salaam. Kongamano hilo liliandaliwa na Benki Kuu ya
Tanzania (BoT)kwa kushirikiana na taasisi nyingine ikiwemo Chuo Kikuu
cha Dar es Salaam,Taasisi ya Mkuki na Nyota na nyinginezo.Katika
Kongamano hilo mada mbalimbali zilijadiliwa ikiwemo vitabu vitatu
vilivyoandika wasifu Mwalimu Nyerere, vilivyozinduliwa hivi karibuni na
Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. PICHA ZOTE NA MICHUZI JR-MMG
Baadhi ya Wadau mbalimbali wakiangalia na kununua machapisho ya vitabu mbalimbali vya Mwalimu Nyerere
Gavana
wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Profesa Florens Luoga akizungumza na
Wadau mbalimbali waliojitokeza kushiriki kongamano la kumbukizi ya miaka
100 ya Mwalimu Nyerere iliyoandaliwa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa
kushirikiana na Taaisisi mbalimbli jana Mei 5,2022 jijini Dar es
Salaam
Gavana
wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Profesa Florens Luoga akizungumza wakati
akifungua kongamano la kumbukizi ya miaka 100 ya Mwalimu Nyerere
iliyoandaliwa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa kushirikiana na Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) jana Mei 5,2022 jijini Dar es Salaam
kwenye ukumbi wa BoT.
Prof.
Saida Yahya-Othman akimuelezea Hayati Mwalimu Nyerere kwenye Kogaamano
hilo, anasema Baba wa Taifa alikuwa muasi tokea akiwa mdogo ambapo
alijikitia kupinga ukandamizaji na dhuluma zilizokuwa zimewekwa na
wakoloni katika maeneo mbalimbali ya shule,makanisani na
vyuoni.Amefafanua kuwa, uasi ambao aliufanya Hayati Baba wa Taifa
Mwalimu Nyerere haukuwa kwa manufaa yake, bali kwa manufaa ya jamii na
ustawi bora wa Taifa likiwemo Bara la Afrika kwa ujumla.
Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Mkuki na Nyota, Walter Bgoyaakieleza
alivyobahatika kufanya kazi katika miaka miwili ya mwisho wa maisha yake
ya Baba wa Taifa, anasema Mwalimu Nyerere alilipa kipaumbele suala la
utu, usawa na haki katika kukuza amani na utulivu nchini, kwa sababu
kusipozingatiwa kunaweza kuleta uvunjifu wa amani au vita katika Afrika.
Alisema kutokana na kuendelezwa maono ya Mwalimu Nyerere, Tanzania
imekuwa mahali salama na kimbilio la nchi rafiki za Afrika wakati
wanapopata shida kwao kama nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, na
nyinginezo.
Dkt. Ng’wanza Kamata kutoka chuo Kikuu cha Dar es Salaam akieleza mambo
mbalimbali aliyoyapitia Hayati Baba wa Taifa kwenye Kongamano la
Kumbukizi ya Miaka 100 ya Kuzaliwa Mwalimu Nyerere katika mtazamo wa
kiuchumi pamoja na uchambuzi wa vitabu lililofanyika kwenye ukumbi wa
benki hiyo jana Mei 5,2022 jijini Dar es Salaam. Kamata amesema kuwa,
Hayati Baba wa Taifa alipitia nyakati nyingi kabla na baada ya Uhuru na
kote huko alishinda."Mwalimu Nyerere alikuwa anapata upinzani mkubwa na
vitisho vingi. Wakati mwingine alijibu kwa ukali na alifanikiwa kushinda
kwa sababu alikuwa na uwezo wa kipekee,"amesema.
Sehemu
ya Meza Kuu, Kutoka kulia ni Prof. Saida Yahya-Othman,Gavana wa Benki
Kuu Prof Florens Luoga pamoja na Prof.Issa Shivji wakifuatilia mijadala
iliyokuwa ikiwasilishwa kwenye kongamano hilo.Wadau mbalimbali wakifuatilia kwa makini yaliyokuwa yakijiri kwenye Kongamano hilo .PICHA ZOTE NA MICHUZI JR-MMG
Friday, May 6, 2022

Home
HABARI
BoT YAENZI MIAKA 100 YA MWALIMU NYERERE KWA KUANDAA KONGAMANO MAALUM, WAGUSIA MFUKO WA UFADHILI WA MASOMO
BoT YAENZI MIAKA 100 YA MWALIMU NYERERE KWA KUANDAA KONGAMANO MAALUM, WAGUSIA MFUKO WA UFADHILI WA MASOMO
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment