HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, April 11, 2022

MAKUMBUSHO YA TAIFA KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA UJERUMANI KUHIFADHI MALIKALE

 Na Mwandishi Wetu

MAKUMBUSHO ya Taifa la Tanzania imesaini mikataba ya mashirikiano na taasisi mbili za Ujerumani kwa lengo la kuboresha uhifadhi wa Makumbusho na uhifadhi wa mali kale nchini.

Katika mikataba hiyo ya mashirikiano Serikali ya Ujerumani itatoa jumla ya Euro 201,130 kwa ajili ya kusaidia katika ukarabati wa jengo la King George V lililopo Makumbusho na Nyumba ya Utamaduni jijini Dar es Salaama na kuandaa onesho la historia ya Tanzania kwa pamoja ambalo litawekwa mjini Berlin Ujerumani na Tanzania.

Mkataba wa mashirikiano hayo imesainiwa jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa, Dkt. Noel Lwoga, Rais wa Kituo cha urithi wa Utamaduni cha Prussian, Ujerumani (Prussian Cultural Heritage Foundation), Prof Herman Partzinger na Mkurugenzi wa Humboldt Forum, Prof. Hartmut Dorgerch.

Utiaji sahihi wa Mikataba hiyo umeshuhudiwa na Waziri wa Nchi wa ujerumani anayeshughulikia Mambo ya Nje, Mhe. Kartja Kaul, Balozi wa Tanzania nchini Ujeruman, Dkt. Abdallah Posi na Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania, Mhe. Regina Hess.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa Makumbusho ya Taifa, Dkt. Noel Lwoga amesema kuwa sekta ya malikale inategemea sana utafiti ili kupata taarifa sahihi za mikusanyo mbalimbali, hivyo ushirikiano wa kiutafiti unasaidia kuweza kufanya tafiti za kisasa na kubadilishana utaalamu katika namna nzima ya uhifadhi thabiti na kutanua wigo wa vivutio vya kiutalii.

Mikataba hiyo inatokana na uhusiano wa muda mrefu wa kufanya kazi kati ya Makumbusho ya Taifa la Tanzania na Shirika la Ujerumani SPK (Stiftung PreuBischer Kulturbesitz) hivyo inawezesha taasisi hizo kufanya kazi pamoja.

Madhumuni ya maonyesho hayo katika historia ya Tanzania ni kuwasilisha historia tajiri na ya eneo la Tanzania ya leo kwa misingi ya vitu vilivyochaguliwa kutoka Afrika Mashariki katika Makumbusho ya Mila ya Ujerumani (SPK) pamoja na Makumbusho ya Taifa Tanzania (NMT).

Naye balozi wa Tanzania Nchini Ujerumani Dkt. Abdallah Posi ameeleza umuhimu wa Tanzania kuonesha ushirikiano na nchi mbalimbali zilizopiga hatua katika uhifadhi wa Malikale na utalii ili kuweza kujipatia maarifa na mbinu adhimu kutoka kwa wataalamu nchini humo kwa manufaa ya Taifa kwa ujumla.

“Katika mkataba huu wa ushirikiano na wadau mbalimbali kama Ujerumani wataanzania tunapaswa kushirikiana kwa umoja wetu ili kupata, kuendeleza na kukuza uelewa juu ya utafiti na uhifadhi sahahi wa Malikale nchini. Hii itatusaidia kutumia teknolojia za kisasa ili kuweza kufikia baadhi ya malikale zilizopo ndani na nje ya Tanzania” ameeleza Dkt. Posi

Kati ya mikataba iliyosainiwa ni pamoja na Mkataba wa ukarabati wa jengo la kihistoria linalotambulika kama jengo la ‘King George V’ ambapo Makumbusho ilianzia mnamo mwaka 1940. Mkataba wa ushirikiano wa utafiti na maonyesho unaohusisha mikusanyo mbalimbali ya kihistoria na kimila ambayo ipo Nchini Ujerumani na kufanya maonyesho nchini humo na Tanzania juu ya mikusanyo hiyo, na mkataba wa kuendesha programu mbalimbali za kuelimisha jamii kupitia semina na mikutano kwa kushirikiaana na Wajerumani.
Mkurugenzi wa Makumbusho ya Taifa, Dkt Noel Lwoga, kulia akibadilishana Nyaraka na Rais wa Kituo cha Urithi wa Utamaduni cha Prussiona, Prof Herman Parzinger baada ya kusaini mkataba wa ushirikiano.
Picha ya pamoja

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad